Habari

Serikali yawataka wakulima wavune mazao yao kabla ya El Nino kuanza

Na CECIL ODONGO September 8th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

WAKULIMA wameshauriwa kutumia wiki tatu zijazo kukamilisha uvunaji, ukaushaji mazao yao na kuandaa mashamba yao kabla ya kuanza kwa msimu wa mvua ya El Nino.

Ushauri huo umetolewa na Idara ya Utabiri wa Hali ya Anga (KMD) inayoshikilia kuwa hali ya ukame itaendelea kushuhudiwa maeneo mengi ya nchi katika mwezi huu wa Septemba.

“Wakati huu ambapo hali ya anga ni kavu, wakulima wanafaa kuvuna mazao yao yaliyokomaa, kuyakausha na kuyahifadhi ili yasiharibike,” akaeleza Naibu Mkurugenzi wa idara hiyo, Paul Oloo.

“Aidha, mwezi huu wa Septemba ni mwafaka kwa wakulima kutayarisha mashamba yao, kurekebisha miundo msingi ya kuvuna maji, kuzibua mitaro ya kupitisha maji, kununua mbegu na pembejeo zingine kwa ajili ya upanzi wakati wa msimu wa mvua wa Oktoba-Novemba-Desemba,” akaongeza.