Habari za Kitaifa

Mateso ya mgomo yazidi kutisha wagonjwa wakiendelea kuaga dunia

Na WAANDISHI WETU September 9th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

TAKRIBAN wanawake 22 walifariki dunia kutokana na matatizo yanayohusiana na uzazi katika kipindi cha wiki moja huku mgomo wa wauguzi ukiendelea nchini.

Aidha, vifo vya watoto wachanga 44 na vifo 130 vya watoto kabla au wakati wa kuzaliwa pia vimeripotiwa, hali inayofichua ukubwa wa janga la afya linalokumba taifa.

Takwimu hizo zimetolewa wakati ambao wauguzi wamesusia kazi kwa zaidi ya mwezi mmoja, jambo ambalo limevuruga huduma katika hospitali nyingi za umma kote nchini.

Wataalamu wa afya wanaonya kuwa hali inaweza kuwa mbaya zaidi iwapo madaktari nao watatekeleza tishio lao la kugoma katika siku chache zijazo.

Mgomo wa wauguzi ulianza Julai 29, 2026, kufuatia mzozo kuhusu utekelezaji wa Mkataba wa Pamoja wa Kazi wa mwaka 2017, marupurupu mbalimbali na kuajiriwa kwa wahudumu wa mpango wa Afya kwa Wote (UHC) kwa masharti ya kudumu.

Kaunti za Nakuru, Kisumu, Kakamega na Kajiado zimetajwa kuwa miongoni mwa maeneo yaliyoathirika zaidi na mgomo huo.

Hospitali ambazo awali zilikuwa zikihudumia mamia ya wagonjwa kila siku sasa zimebaki na shughuli chache huku wagonjwa wakikosa huduma muhimu.

Katika Hospitali ya Rufaa na Mafunzo ya Nakuru ambazo kwa kawaida huwa zimejaa wagonjwa na wahudumu wa afya zimekuwa tulivu isivyo kawaida.

Huduma chache zinazotolewa sasa zinategemea maafisa wa utabibu na wanafunzi wa udaktari, huku wagonjwa wakisema kiwango cha huduma si sawa na kile walichokuwa wakipata kabla ya mgomo.

Pwani nayo imeathirika vibaya. Katika Hospitali Kuu ya Rufaa ya Coast General mjini Mombasa, huduma za uzazi, meno, masikio, pua na koo pamoja na vitengo vingine muhimu zimekwama.

Baadhi ya familia zimehamisha wagonjwa wao hadi hospitali za kibinafsi kwa hofu ya kupoteza maisha.

“Tumeamua kumtoa mgonjwa wetu hospitalini kwa sababu hajapata matibabu ya maana kwa wiki tatu. Tunampeleka hospitali ya kibinafsi kwa matumaini ya kupata huduma bora,” alisema mmoja wa jamaa za mgonjwa.

Katika Kaunti za Meru, Laikipia, Narok, Bomet na Uasin Gishu, hali si tofauti. Wagonjwa wanaohitaji huduma za kulazwa hospitalini wamekuwa wakielekezwa katika hospitali za kibinafsi na za makanisa, jambo ambalo limeongeza mzigo wa gharama kwa familia nyingi.

Wajawazito ni miongoni mwa walioathirika zaidi. Milka Kimani kutoka Mpeketoni, Lamu, alisema amelazimika kutafuta huduma katika kliniki za kibinafsi baada ya kukosa kuhudumiwa katika hospitali ya serikali.

“Unafika hospitalini kwa kliniki lakini hakuna anayekuhudumia. Nililazimika kutafuta huduma mahali pengine ingawa gharama ni kubwa,” alisema.

Katika baadhi ya maeneo, wanaougua magonjwa sugu kama pumu, kisukari na shinikizo la damu pia wamekosa huduma za kawaida.

Wengine wanalazimika kununua dawa katika maduka ya kibinafsi kwa gharama kubwa huku baadhi ya hospitali za serikali zikiripotiwa kukosa dawa.

Huku mazungumzo kati ya viongozi wa Chama cha Wauguzi na Baraza la Magavana yakikosa kuzaa matunda, wananchi wanaendelea kulipa gharama kubwa zaidi.

Wengi wanasema serikali za kaunti na serikali kuu zimekuwa zikilaumiana huku maisha ya wagonjwa yakiendelea kuwa hatarini.

Sasa hofu kubwa ni kwamba iwapo mgomo utaendelea kwa muda mrefu zaidi, vifo vitaongezeka na hospitali za umma, ambazo ndizo tegemeo la mamilioni ya Wakenya maskini, zitaendelea kuwa maeneo ya mateso badala ya vituo vya kuokoa maisha.