Habari

Ng’ombe, mbuzi na kondoo kupewa vitambulisho kudhibiti wizi

Na MERCY MWENDE September 13th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

SERIKALI imeanza kutekeleza mfumo mpya wa kitaifa wa kutambua na kufuatilia mifugo unaolenga kudhibiti wizi na kuboresha biashara ya bidhaa za mifugo nchini.
Waziri wa Kilimo na Maendeleo ya Mifugo, Mutahi Kagwe, alisema kila ng’ombe nchini atakuwa na alama maalum ya manjano ya mfumo wa Animal Identification and Traceability (ANITRAC) itakayowezesha kufuatilia alikotoka, afya yake na mahali alikopitia.
Akizungumza katika Maonesho ya Kilimo ya Kanda ya Kati ya Kenya mjini Nyeri, Bw Kagwe alisema mifugo itakayopatikana bila vitambulisho hivyo itazua maswali kuhusu usalama.
 “Katika siku zijazo kila ng’ombe atakuwa na alama maalum. Mtu akipatikana na ng’ombe asiye na alama hiyo atalazimika kueleza alikotoka,” alisema.
Mfumo huo pia unatarajiwa kusaidia serikali kufuatilia magonjwa ya mifugo na kuimarisha usalama wa chakula huku ukisaidia Kenya kutimiza masharti ya kimataifa ya masoko ya nje.
Waziri huyo pia alitangaza hatua za kupunguza gharama ya uzalishaji kwa wafugaji wa maziwa kupitia ruzuku ya mbegu za kisasa upatikanaji wa malisho bora na vifaa vya kupooza maziwa.
Aidha, alisema mageuzi katika sekta ya kahawa yanaendelea kutekelezwa kufuatia kuanza kazi kwa Bodi ya Kahawa ya Kenya. Kwa upande wa chai, ushuru mpya wa asilimia 0.8 kwa mauzo ya nje utasaidia kuboresha miundombinu na kuongeza thamani ya bidhaa hiyo.
Hata hivyo, aliwaonya wakulima dhidi ya kuvuna mazao kabla ya kukomaa, akisema hali hiyo huharibu sifa ya Kenya katika masoko ya kimataifa na kupunguza mapato ya wakulima.