Mwanamume ataka ukosefu wa nguvu za kiume utambuliwe kama ulemavu
MWANAUME mmoja Mkenya anataka matatizo kama vile ukosefu wa nguvu za kiume yatambuliwe kisheria kama ulemavu.
Katika ombi alilowasilisha Bungeni, Dkt Benson Kibore amesema tatizo la nguvu za kiume na ukosefu wa hamu ya kushiriki mapenzi, hali inayojulikana kama HSDD, linahitaji kushughulikiwa kupitia sheria na sera za afya.
Anasema matatizo haya, ambayo hapo awali yalihusishwa zaidi na wazee, sasa yanaonekana pia miongoni mwa vijana.
Dkt Kibore anarejelea utafiti wa 2026 uliofanywa Nairobi na kuchapishwa kwenye medRxiv, ambao ulionyesha kuwa asilimia 10.4 ya vijana waliofanyiwa utafiti walikuwa na tatizo la nguvu za kiume.
Wastani wa umri wao ulikuwa miaka 27.
“Kwa hivyo, ukosefu wa hamu ya ngono unaohusishwa na tatizo la nguvu za kiume si tatizo la wazee pekee bali ni hali inayowakumba vijana pia,” alisema katika ombi lake kwa Bunge la Kitaifa na Seneti.
Dkt Kibore pia anataka HSDD itambuliwe kama suala la afya ya umma ili wanaohitaji matibabu waweze kupata huduma hiyo.
Anasema matatizo ya ukosefu wa nguvu za kiume yanaweza kuathiri afya ya akili, ndoa, mahusiano na afya ya uzazi.
Katika ombi hilo la Julai, anataja kutoridhika katika ndoa, kutengana kihisia, msongo wa mawazo, kuvunjika kwa mahusiano na ukosefu wa uaminifu katika ndoa kama baadhi ya madhara yanayoweza kuwapata waathiriwa.
Iwapo Bunge litaidhinisha pendekezo hilo, sheria kadhaa zitalazimika kufanyiwa marekebisho, zikiwemo Sheria ya Watu Wenye Ulemavu na Sheria ya Bima ya Afya ya Jamii (SHA).
Mabadiliko hayo yanaweza kuwezesha watu wenye matatizo sugu ya kingono yaliyothibitishwa kutambuliwa chini ya vigezo vya ulemavu.
Pia, huduma kama uchunguzi, ushauri nasaha na matibabu zinaweza kugharamiwa kupitia Mamlaka ya Afya ya Jamii (SHA).
Dkt Kibore anasema gharama ya matibabu imekuwa kikwazo kwa Wakenya wengi. Wagonjwa wengi hulipia huduma kutoka mifukoni mwao, huku ada za mashauriano katika hospitali za kibinafsi zikianzia takriban Sh5,000 na gharama ya matibabu kufikia mamia ya maelfu ya shilingi.
Upasuaji wa uume, unapohitajika, unaweza kugharimu zaidi ya Sh1 milioni.
Dkt Kibore pia anasema tatizo hilo linaweza kusababisha mtu kukosa kujiamini na kuathiri afya ya akili.
Anarejelea pia utafiti mwingine unaoonyesha uhusiano kati ya hamu ya kushiriki ngono na afya ya moyo.
Anasema kuwa kudumisha hamu nzuri ya ngono kunaweza kuwa na manufaa kwa afya ya moyo na mwili kwa ujumla.
Dkt Kibore anasema unyanyapaa unaohusishwa na matatizo ya kingono huwazuia wanaume na wanawake wengi kutafuta matibabu.
“Unyanyapaa unaozunguka matatizo ya kingono kwa wanaume na wanawake mara nyingi huwazuia kutafuta msaada, hivyo kuongeza muda wa mateso ndani ya familia,” alisema.