Abautani nyingi za Ruto zaibua maswali iwapo ni mbinu ya kusaka uungwaji
RAIS William Ruto amekuwa akitoa matamshi ambayo yanaonekana kuridhisha umma kwenye mikutano kisha kauli hizo zinabadilishwa kutokana na sera kuzimwa na sera ya serikali kukinzana na matamshi hayo.
Matamshi mengi ya Rais William Ruto katika mikutano ya kisiasa na kubadilishwa kwa baadhi ya sera na maagizo ya serikali kumeibua maswali kuhusu iwapo utawala wake unaendeshwa zaidi na malengo ya kisiasa kuliko utoaji wa huduma kwa wananchi.
Huku uchaguzi wa 2027 ukikaribia na upinzani ukizidi kumkabili, Rais amekuwa akionekana kulegeza baadhi ya misimamo yake baada ya kukumbana na upinzani kutoka kwa wananchi.
Tukio la hivi punde ni kubadilishwa kwa uamuzi wa Mamlaka ya Ukusanyaji Ushuru Nchini (KRA) kuongeza kiwango cha chini cha thamani ya mizigo iliyounganishwa inayotozwa ushuru kutoka Sh2.5 milioni hadi Sh3.2 milioni.
Baada ya wafanyabiashara wadogo kupinga hatua hiyo wakisema ingeongeza mzigo wao wa kodi, Rais aliagiza KRA kupunguza kiwango hicho hadi Sh2 milioni.
“KRA itapunguza kiwango kinachotumika kwa mizigo yote iliyounganishwa kutoka Sh2.5 milioni hadi Sh2 milioni,” ilisoma taarifa ya Wizara ya Biashara.
Wafanyabiashara wadogo ni kundi muhimu la wapigakura na mabadiliko hayo yameonekana na baadhi ya wachanganuzi kama jaribio la serikali kuwapunguza hasira kabla ya uchaguzi wa 2027.
Rais pia alibadili msimamo kuhusu wafanyabiashara wa kigeni wanaojihusisha na biashara ndogo nchini.
Mnamo Septemba 2, alitangaza kuwa wafanyabiashara hao walipaswa kufunganya virago ifikapo Septemba 7. Baadaye, serikali iliwapa siku 90 ili wapate leseni na kuwa nchini kihalali.
“Kuanzia wiki ijayo, wafanyabiashara wote (wageni) wanaofanya biashara hizo ndogo wanapaswa kufunga,” Rais alisema baada ya kukutana na wafanyabiashara wadogo wadogo katika Ikulu ya Nairobi.
Hatua hiyo ilikosolewa na mashirika ya kiraia yaliyomtaka Rais kuomba msamaha na kuwalipa fidia walioathirika.
Waziri wa Biashara Lee Kinyanjui alijaribu kufafanua kuwa serikali inalenga kuhakikisha wageni wanatii sheria za uhamiaji na leseni na hawashindani visivyo na wafanyabiashara raia wa Kenya.
Mabadiliko hayo pia yameonekana katika mzozo wa Kiwanda cha Kemikali cha Tata kinachopatikana Magadi, Kaunti ya Kajiado.
Rais alikuwa ameamuru kampuni hiyo ya India kuondoka nchini, akidai haikuwa ikitoa thamani ya kutosha kwa Wakenya.
“Tumechukua uamuzi wa kisera kwamba hatutaendelea kuuza malighafi nje. Tutaandaa madini yote yanayopatikana Kenya hapa nchini,” akasema Rais alipokuwa akitafuta kura za jamii ya Maa Kaunti ya Kajiado.
Hata hivyo, serikali baadaye ilibadilisha msimamo na kusema itafanya mazungumzo na wawekezaji hao kwa kuzingatia sheria, hivyo kufungua mlango wa mazungumzo na uongozi wa kampuni ya kemikali ya Tata.
Mchanganuzi wa masuala ya kisiasa Javas Bigambo anasema ukosefu wa maelezo ya kina kabla ya serikali kutoa maagizo umeifanya ionekane kama inategemea matamshi ya kisiasa.
Hata hivyo, alisema baadhi ya hatua hizo zinaweza kuwa na msingi wa kisheria.
“Kuhusu kampuni ya Tata, ni kutotii Sheria ya Uchimbaji Madini ya 2016. Kwa hivyo, suala linapaswa kuwa ni kampuni ngapi za uchimbaji madini zinatii sheria,” akasema.
Serikali pia imebadili msimamo kuhusu ufadhili wa elimu ya juu.
Hii ni baada ya mfumo mpya wa ufadhili kukosolewa, Rais akisema wanafunzi wote watakaotimiza vigezo vya kujiunga na vyuo vikuu watapata ufadhili kamili wa serikali chini ya mfumo unaopendekezwa.
“Mfumo ambao tuliujaribu, haukufanya kazi na karibu ulisababisha vyuo vyetu vingi kufungwa,” akasema Rais.
Mabadiliko hayo yanazua kumbukumbu kuhusu hatua nyingine zilizochukuliwa tangu Rais aingie mamlakani mnamo 2022.
Miongoni mwa hizo ni kuondolewa kwa ruzuku ya unga wa mahindi na mafuta, ambayo Rais alisema ilikuwa mzigo mkubwa kwa serikali.
Hata hivyo, kutokana na kupanda kwa gharama ya maisha, serikali baadaye ilirejesha kwa muda ruzuku ya mafuta.
Hivi majuzi, Waziri wa Hazina John Mbadi alisema serikali inatafuta fedha za kutoa ruzuku kwa mafuta ili kuwalinda Wakenya kutokana na kupanda kwa bei.
Serikali pia ilibadili msimamo wake kuhusu ushirikiano na upinzani. Rais Ruto aliwahi kukataa vikali kurejea kwa mfumo wa “handisheki”, lakini maandamano makubwa ya vijana mnamo 2024 yalimfanya kuingia katika Serikali Jumuishi na ODM ya marehemu Waziri Mkuu Raila Odinga.
Hatua hiyo ilifuatwa na kuondolewa kwa baadhi ya mapendekezo ya kodi yaliyokuwa katika Mswada wa Fedha wa 2024.
Rais pia alilazimika kuvunja Baraza lake la Mawaziri na kufanya mabadiliko kadhaa baada ya maandamano hayo.
Licha ya mabadiliko hayo, Rais amekuwa akitetea Serikali Jumuishi akisema imesaidia kuleta utulivu na maendeleo nchini.
“Serikali Jumuishi haikuwa kosa ila niliibuni kimakusudi,” akasema kwenye mkutano mmoja wa kisiasa Kaunti ya Kisii mnamo Aprili mwaka huu.
Kwa wananchi, changamoto sasa ni kujua ikiwa mabadiliko haya ni marekebisho ya sera baada ya kusikiliza maoni yao au ni mikakati ya kisiasa ya kutafuta uungwaji mkono kuelekea 2027.