Kaunti zapambana kuokoa huduma za Ukimwi baada ya ufadhili wa Amerika kukatika
KUPUNGUZWA ghafla kwa ufadhili wa kimataifa wa afya kumezilazimisha kaunti zenye idadi kubwa ya watu wanaoishi na virusi vya Ukimwi kubuni njia mpya za kuhakikisha huduma haziathiriki.
Homa Bay, Kisumu, Siaya, Migori na Mombasa ni miongoni mwa kaunti zinazokabili changamoto hiyo baada ya misaada kutoka kwa wafadhili wa kimataifa, hasa Mpango wa Dharura wa Rais wa Amerika wa Kukabiliana na Ukimwi (PEPFAR), kupungua.
Kwa miaka mingi, fedha hizo zilisaidia kugharamia wahudumu wa afya, usambazaji wa dawa na vifaa, pamoja na huduma maalumu kuhusu Ukimwi.
Tathmini iliyochapishwa Aprili 2025 na Harm Reduction International (HRI) na Kenya Legal & Ethical Issues Network on HIV and AIDS (KELIN) ilionyesha ukubwa wa pengo hilo.
Takriban kliniki 28 zilizokuwa zikitoa huduma za Ukimwi na tiba ya uraibu wa dawa za kulevya zililazimika kufungwa au kupunguza shughuli.
Ripoti hiyo ilikadiria kuwa Serikali ya Kenya ingehitaji takriban Sh66.9 bilioni kufidia kikamilifu pengo lililoachwa na kupunguzwa kwa ufadhili wa Amerika.
Hata hivyo, kaunti zimeanza kutumia mapato yao na kuunganisha huduma za Ukimwi na huduma nyingine za afya ili kuendelea kuwahudumia wagonjwa.
Mwenyekiti wa Kamati ya Afya ya Baraza la Magavana na Gavana wa Mombasa Abdulswamad Shariff Nassir alisema mpito huo umekuwa wa hatua kwa hatua badala ya kusitisha huduma ghafla.
“Kaunti zinatumia fedha zao za kuboresha vituo vya afya (FIF) kusaidia mahitaji yanayoendelea,” alisema.
Huko Migori, asilimia 30 ya fedha zinazokusanywa kila mwezi kupitia FIF hutumika kununua dawa na vifaa kulingana na mahitaji ya vituo.
Afisa Mkuu wa Afya wa kaunti hiyo Caleb Opondi alisema pia wanapata msaada kutoka kwa washirika wa eneo hilo.
Migori pia imeanza kuwaajiri baadhi ya wahudumu wa afya waliopoteza ajira baada ya wafadhili kusitisha ufadhili.
Kisumu imeunda kamati maalumu ya mpito inayoongozwa na Naibu Gavana Matthew Ochieng ili kuandaa kaunti kukabiliana na mabadiliko hayo na kuwaajiri baadhi ya wahudumu walioathirika.
Kaunti pia imeanza kupata fedha moja kwa moja kupitia makubaliano ya ushirikiano na Kituo cha Kudhibiti na Kuzuia Magonjwa cha Amerika (CDC).
Homa Bay nayo imeunganisha huduma za Ukimwi na kifua kikuu (TB) katika huduma za kawaida za wagonjwa wa nje badala ya kuziendesha katika kliniki maalumu za Ukimwi.
Afisa Mkuu wa Afya Grace Osewe alisema kaunti inalenga kuhakikisha huduma zinaendelea bila kuathiriwa na mabadiliko ya ufadhili.
“Kuondoka kwa wafadhili hakupaswi kusababisha kukatizwa kwa huduma wala kupoteza mafanikio ambayo Homa Bay imepata katika kudhibiti Ukimwi na TB,” alisema.
Homa Bay pia imeongeza mafunzo kwa wahudumu wa afya na kutumia Wahudumu wa Afya ya Jamii (CHPs) kuwafikia wagonjwa katika jamii.
Siaya imechukua hatua kama hiyo kwa kuunganisha huduma za Ukimwi na magonjwa mengine sugu.
Hatua hiyo pia inalenga kupunguza unyanyapaa kwa kuhakikisha wagonjwa wote wanapata huduma katika sehemu moja.
Nairobi imeanza kutumia mapato kutoka kwa Mamlaka ya Afya ya Jamii (SHA) kugharamia huduma.
Kaunti hiyo imekusanya Sh1.8 bilioni kutoka SHA tangu Oktoba mwaka jana na sehemu ya fedha hizo inatumika kuendesha vituo vya afya.
Afisa wa Afya ya Kinga Nairobi, Dkt Carol Ngunu, alisema karibu wahudumu 600 waliokuwa wakifanya kazi katika kliniki zilizokuwa zikifadhiliwa na washirika wamechukuliwa na kaunti.
Hata hivyo, kupunguzwa kwa ufadhili kumeathiri zaidi huduma maalumu kwa watu wanaotumia dawa za kulevya, wakiwemo wanaopokea tiba ya methadone.
HRI na KELIN zinakadiria kuwa Kenya ina takriban watu 27,056 wanaodunga dawa za kulevya, huku kiwango cha maambukizi ya HIV miongoni mwao kikiwa asilimia 11.3.
Baadhi ya vituo vimefungwa kutokana na ukosefu wa fedha, huku vingine vikikabiliwa na uhaba wa dawa na huduma za ushauri nasaha.
Changamoto hizo zimeongeza shinikizo kwa kaunti kuhakikisha kuwa kupungua kwa misaada ya kimataifa hakubadili huduma zinazohusiana na Ukimwi kuwa janga jipya la afya ya umma.