Siasa

Duale akabwa koo vita vya ubabe Kaskazini vikishika kasi kuelekea 2027

Na MANASE OTSIALO September 10th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WAZIRI wa Afya, Aden Duale amekuwa akichukuliwa kama kigogo wa siasa za Kaskazini Mashariki ila kwa sasa ushawishi wake unakabiliwa na visiki huku akiendelea kurindima ngoma ya kuchaguliwa tena kwa Rais William Ruto.

Baada ya kuhudumu kama mbunge, Kiongozi wa Wengi katika Bunge la Kitaifa na sasa waziri, Bw Duale amekuwa akionekana kama mwanasiasa ambaye huamua mkondo wa siasa katika eneo la Kaskazini Mashariki.

Wakati huu ambapo anashikilia nafasi ya uwaziri, baadhi ya wanasiasa kutoka Garissa, Wajir na Mandera, sasa wanamtaka ajiepushe kuamua viongozi wanaostahili kushikilia nyadhifa mbalimbali eneo hilo.

Mnamo Agosti 9, Mwakilishi wa Wanawake wa Wajir Fatuma Abdi Jehow alimwambia hadharani Bw Duale ajiepushe na siasa za Wajir, akidai ameingilia uongozi wa eneo hilo na kujaribu kuwagawa wakazi kwa misingi ya koo.

Kauli yake ilifuatia madai ya Bw Duale kuhusu matumizi ya utajiri na helikopta kushawishi siasa na kumng’oa madarakani.

Bi Jehow alijibu kwa ujasiri kwamba hatima yake ya kisiasa itaamuliwa na wapigakura, wala si watu kutoka nje.

“Kuna watu wanatuambia kwamba wana utajiri na helikopta na wameazimia kuhakikisha hatuchaguliwi tena. Ni Allah pekee anayeweza kutuangusha. Unatoka wapi na wewe ni nani? Shikilia eneo ulikochaguliwa. Ikiwa unataka kuwa kinara wa kisiasa, walete watu pamoja lakini usiwagawe,” akasema.

Wiki mbili baadaye, mvutano huo ulihamia Garissa na ukachacha zaidi.

Mnamo Agosti 20, Mbunge wa Dadaab Farah Maalim alitishia kuhamasisha wakazi kushinikiza Bw Duale aondolewe serikalini, akidai ameingilia siasa za eneo hilo na kulemaza mfumo wa demokrasia ya maafikiano unaotumiwa.

“Si sisi tuliokupa jina la Sultan Hasid. Halikuwa watu wa Wajir wala Mandera, bali watu walio karibu nawe. Tukianza kushawishi, haitachukua siku 14 kukuondoa katika nafasi hiyo,” akasema Bw Maalim kwa Kisomali.

Alimwonya Bw Duale dhidi ya kutumia mamlaka yake kupita kiasi.

“Tafadhali nenda polepole, wewe ni kijana. Tumekuwa mara nyingi tukikulinda lakini ukiendelea, hatutakulinda tena,” akasema.

Jina la ‘Sultan Hasid’, linaloweza kutafsiriwa kwa urahisi kuwa ‘Sultani mwenye wivu’, sasa limegeuka kuwa kejeli ya kisiasa dhidi ya waziri huyo.

Lakini nyuma ya malumbano hayo kuna vita kubwa zaidi kuhusu nani atakayeamua mustakabali wa kisiasa wa eneo hilo.

Mvutano mkubwa zaidi unaonekana Garissa, ambako Seneta Abdulkadir Mohamed Haji ametangaza wazi vita dhidi ya ushawishi wa Bw Duale.

Mnamo Julai 21, Seneta Haji aliapa kufuta nyayo za kisiasa za Bw Duale kutoka kaunti hiyo.

Tangu wakati huo ameungwa mkono na Baraza la Wazee wa Koo Garissa kuwania ugavana, hatua inayomweka katika njia ya makabiliano na Bw Duale na washirika wake.