Moto kambi ya Ruto wandani wakivurugana wakisaka ubabe
UBABE wa kisiasa kati ya mawaziri au watumishi wa umma na wanasiasa wanaoumuunga mkono Rais William Ruto unaendelea kutokota, hali inayoweza kuathiri kuchaguliwa kwake tena mnamo 2027.
Mivutano hiyo imejitokeza katika maeneo ambayo Rais anatarajiwa kupata kura nyingi huku ikiwa wazi Mlima Kenya iliyokuwa ngome yake ya kisiasa inaendelea kumponyoka.
Katika Kaunti ya Kakamega, mvutano kati ya Waziri wa Vyama vya Ushirika Wycliffe Oparanya na Gavana Fernandes Barasa umetokota na kufikia kilele.
Bw Barasa amemtaka Rais Ruto amtimue Bw Oparanya, akidai waziri huyo amekuwa akifanya mikutano ya usiku kupanga njama za kumng’oa 2027.
“Namwambia Rais Ruto kwamba tunamheshimu, lakini hapa Kakamega umetuletea mzozo kupitia Waziri Oparanya, ambaye hajui kazi yake wala haelewi majukumu yake. Kazi yake hapa ni kufanya mikutano ya usiku ya kuniondoa madarakani na kunipangia mabaya. Kazi uliyompa haitusaidii. Tafadhali mpe mtu mwingine,” akasema Bw Barasa.
Gavana huyo pia anadai Bw Oparanya anamuunga mkono Mbunge Mwakilishi wa Kike wa Kakamega Elsie Muhanda kuwania ugavana.
Bw Oparanya, aliyekuwa gavana wa Kakamega kati ya 2013 na 2022, amekanusha madai hayo akisema hana mgombea anayemuunga mkono. Alimtaka Bw Barasa kujikita katika kutetea kiti chake.
“Anaonekana kupigana vita na nafsi yake kwa sababu yeye si mtu wa hadhi yangu kisiasa. Kwa nini nimfadhili mtu ampinge? Uchaguzi ni wa ushindani na ikiwa anaogopa ushindani basi aachane na siasa,” akasema Bw Oparanya kwenye mahojiano na Taifa Leo.
Mbunge wa Khwisero Christopher Aseka pia alimkosoa Bw Barasa, akisema rekodi yake ya maendeleo si ya kuridhisha.
“Amewahi kufanya nini kuhusiana na masuala ya maendeleo? Amekuwa akiorodheshwa vibaya katika maendeleo na miradi mingi iliyoanzishwa na Oparanya haijakamilika. Rekodi ya Barasa katika maendeleo ni duni na hatutamruhusu kuendeleza siasa za chuki hadi kumtaka Rais amtimue Oparanya,” akasema Bw Aseka.
Kajiado pia imekuwa uwanja wa mzozo kati ya Msimamzi wa Wafanyakazi Ikulu Katoo ole Metito na Gavana Joseph Ole Lenku, ambao wote waligombea ugavana 2022.
Bw Lenku, anayelenga sasa kiti cha useneta, amepinga mpango wa kisiasa wa UDA na ODM unaomuunga mkono Bw Metito kugombea ugavana na Judy Pareno kuwania useneta.
Pia ametishia kuondoka ODM na kujiunga na Linda Mwananchi.
“Kuna mtu anatudharau mbele yako, lakini hatutavuruga mkutano wako wala kulipiza kisasi. Katoo anadai kuwa msemaji wa Wamaasai ilhali yeye ni msemaji wako. Walisema pia Amboseli haitarejeshwa kwa jamii, lakini neno lako ndilo la mwisho,” akasema Bw Lenku wakati wa mkutano wa Rais katika kaunti yake wikendi.
Katika Bonde la Ufa, Waziri wa Usalama wa Ndani Kipchumba Murkomen anakabiliwa na upinzani kutoka kwa baadhi ya wanasiasa wanaodai anawadhamini wagombeaji ili kuwa na ushawishi eneo hilo baada ya Rais Ruto.
Mbunge wa Keiyo Kusini Gideon Kimaiyo mnamo Agosti 5 alikerwa na Bw Murkomen na akasema Kaunti ya Elgeyo-Marakwet si himaya yake kisiasa.
“Elgeyo-Marakwet haitakuwa ufalme wa mtu yeyote, wala hatafanikiwa na mipango yake Keiyo Kusini. Ikiwa unataka kuwa kinara, pigana na wanaowania nafasi hiyo pamoja nawe, si Keiyo Kusini,” akasema Bw Kimaiyo.
Seneta wa Nandi Samson Cherargei pia alimtaka Bw Murkomen kuweka kando ndoto zake za 2032 na kumsaidia Ruto katika uchaguzi wa 2027.
“Aweke kando kwa sasa ndoto zake za 2032 na za kuwa kinara, na amsaidie Rais. Hawezi kupigania kuwa msemaji wa jamii wakati tuna Rais Ruto,” akasema.
Busia nako hali si tofauti, Katibu Mkuu wa Biashara Ndogo Ndogo Susan Mangéni naye akimshambulia aliyekuwa Waziri wa Michezo Ababu Namwamba, akidai anapinga kuchaguliwa kwa Rais Ruto kichinichini.
“Ababu Namwamba, unapinga kuchaguliwa tena kwa Rais Ruto kwa sababu umeumia. Watu wa Budalang’i hawataendelea kuishi katika umaskini wa kudumu kwa sababu ya ubinafsi wako. Wewe si Budalang’i na Budalang’i si wewe,” akasema Bi Mangéni.
Wawili hao wamekuwa na uhasama mkali kuhusiana na siasa za UDA.