Siasa

Sheria dhaifu zachochea utovu wa nidhamu ndani ya vyama vya kisiasa

Na MOSES NYAMORI September 4th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

KATIKA mikutano ya kisiasa, ni kawaida kwa baadhi ya viongozi wa United Democratic Alliance (UDA) kumpigia debe Rais William Ruto ili achaguliwe tena mnamo Agosti 10, 2027.

Kisheria, viongozi hao bado ni wanachama wa vyama vilivyowapitisha katika uchaguzi wa 2022.

Lakini hadharani, wamehamia vyama vingine na sasa wanatafuta kuchaguliwa kupitia vyama hivyo.

Baadhi yao wamepewa nyadhifa za juu katika vyama vipya.

Hali hii imeongeza vurugu katika siasa za Kenya miezi 11 kabla ya uchaguzi mkuu wa 2027, huku vyama vikionekana kushindwa kuwachukulia hatua wanachama wanaokiuka kanuni.

Baadhi ya vyama havijaanzisha hata taratibu za kinidhamu dhidi ya viongozi hao, hali inayodhihirisha udhaifu katika utekelezaji wa sheria zao.

Mwanasheria wa Katiba Bobby Mkangi alisema mianya ya kisheria na kisiasa imechangia viongozi kuhama vyama kiholela.

“Vyama vyenyewe vina nidhamu kabla ya kutaka wanachama wao wafuate kanuni? Vyama vingi ni kama magari ya uchaguzi. Watu hujiunga navyo ili kushinda viti,” alisema.

Alisema vyama vingi havina misingi thabiti ya itikadi, ndiyo maana wapinzani huungana baada ya uchaguzi bila kuwashirikisha wanachama.

Katika Mlima Kenya, viongozi kadhaa waliochaguliwa kupitia UDA wamejiunga na Democracy for the Citizens Party (DCP) ya aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua.

Seneta wa Nyandarua, John Methu ametajwa kuwa Katibu Mkuu mteule wa DCP, ingawa bado ni mwanachama wa UDA.

Magavana Irungu Kang’ata na Kiarie Badilisha pia wamejiunga na DCP, pamoja na maseneta Joe Nyutu, Karungo Thang’wa na James Murang.

Mbunge wa Kiharu Ndindi Nyoro amejiunga na People’s Party of Kenya (PPK), huku Mbunge wa Nyali Mohammed Ali akijiunga na Wiper Patriotic Front ya Kalonzo Musyoka.

Ndani ya ODM, Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna anaongoza kundi la Linda Mwananchi katika mzozo wa uongozi na kiongozi wa chama Oburu Oginga.

Wanasiasa wengine wanaohusishwa na kundi hilo ni Gavana wa Siaya James Orengo, Seneta wa Vihiga Godfrey Osotsi na wabunge Babu Owino na Caroli Omondi.

Gavana wa Mombasa Abdullswamad Nassir, ambaye ni naibu kiongozi mwenza wa ODM, alisema ni vigumu kuwafukuza wanachama waasi kutokana na mchakato mrefu wa kisheria.

Alipendekeza marekebisho ya Sheria ya Vyama vya Kisiasa ili kurahisisha vyama kuwachukulia hatua wanachama wanaokiuka kanuni.

Hata hivyo, Mwenyekiti wa Bodi ya Kitaifa ya Uchaguzi ya UDA Anthony Mwaura alisema chama hicho kimechukua hatua dhidi ya baadhi ya waasi, akitaja kufukuzwa kwa Seneta mteule Gloria Orwoba.

Mzozo huo unaonyesha changamoto ambayo vyama vya kisiasa vimekuwa vikikabili kwa miaka mingi.

Majaribio ya ODM, Jubilee na ANC kuwafukuza viongozi walioasi yamewahi kuzuiwa na Mahakama au Mabaraza ya Migogoro ya Vyama vya Kisiasa, huku baadhi ya viongozi wakibaki madarakani hadi mwisho wa mihula yao.