Habari

Ruto atuliza ODM, aahidi kudumisha falsafa ya uongozi wa Raila Odinga

Na DOMNIC OMBOK September 14th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

RAIS William Ruto jana alionekana kupunguza mvutano wa kisiasa kati ya ODM na UDA, akisema vyama hivyo ni washirika katika Serikali Jumuishi akiahidi kulinda urithi wa kisiasa wa marehemu Raila Odinga.
Akizungumza jijini Kisumu, Rais Ruto alisema atashirikiana na ODM kuhakikisha maono na ndoto ya marehemu Raila kuhusu Kenya yanatimia.
“Nataka kuwahakikishia kama kiongozi wa taifa na kama mwanafunzi wa marehemu Raila Odinga kwamba tutatembea pamoja. ODM na UDA si washindani bali ni washirika katika Serikali Jumuishi,” akasema Dkt Ruto.
Alisema atahakikisha mchango wa Bw Odinga kwa Kenya unaendelea kukumbukwa, akimtaja aliyekuwa Waziri Mkuu kama mzalendo ambaye maono yake ya kisiasa yalikuwa si Nyanza pekee bali taifa zima.
“Kwa heshima ya ndugu yangu Raila Odinga, nitafanya kuwa jukumu langu kuhakikisha urithi wake, chama chake na yale aliyoyaamini yanaendelea tunaposhirikiana kujenga taifa,” akasema.
Dkt Ruto alikuwa akizungumza katika Kanisa la Voice of Salvation and Healing jijini Kisumu, mwanzoni mwa ziara yake ya Nyanza. Alikuwa ameandamana na Gavana wa Kisumu Anyang’ Nyong’o, Gladys Wanga (Homa Bay) , Ochilo Ayacko (Migori) na viongozi wengine wanaounga mkono serikali.
Kiongozi wa ODM Oburu Oginga hakuhudhuria, kwa sababu yuko Uingereza anakoendelea kupokea matibabu.
Rais alieleza uhusiano wake na Bw Odinga kuwa ulijengwa juu ya maono ya pamoja ya maendeleo, akitaja reli ya kisasa ya SGR, nyumba za gharama nafuu na ajira kama baadhi ya miradi waliyoibuni walipokuwa pamoja katika ODM.
“Nasimama hapa Kisumu, jiji la ndugu yangu marehemu Raila Amolo Odinga, ambaye najua angependa kuwa hapa Kisumu leo, mtu ambaye nilishirikiana naye kutekeleza maono makubwa ya Kenya,” akasema.
Dkt Ruto alisema SGR ni miongoni mwa miradi ambayo Bw Odinga angejivunia kuona ikiendelea. Alisema upanuzi wa reli kutoka Narok hadi Kisumu hatimaye utatimiza mojawapo ya malengo muhimu ya maendeleo ya Bw Odinga.
Gavana Wanga alisema Nyanza inashuhudia maendeleo makubwa chini ya serikali hiyo.
“Leo tunashuhudia maendeleo katika eneo hili kwa kiwango ambacho hatujawahi kuona,” akasema. Alikosoa kundi la Linda Mwananchi, akisema ODM imechagua kushirikiana na serikali ya Ruto ili kupata maendeleo kwa wakazi wa Nyanza.
 “Wapo watu ambao kazi yao pekee ni kutoka hoteli moja hadi nyingine ilhali hawana mgombea wala sera. Sisi katika serikali ya muungano mpana tuna mgombea,” alisema.