Trump adai Iran inakataa kusitisha vita ‘ili kumuumiza’ katika uchaguzi wa ‘mid-term’ Novemba
WASHINGTON, Amerika:
RAIS Donald Trump amesema anaamini vita kati ya Amerika na Iran vitamalizika mara tu baada ya uchaguzi wa katikati ya muhula utakaofanyika Novemba.
Trump amesema Iran haitaweza kuendelea na vita hivyo kwa muda mrefu na kwamba Tehran inajaribu kutumia mzozo huo kuathiri matokeo ya uchaguzi wa Amerika.
Akizungumza na wanahabari Jumatano, Trump alisema vita hivyo vitamalizika mara moja baada ya uchaguzi kwa sababu Iran, kwa mujibu wake, haina uwezo wa kuendelea kupambana.
Trump amekuwa akiweka muda wa kumalizika kwa vita hivyo hapo awali, lakini kauli yake ya sasa inaweka mwisho wa uchaguzi wa Novemba kama muda muhimu wa kusitisha mapigano.
Uchaguzi huo wa katikati ya muhula utaamua iwapo chama cha Trump cha Republican kitaendelea kudhibiti Congress, na rais huyo anadai kuwa Iran inajaribu kuingilia mchakato huo wa uchaguzi.
Hata hivyo, ripoti ya Jarida la Wall Street imesema baadhi ya washauri wakuu wa Trump katika Ikulu ya White House, akiwemo Makamu wa Rais JD Vance na Waziri wa Mambo ya Nje Marco Rubio, wamemwambia kwenye kikao cha faragha kwamba vita hivyo vinaweza kuendelea hadi mwisho wa muhula wake wa urais, Januari 2029.
Wakati huohuo, mapigano kati ya Amerika na Iran yameendelea kusababisha bei ya mafuta duniani kupanda huku njia muhimu za usafirishaji katika Mlango wa Hormuz na Bahari ya Shamu zikiendelea kuvurugwa.
Kauli ya Trump kuhusu kumalizika kwa vita baada ya uchaguzi wa Novemba kwa sasa imezua maswali kuhusu uhalisia wa vita hivyo kuisha.