Polisi wapiga kambi katika boma la mbunge kuhusiana na ghasia za Embu
MAAFISA wa polisi waliojihami kwa silaha jana walizingira makazi ya Mbunge wa Manyatta Gitonga Mukunji huko Mutunduri, siku moja baada ya vijana wenye hasira kujaribu kuvuruga mkutano wa Naibu Rais Profesa Kithure Kindiki.
Baadhi ya maafisa hao walikuwa wamevalia nguo za kiraia na walikuwa wamejipanga kimkakati nje ya makazi ya mbunge huyo, wakidaiwa kusubiri kumkamata kufuatia ghasia zilizozuka wakati wa mkutano wa naibu rais katika Uwanja wa Nembure Jumamosi.
Maafisa hao walifika karibu saa 12 asubuhi na kuzingira makazi hayo, hali iliyozua hofu katika boma hilo. Walikaa hapo kwa saa kadhaa huku wakijaribu kubaini iwapo mbunge huyo alikuwa ndani.
Kufikia adhuhuri, maafisa hao walikuwa bado hawajaondoka. Juhudi za kumpata mbunge huyo ili kutoa maoni yake hazikufaulu kwani simu yake ilikuwa imezimwa.
Wakati wa ghasia za Jumamosi katika Uwanja wa Nembure, mtu mmoja alipigwa risasi na kuuawa na polisi huku magari sita yakichomwa.
Vijana walikuwa wakali baada ya polisi kuwazuia kuingia kwa nguvu uwanjani, ambako Profesa Kindiki alikuwa akihutubia maafisa wa UDA.
Kuzingirwa kwa makazi ya mbunge huyo kulitokea baada ya Profesa Kindiki kulaani vikali ghasia zilizovuruga mkutano wake.
Alisema UDA ilijutia vifo na uharibifu uliosababishwa na watu waliowapanga vijana kuvuruga mkutano huo.
“Ninalaani ghasia na kutaka vyombo vya usalama kuchukua hatua kali dhidi ya wote waliohusika kuchochea vurugu za kisiasa,” akasema.
Alisisitiza kuwa UDA inaunga mkono siasa zinazozingatia masuala na ushindani kuhusu ni chama gani kina rekodi bora ya maendeleo na sera nzuri kwa mustakabali wa Kenya, badala ya kulazimisha watu kuunga mkono kwa kutumia uongo, ghasia na kauli mbiu zisizo na maana.
“Uongozi wa chama chetu Embu umepewa jukumu la kuthibitisha hasara na uharibifu uliotokea, na kuratibu hatua za kuhakikisha tunasimama pamoja na wote walioathirika kwa njia moja au nyingine,” akasema.
Gavana wa Embu Cecily Mbarire alishutumu upinzani kwa kuhisi umeshindwa kuelekea uchaguzi wa 2027.
“Upinzani unajaribu kutuuzia hofu baada ya kutambua kuwa utashindwa katika uchaguzi wa 2027. Hatutanunua hofu hiyo,” Bi Mbarire alisema huku akimhusisha Bw Mukunji kupanga ghasia hizo.
Hata hivyo, mbunge huyo alijitetea akisema serikali inamtumia kama kafara.
“Haiwezekani kila mara wanilaumu kwa kupanga ghasia. Sijahusika kwa njia yoyote,” Bw Mukunji aliwaambia wanahabari mjini Embu Jumamosi.
Kwa upande mwingine, wanahabari wa Embu walilaani ghasia hizo ambapo magari mawili yaliyokuwa yakitumiwa na wanahabari yalichomwa.
Wanahabari hao, wakiongozwa na mwenyekiti wa Muungano wa Wanahabari Embu Brian Malila, walisema usalama wa wanahabari lazima ulindwe katika kila mkutano wa hadhara au wa kisiasa.
“Muungano huu umeshtushwa na ghasia na uharibifu ulioshuhudiwa katika Uwanja wa Nembure wakati wa mkutano wa wajumbe wa UDA,” akasema Bw Malila.