Kasisi aasi upadri na kuoa mmoja wa ‘kondoo’ wake
ALIYEKUWA kasisi wa Kanisa Katoliki kutoka Italia, Sandro Ferretto, alimuoa Sharon Jepngok Kibet, 37, wikendi katika sherehe ya kitamaduni ya Tugen iliyofanyika Kasiela, Baringo Kusini.
Ferretto, 53, aliwahi kuhudumu kama kasisi katika eneo hilo kwa karibu miaka 12 kabla ya kuacha ukuhani na kurejea Italia.
Sherehe hiyo ilivutia maelfu ya wakazi waliokuwa wamekusanyika katika boma la babake Sharon, John Wendot, baada ya kusikia kuwa Mzungu alikuwa akimuoa binti wa eneo hilo.
Hata hivyo, wengi walishangaa kumtambua bwana harusi kuwa kasisi wao wa zamani ambaye waliwahi kumwona akihudumu katika maeneo ya Kasiela, Chebinyiny, Sinoni, Embosos na Nyimbei.
Bw Ferretto aliwasili Kenya mnamo 2008 na kwa miaka yake ya utumishi alitembelea familia, kuhudhuria shughuli za shule, kuwashauri vijana, kusaidia familia zilizohama makwao kutokana na ukosefu wa usalama na kuendesha misa.
Sharon alilelewa Kasiela kabla ya kumaliza shule ya upili na kusomea udaktari wa kliniki. Baadaye alisafiri hadi Italia ambako uhusiano wake na Ferretto ulianza.
Mnamo 2022, Bw Ferretto aliwasaidia Sharon na vijana wengine saba kutoka eneo hilo kupata ajira nchini Italia.
Sharon alimweleza babake mnamo 2024 kuwa Bw Ferretto alikuwa ameacha ukuhani na alitaka kumuoa.
“Binti yangu aliniambia kwamba Padre Sandro alikuwa amejiuzulu na alitaka kumuoa. Nilijiuliza, kasisi anawezaje kuoa?” akasema Bw Wendot.
Alisema baadaye alikubali baada ya kufahamishwa kuwa Ferretto alikuwa amekamilisha taratibu zote za kuacha ukuhani na kupewa idhini ya kuoa.
Wawili hao walifanya harusi ya kanisani nchini Italia Aprili mwaka huu kabla ya kurejea Kenya kwa sherehe ya koito.
Bw Wendot alisema hakutaka kutumia uraia wa Bw Ferretto kama kisingizio cha kudai mahari ya kupita kiasi.
“Niliozesha binti yangu kwa raia wa Italia kama mtu mwengine yeyote. Sikutarajia kumtendea kama mgeni na kumpunja pesa,” akasema.
Bw Ferretto aliongozana na jamaa 12 kutoka Italia, marafiki na waliokuwa wafanyakazi wenzake katika Parokia ya Mochongoi.
Sherehe hiyo ilijawa na nyimbo na ngoma za Kalenjin huku Bw Ferretto akicheza pamoja na wakwe na marafiki wake Wakenya.
Raymond Cheboi, mdogo wa Sharon, alisema Bw Ferretto alikuwa rafiki wa familia na aliwahi kumsaidia mmoja wa ndugu zao kuwa katekista.
Henry Cheburet, mkazi aliyemjua Ferretto tangu alipokuwa kasisi, alisema ndoa hiyo imekuwa gumzo kijijini.
“Wengi walifika wakitarajia kumuona Mitalia akimuoa Sharon, lakini baadaye wakagundua kuwa alikuwa kasisi wao wa zamani,” alisema.
Wendot alisema amewabariki walioana.
“Nimewapa baraka zangu. Mungu awabariki katika ndoa yao,” alisema.