Ruto afichua ‘kusafirisha’ kampuni ya Tata Chemicals akiilaumu kwa kutonufaisha Wakenya
RAIS William Ruto amemshambulia vikali mwekezaji wa kimataifa, Tata Chemicals, eneo la Magadi, Kajiado, akisema kampuni hiyo imeshindwa kuwanufaisha Wakenya licha ya kufanya biashara nchini kwa zaidi ya miaka 100.
Rais alisema kampuni hiyo imekuwa ikisafirisha malighafi ya Kenya nje ya nchi badala ya kujenga viwanda vya kutengeneza vioo na kemikali nchini.
“Nimewaambia waondoke. Wameshindwa kujenga kiwanda cha vioo nchini. Wanasafirisha tu rasilimali zetu hadi nchi yao. Serikali italeta mwekezaji mpya kwa masharti mapya,” alisema.
Alisema serikali pia itafadhili usambazaji wa maji kwa wakazi wa Magadi, akisema maji ni miongoni mwa huduma ambazo Tata Chemicals imekuwa ikitoa kwa jamii.
Rais alimuomba Gavana wa Kajiado Joseph Lenku kumuunga mkono katika kuhakikisha kampuni hiyo inaondoka katika kaunti hiyo.
Kauli hiyo inajiri mwezi mmoja baada ya Wizara ya Madini na Uchumi wa Baharini kuamuru kampuni hiyo kusitisha shughuli za uchimbaji kutokana na madai ya kutofuata masharti ya kisheria.
Kesi kuhusu suala hilo bado iko katika Mahakama Kuu na itasikilizwa Oktoba 6, 2026.
Rais Ruto alikuwa Kajiado kuanza ziara ya siku tatu kukagua miradi ya maendeleo katika maeneo bunge matano.
Ziara hiyo pia imeonekana kama juhudi za kuimarisha uungwaji mkono wa chama cha UDA kuelekea uchaguzi wa 2027.
Rais aliahidi kukamilisha kiwanda cha kusindika nyanya cha Rombo chenye thamani ya Sh1.2 bilioni, ambacho kimekamilika kwa asilimia 70.
Alisema kiwanda hicho kitawasaidia wakulima wa nyanya kupata soko bora na kuongeza mapato yao.
Eneo la Rombo huzalisha takriban tani 70,000 za nyanya kwa mwaka.
Rais pia alitetea Hazina ya Michezo, Sanaa na Maendeleo ya Jamii (SASDF), akisema imewezesha ujenzi wa viwanja 32 nchini.
Aidha, aliwataka viongozi wa upinzani kukutana naye kwenye uchaguzi wa 2027 badala ya kutumia kauli mbiu za kisiasa.
“Tutakutana kwenye sanduku la kura,” alisema.
Tata Chemicals, zamani ikijulikana kama Magadi Soda, ni moja ya waajiri wakubwa katika sekta ya uchimbaji madini nchini.
Kampuni hiyo iko takriban kilomita 120 kusini-magharibi mwa Nairobi, karibu na Ziwa Magadi, eneo linalojulikana kwa madini ya chumvi aina ya trona.
Kampuni hiyo pia ni miongoni mwa wauzaji wakubwa wa bidhaa nje ya Kenya, ikichangia takriban asilimia sita ya mauzo ya nchi nje.
Kwa miaka mingi, Tata Chemicals imeendesha miradi ya kijamii katika afya, maji, elimu na uwezeshaji wa jamii.
Hata hivyo, imekuwa ikikabiliana na mzozo wa muda mrefu na Serikali ya Kaunti ya Kajiado kuhusu ushuru wa ardhi na malipo ya mrabaha wa madini.