Wakenya wengi wasema nchi inaelekea pabaya, wasota kuliko walivyokuwa 2022
ASILIMIA 76 ya Wakenya wanaamini nchi inaelekea vibaya, huku asilimia 65 wakisema hali yao ya kiuchumi imezorota tangu Rais William Ruto aingie mamlakani mnamo 2022.
Hii ni kwa mujibu wa utafiti mpya wa Kampuni ya Utafiti ya TIFA.
Utafiti huo uliofanywa kati ya Juni 13 na 22, 2026, kwa kuwahoji watu 2,048 katika kaunti zote 47, umeonyesha kiwango cha kutoridhika kimefika juu zaidi tangu TIFA ianze kufuatilia suala hilo mnamo 2023.
Ni asilimia 14 pekee walioamini Kenya inaelekea upande unaofaa, huku asilimia 12 wakisema hali yao ya kifedha imeimarika tangu uchaguzi wa 2022. Asilimia 23 walisema hali yao haijabadilika.
Mlima Kenya ndio uliorekodi hisia hasi zaidi, ambapo asilimia 90 ya waliohojiwa walisema nchi inaelekea pabaya, ikifuatiwa na Nairobi kwa asilimia 89.
TIFA ilisema ukosefu wa ajira na umaskini ndio matatizo makubwa zaidi nchini, yakitajwa na asilimia 44 ya waliohojiwa.
Kupanda kwa bei ya bidhaa na ushuru mkubwa ulitajwa na asilimia 25 ya waliohojiwa.
Utafiti pia ulionyesha imani ndogo kwa taasisi za umma. Hakuna taasisi iliyopata imani ya zaidi ya asilimia 40.
Mahakama iliongoza kwa asilimia 36, ikifuatiwa na serikali za kaunti kwa asilimia 31 na Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka Nchini (IEBC) kwa asilimia 30.
Imani kwa Rais Ruto iligawanyika kisiasa. Asilimia 58 ya wanaounga mkono Serikali ya Jumuishi walisema wanamwamini, ikilinganishwa na asilimia 16 ya wanaopinga utawala huo.
TIFA ilisema iwapo hali ya kiuchumi haitaimarika mwaka ujao, huenda ikawa changamoto kwa wanasiasa wanaotafuta kuchaguliwa tena, hasa wanaohusishwa na serikali ya sasa.