Siasa

Wataalamu 12 waanza kuandaa manifesto ya UDA-ODM kuelekea 2027

Na JUSTUS OCHIENG August 30th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

KAMATI ya wataalamu walioteuliwa kuandaa mwongozo wa kisiasa na manifesto ya pamoja ya vyama vya UDA na ODM kuelekea Uchaguzi Mkuu wa 2027 imeanza kazi rasmi huku ikipanga kufanya mashauriano kitaifa yatakayohusisha wananchi kutoka maeneo mbalimbali nchini.

Mkurugenzi Mkuu wa UDA, Nicodemus Bore, ambaye ni mwanachama wa kamati hiyo alisema wataalamu hao tayari wamefanya mkutano wao wa kwanza na sasa wanajipanga katika makundi ya kiufundi ili kuanza kazi ya kuandaa msingi wa ushirikiano wa kisiasa kati ya Rais William Ruto na kiongozi wa ODM, Dkt Oburu Oginga.

“Tayari tumekutana na kufanya kikao chetu cha kwanza. Sasa tunaandaa mikutano mingine na kupanga jinsi ya kufanya kazi kupitia makundi ya kiufundi. Kazi imeanza rasmi,” alisema Bore.

Alisema wananchi wanapaswa kutarajia mashauriano makubwa kote nchini ili kuhakikisha maoni ya makundi mbalimbali yanazingatiwa kabla ya mapendekezo ya mwisho kuandaliwa.

Kwa mujibu wa Bore, hatua ya kwanza itakuwa kupitia upya manifesto za UDA na ODM za 2022, kutathmini utekelezaji wa ahadi zilizotolewa na kubaini maeneo yaliyofanikiwa na yale yanayohitaji kuboreshwa.

“Tunataka kuhakikisha ahadi tulizotoa 2022 zinatimizwa kikamilifu,” alisema.

Kamati hiyo ina wanachama 12, ambapo kila chama kimetoa wataalamu watano huku Bore na Mkurugenzi Mkuu wa ODM Oduor Ong’wen wakihudumu kama wanachama wa moja kwa moja.

Kwa upande wa ODM, wanachama ni Isaac Wanuge, Maryam Abdullahi Mbaruk, Profesa Leonida Kerubo Omosa, Carey Orege na Profesa Bernard Muok.

UDA imewakilishwa na Dkt Emmanuel Nzai, Dkt Daniel Mwai, Bramwel Simiyu, Mohammed Hassan na Dkt Cecilia Ng’etich.

Orege, ambaye ni mwenyekiti wa muda wa kamati hiyo, alisema wamemaliza mkutano wa utangulizi na sasa wanasubiri mwongozo rasmi wa majukumu yao kabla ya kuandaa ratiba kamili ya kazi.

Muundo wa kamati hiyo unaonyesha kuwa UDA na ODM zimeweka mkazo katika badala ya umaarufu wa kisiasa.

Wanachama wake wanatoka katika sekta za uchumi, afya, miundombinu, elimu, sayansi, maendeleo, utawala wa umma na uongozi wa vyama vya siasa.

Changamoto kubwa inayowakabili wataalamu hao ni kuoanisha sera za vyama viwili ambavyo vilikuwa katika pande tofauti za kisiasa katika uchaguzi uliopita na kuandaa ajenda moja itakayowavutia wapigakura.

Bore alisema kamati hiyo itachunguza mafanikio yaliyopatikana, changamoto zilizobaki na maeneo ambayo serikali ingeweza kufanya vizuri zaidi.

“Hatutaki kuonekana tunaishi katika ulimwengu wa njozi. Tunataka matarajio ya wananchi kutoka maeneo yote ya nchi yawe sehemu ya manifesto,” alisema.

Rais Ruto alitangaza kuundwa kwa kamati hiyo baada ya mkutano wa viongozi wa UDA na ODM, akisema kazi yao haitakuwa tu kuandika manifesto ya kampeni bali pia kuweka msingi wa maono ya maendeleo ya taifa.