Siasa

Sifuna awatikisa Mudavadi, Atwoli; waanza ziara Magharibi kumtetea Ruto kwa wananchi

Na MOSES NYAMORI September 8th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WIMBI la kisiasa la Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna kupitia vuguvugu la Linda Mwananchi limewafanya baadhi ya viongozi wakuu wa serikali kutoka eneo la Magharibi kuanza kampeni kali kwa Rais William Ruto katika uchaguzi wa 2027.

Kinara wa Mawaziri Musalia Mudavadi, ambaye amekuwa akijiepusha na shughuli za kisiasa, ameanza ziara za mashinani kuimarisha uungwaji mkono wa chama tawala cha UDA.

Mwishoni mwa wiki, Bw Mudavadi alikutana na waliowania tiketi za UDA kutoka Magharibi, huku Katibu Mkuu wa Cotu-K Francis Atwoli akiwa miongoni mwa waliohusika na mikakati ya kupanga mkutano huo.

Mnamo Jumatatu, Waziri wa Vyama vya Ushirika Wycliffe Oparanya pia alikutana na wabunge 25 kutoka Magharibi jijini Kisumu kujadili jinsi ya kumfanyia Rais Ruto kampeni.

“Tulikutana kujadili masuala yanayohusu uchaguzi ujao na jinsi tunavyoweza kujiweka vyema kama jamii,” akasema Bw Oparanya.

Waziri wa Kawi Opiyo Wandayi na Naibu Gavana wa Kakamega Ayub Savula nao wamebuni kikosi cha kampeni kinacholenga Magharibi na Nyanza, kwa lengo la kuimarisha uungwaji mkono kwa Rais Ruto.

Wadadisi wa masuala ya kisiasa wanasema shughuli hizo zinaonekana kulenga kukabili kuongezeka kwa ushawishi wa mrengo wa Linda Mwananchi.

Azma ya Bw Sifuna kuwania urais imeibua msisimko katika eneo hilo, huku kukiwa na hofu kwamba vuguvugu hilo linaweza kutokomeza umaarufu wa ODM na pia UDA.

Bw Mudavadi alisema uchaguzi wa 2027 utahitaji maandalizi mazuri, akiwataka wagombea wa UDA kuimarisha miundo ya chama mashinani na kuhakikisha usajili wa wapigakura unaongezwa.

Alikadiria kuwa kuna wapiga kura milioni 1.5 wenye vitambulisho ambao bado hawajajisajili kutoka eneo la Magharibi.

“Njia ya kuelekea 2027 haitashindwa kwa kelele, bali kwa mpangilio, uaminifu na kura,” akasema.

Bw Atwoli aliwataka wagombea kumuunga mkono Bw Mudavadi kama kinara wa kisiasa wa eneo hilo, akisema Bw Sifuna bado hajatosha mboga.

“Yeye atakuwepo baada yetu, lakini wakati wake si sasa,” akasema Bw Atwoli.

Hata hivyo, Seneta wa Vihiga Godfrey Osotsi anayeegemea mrengo wa Linda Mwananchi alipuuzilia mbali mkutano huo, akisema hauwatikisi.

Alisema UDA imepoteza umaarufu Magharibi na ndio maana mkutano huo ulifanyika Kisumu badala ya mji wa Magharibi.

“Wameingiwa na hofu na unaweza kuona kukata tamaa katika shughuli zao. Eneo hili lina maeneobunge 33, lakini uliuona idadi ya wagombea waliohudhuria mkutano huo,” akasema. 

Bw Osotsi alidai kuwa baadhi ya viongozi na wagombea kutoka eneo hilo wanasubiri tu chama kipya cha Linda Mwananchi kuanzishwa rasmi ili waondoke UDA na ODM.

Hata hivyo, Bw Wandayi na Bw Savula wamesisitiza kuwa wataendelea kuwarai wenyeji wa Magharibi na Nyanza kumuunga mkono Rais Ruto, wakisema uongozi wake ndio utahakikisha maendeleo zaidi katika maeneo hayo.