Habari

Gachagua afichua sababu kutotaja mwaniaji urais wa upinzani mapema

Na MWANGI MUIRURI September 13th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

KINARA wa chama cha Democracy for the Citizens Party (DCP), Rigathi Gachagua, amesema upinzani umeamua kuchelewesha kuunda afisi ya pamoja kwa sababu ya hofu ya kuingiliwa na serikali, huku akisisitiza kuwa lengo lao kuu ni kumng’oa Rais William Ruto mamlakani katika uchaguzi mkuu mwaka ujao.
Akizungumza Ijumaa jioni mbele ya wafuasi wake mjini Portland, Oregon, Amerika anakozuru, Bw Gachagua alidai Rais William Ruto atashindwa kwa tofauti ya kura zaidi ya milioni saba.
Alisema anatarajia kupokea simu kutoka kwa Rais Ruto usiku wa manane wa Agosti 10, 2027, akikubali kushindwa na kuomba kulindwa baada ya kuondoka madarakani.
Gachagua pia alidai Rais amepenyeza watu wake ndani ya baadhi ya makundi ya upinzani ili kupata taarifa za siri kuhusu mikakati yao.
“Majuzi tulikuwa katika kikao cha mkakati katika hoteli moja Nairobi. Kulikuwa na mmoja wa viongozi wa upinzani aliyekuwa amejiunga na muungano wetu akiwa na wanawake wawili. Hatukuwa hata tumemaliza kikao nilipoona taarifa ya kile tulichokuwa tunajadili ikiibuka kwenye simu yangu,” alisema.
Hata hivyo, alionya kuwa serikali ya upinzani haitawalinda wale watakaopatikana na makosa ya ufisadi, mauaji au utekaji nyara wa vijana waliokuwa wakishiriki maandamano.
“Nataka iwe wazi kuwa serikali ya upinzani haitawalinda wezi wa rasilimali za umma, wauaji au waliotekeleza utekaji nyara. Wote watawajibishwa kwa mujibu wa sheria,” alisema.
Gachagua pia alikanusha madai kwamba anapanga kukutana na Rais Ruto wakati wa ziara zao nchini Amerika. “Puuzeni propaganda zinazoenezwa kwamba nina nia ya kukutana na Rais Ruto hapa Amerika. Hilo halipo kabisa katika mipango yangu,” alisema.
Alieleza sababu ya kucheleweshwa kwa sekretarieti ya pamoja ya upinzani, Gachagua akisema ni rahisi kuvurugwa na serikali.