Polisi wazima jaribio la kutibua mkutano wa Profesa Kindiki
POLISI wa kutuliza ghasia Jumamosi walizuia jaribio la kundi la vijana kuvuruga mkutano wa kisiasa wa Naibu Rais Kithure Kindiki katika Uwanja wa Nembure, Kaunti ya Embu.
Maafisa hao walirusha gesi ya kutoa machozi na kufyatua risasi hewani kuwatawanya vijana hao waliokuwa wakipiga kelele na kurusha mawe.
Vurugu hizo zilianza wakati Profesa Kindiki alipokuwa akihutubia maafisa wa chama cha UDA kutoka vituo mbalimbali vya kupigia kura katika kaunti hiyo.
Alipokuwa akizungumza, vijana waliokuwa nje ya uwanja huo walianza kupaza sauti na kurusha mawe kwa lengo la kuvuruga mkutano huo. Wakati mmoja walijaribu kuvamia uwanja huo lakini walizuiwa na maafisa wa usalama.
Hatimaye polisi waliwarushia gesi ya kutoa machozi, hatua iliyozua mapambano ya kukimbizana kati yao na vijana hao yaliyodumu kwa saa kadhaa nje ya uwanja huku Kindiki akiendelea na hotuba yake bila kusitisha mkutano.
Baadaye, vijana hao walitawanyika lakini walikusanyika tena baada ya mkutano kumalizika na kuzua vurugu katika eneo hilo.
Walivamia barabara iliyo karibu, kuwashambulia madereva na wakazi huku wakichoma magari kadhaa, jambo lililozua hofu.
Miongoni mwa magari yaliyochomwa moto ni la mwanahabari wa eneo hilo. Mfuasi mmoja wa UDA pia alijeruhiwa usoni baada ya kupigwa na jiwe na kupatiwa huduma ya kwanza.