Habari

Viongozi wa upinzani waeleza wasiwasi kuhusu kuenea kwa ghasia kuelekea 2027

Na WINNIE ATIENO September 14th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

VIONGOZI wa upinzani wakiongozwa na vinara wa Wiper Patriotic Front, Bw Kalonzo Musyoka, Democratic Party Bw Justin Muturi na mwenzao wa DAP-Kenya Bw Eugene Wamalwa, wameelezea wasiwasi wao kuhusu hali ya usalama nchini, wakionya kuwa ghasia za kisiasa zinaweza kuhatarisha uchaguzi mkuu wa 2027.

Viongozi hao walinukuu tukio la hivi majuzi kaunti ya Embu ambapo Naibu Rais Kithure Kindiki alilazimika kukimbilia usalama wakati wa mkutano wa hadhara baada ya kuzuka kwa ghasia.

Walisema tukio hilo limeibua maswali kuhusu usalama wa viongozi na Wakenya wa kawaida.

Bw Musyoka aliwataka Wakenya kuombeana amani, huku akiikosoa idara ya usalama kwa kile alichokitaja kuwa ni kumdhulumu Mbunge wa Manyatta Gitonga Mukunji kufuatia tukio hilo.

“Kama viongozi, tunalaani tukio hilo. Kuuzingira nyumba ya mbunge ni jambo la kusikitisha… kwa sababu tumeambiwa kwamba wakazi walisikia kuwa kulikuwa na pesa zikigawiwa, hivyo wakakimbilia kwenye mkutano kupata sehemu yao. Hilo ndilo lililosababisha vurugu, lakini kwa nini kumlaumu mbunge?” aliuliza.

Bw Musyoka alisema aliwahi kumtetea Bw Mukunji kama wakili wakati mbunge huyo alishtakiwa kwa kujihusisha na ugaidi.

“Alifikishwa mahakamani na kushtakiwa chini ya Sheria ya Kuzuia Ugaidi,” alisema, akiongeza kuwa Bw Mukunji hapaswi kudhulumiwa.

Alisema Bw Muturi atamtetea mbunge huyo.

Bw Musyoka alihoji hali ya usalama nchini, akisema tukio lililomhusisha Naibu Rais linaonyesha kuwa hata maafisa waandamizi wa serikali wako katika mazingira hatarishi.

“Tuombeane. Kwa kweli, kwa wakati kama huu, nchi yetu iko katika hali mbaya. Unapomwona Naibu Rais wa Jamhuri akikimbilia msituni kwa usalama, lazima ujiulize, usalama uko wapi? Ikiwa Naibu Rais anakimbilia msituni kwa usalama, raia wa kawaida ataenda wapi?” aliuliza Bw Musyoka.

Pia alirejelea tukio la hivi majuzi ambapo msafara wa viongozi wa upinzani ulipigwa mawe walipoingia Garissa.

“Tulikuwa na tukio Garissa, lakini tulikaribishwa vizuri sana Kaskazini Mashariki. Sasa tuko katika eneo la Pwani kuzungumza na Wakenya kuhusu changamoto zinazoikabili nchi hii,” alisema.

Bw Wamalwa alisema viongozi wa upinzani wameazimia kuendelea kutembelea maeneo mbalimbali nchini licha ya uhasama waliokumbana nao katika baadhi ya maeneo.

Alifananisha kuingia kwao Garissa na kuingia kwa Jeshi la Ulinzi la Kenya (KDF) Kismayu, Somalia, akisema walikumbana na upinzani kutoka kwa makundi aliyodai yalikuwa yamehamasishwa dhidi yao.

“Tulihangaika kuingia katika eneo hilo, kwa sababu hii ni timu ya Serikali Mbadala ya Umoja, upinzani wa kwanza kuingia Kaskazini Mashariki. Hata hivyo, serikali haikutaka tuende kueneza ujumbe wetu Kaskazini Mashariki,” alisema.

Bw Wamalwa alidai kuwa makundi yaliyowakabili yalikuwa yamehamasishwa na Serikali, madai ambayo hayakuweza kuthibitishwa kwa njia huru.

Alisema makabiliano kati ya upinzani na tukio la Embu yanapaswa kuwa onyo dhidi ya matumizi ya ghasia katika siasa.

“Hakuna mtu anayeweza kudhibiti uhuni,” alisema Bw Wamalwa, akitaja Haiti ambako alisema wanasiasa waliwahi kutegemea magenge kabla ya kuyapoteza kabisa mamlaka ya kuyadhibiti.

“Hatutaki kwenda katika njia hiyo; tunataka nchi yenye amani na uchaguzi wa amani. Wale walio serikalini, wale wanaotaka kupanda chui wa ghasia, mwishowe mtaliwa na huyo chui kwa sababu hamtakuwa na uwezo wa kudhibiti uhuni au ghasia,” alisema.

Bw Wamalwa aliwataka Wakenya kudumisha amani huku nchi ikielekea katika uchaguzi mkuu wa 2027.

“Ni lazima tuombee nchi hii, tuwe vyombo vya amani. Tunaelekea kwenye uchaguzi mkuu, zikiwa zimesalia miezi 10 pekee kabla ya uchaguzi. Wakenya wote waruhusiwe kuwachagua kidemokrasia viongozi wanaowataka madarakani,” alisema.

Aliwataka viongozi kuruhusu wanasiasa kufanya kampeni kwa uhuru katika maeneo yote ya nchi bila kujali misimamo yao ya kisiasa.

“Iwe uko muhula wa pili au wa kwanza, ni lazima tuwe mabalozi wa amani na tuchague yeyote tunayemtaka kidemokrasia. Hiyo ni haki yenu. Viongozi pia wanapaswa kuwa huru kutembelea sehemu yoyote ya nchi kutafuta kura,” alisema.

Bw Muturi alisema mazingira ya kisiasa nchini yamezidi kuwa yenye vikwazo, akidai kuwa maafisa wa usalama walizunguka kanisa ambako viongozi wa upinzani walikuwa wameenda kuomba.

“Kwa mara ya kwanza katika historia ya nchi, kanisa linazingirwa na maafisa wa usalama wenye silaha kwa sababu viongozi wa upinzani wameenda kuomba,” alisema.

“Hata wakati wa siku za giza za mfumo wa chama kimoja, haikuwahi kuwa hivi. Wakenya, tuombe kwa Mungu. Wakenya lazima wawe na uhuru wa kuwa na misimamo yao, kuieleza na kushirikiana na yeyote wanayemtaka. Hiyo ndiyo demokrasia,” alisema Bw Muturi.

Alimtetea Bw Mukunji, akisema mbunge huyo hapaswi kulaumiwa kwa vurugu zilizotokea Embu.

Bw Muturi alidai kuwa zaidi ya watu 20,000 walikusanyika baada ya kusikia kuwa pesa zilikuwa zikigawiwa katika mkutano huo.

Aliitaka serikali kuhakikisha usalama wa kutosha kwa wakenya wote na viongozi wa kisiasa huku nchi ikijiandaa kwa uchaguzi mkuu wa 2027.