Habari

Tume ya IEBC yaagizwa kuangazia upya zabuni ya teknolojia ya uchaguzi

Na SAM KIPLAGAT September 5th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

TUME Huru ya Uchaguzi na Mipaka ncini (IEBC) imeagizwa kufanya marekebisho katika zabuni yake ya ununuzi wa teknolojia itakayotumika katika Uchaguzi Mkuu wa 2027 baada ya Bodi ya Ukaguzi wa Ununuzi ya Umma (PPARB) kugundua mapungufu katika vigezo vya tathmini na mahitaji ya kiufundi yaliyowekwa kwenye nyaraka za zabuni hiyo.

Bodi hiyo ilisema kuwa zabuni hiyo haikueleza kwa uwazi jinsi kutimiza mahitaji ya kiufundi yangepimwa sambamba na mfumo wa alama za tathmini, hali ambayo ingeweza kusababisha wakaguzi kutoa alama tofauti kwa mapendekezo yenye sifa zinazofanana.

“Stakabadhi za zabuni zinapaswa kueleza wazi ikiwa kutimiza kila kipengele cha kiufundi ni lazima au ikiwa kuna njia mbadala za kuthibitisha utiifu huo,” bodi ilisema.

Bodi iliongeza kuwa pale ambapo maelezo ya kiufundi yanahusisha masharti kadhaa, stakabadhi za zabuni zinapaswa pia kufafanua iwapo masharti yote lazima yatimizwe au kama kutimiza idadi fulani ya masharti kunatosha ili zabuni ichukuliwe kuwa imekidhi vigezo.

Aidha, IEBC imeagizwa kutafuta ushauri na msaada wa kiufundi kutoka kwa Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi ya Umma (PPRA) kabla ya kuendelea na mchakato huo wa ununuzi.

Ukaguzi huo unalenga kuhakikisha kuwa mahitaji yote yanaelezwa kwa uwazi, ushahidi unaohitajika kuthibitisha unatambuliwa bayana, na mfumo wa kutoa alama unakuwa wa haki, wa wazi na unaoweza kupimika.

PPARB iliagiza IEBC kufanya marekebisho, ufafanuzi na mabadiliko yanayohitajika katika stakabadhi za zabuni, kisha ichapishe toleo jipya na kupatia wote wanaowania zabuni muda unaotakiwa kisheria, lakini usiopungua siku saba, ili kuzingatia marekebisho hayo na kuwasilisha zabuni zao.

Uamuzi huo ulitokana na malalamishi yaliyowasilishwa na kampuni ya Galadirel Investment Limited, ambayo ilitaka kusitishwa kwa zabuni hiyo ikidai kuwa masharti yake yalikuwa ya kibaguzi na yalitungwa kwa njia inayonufaisha kampuni ya Miru Systems ya Korea Kusini, inayojihusisha na teknolojia za uchaguzi.

Zabuni hiyo inahusu Mfumo Jumuishi wa Kusimamia Uchaguzi (IEMS) pamoja na vifaa vinavyohusiana nao, ambavyo vitasaidia vifaa vya KIEMS vinavyotumika kutambua wapigakura kwa alama za kibayometriki na kusambaza matokeo ya uchaguzi.

Hii ni moja ya zabuni mbili kubwa za kimataifa zilizotangazwa na IEBC kwa maandalizi ya Uchaguzi Mkuu wa 2027.

 

Zabuni nyingine inahusu uchapishaji wa karatasi za kura, vifaa maalum vya wapigakura wenye ulemavu wa kuona, Daftari la Wapigakura na fomu rasmi za uchaguzi.

Galadirel ilidai kuwa stakabadhi za zabuni zilikuwa na masharti magumu ambayo yangeweza kuwazuia washindani wengine kushiriki.

Miongoni mwa masharti yaliyopingwa ni hitaji la wanaowania zabuni kuwa na angalau miaka mitano ya uzoefu katika usambazaji wa teknolojia za uchaguzi, vifaa, mitambo na vifaa saidizi.

Pia, walitakiwa kuthibitisha kuwa kati ya mwaka 2021 na 2025 walitekeleza angalau mkataba mmoja wa teknolojia ya uchaguzi na kusambaza angalau vifaa 50,000 kwa mteja mmoja katika kipindi hicho.

Kampuni hiyo ilidai kuwa masharti hayo yalionekana kuakisi uzoefu na mafanikio ya Miru Systems.

“Haya ni masharti yanayoonekana kufanana moja kwa moja na mafanikio ambayo Miru Systems imepata katika zabuni za hapo awali,” Galadirel ilisema mahakamani.

Hata hivyo, bodi ilikataa hoja kwamba kuwepo kwa mahitaji maalum pekee kunamaanisha kuwa zabuni hiyo ilibuniwa kinyume cha sheria kunufaisha kampuni fulani.

Bodi ilieleza kuwa taasisi inayofanya ununuzi ina haki ya kuweka viwango vya uzoefu, uwezo wa kiufundi na umahiri wa kitaaluma vinavyohitajika kwa utekelezaji wa kandarasi husika.