Habari

Kauli mbiu ya Wantam yatawala Nairobi Sifuna akitamba jijini

Na KEVIN CHERUIYOT na MOSES NYAMORI September 14th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

SENETA wa Nairobi, Edwin Sifuna na viongozi wa Linda Mwananchi jana walitikisa Jiji Kuu la Nairobi kupitia misururu ya mikutano mikubwa iliyovumisha ujumbe wa kumbandua Rais William Ruto madarakani mnamo 2027.
Ziara hiyo ilitumiwa kama ratili ya kuonyesha ushawishi wa kisiasa wa Bw Sifuna jijini, huku idadi kubwa ya waliojitokeza ikiashiria kuunga mkono vuguvugu hilo.
Tofauti na mikutano ya awali ya kundi hilo Homa Bay na Kisumu, ambako kulishuhudiwa vurugu, mkutano wa Nairobi ulikuwa wa amani polisi wakitoa usalama.
Bw Sifuna aliandamana na Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino, Seneta wa Vihiga Godfrey Osotsi na Gavana wa Siaya James Orengo, Gavana wa Trans Nzoia George Natembeya miongoni mwa viongozi wengine.
Viongozi hao walianza ziara yao kwa kuhudhuria ibada katika Kanisa la All Saints Cathedral kabla ya kupitia masoko ya Marikiti na Gikomba hadi Uwanja wa Jacaranda.
Wakiwa Gikomba, waliwataka wapiga kura kumng’oa Rais Ruto madarakani katika uchaguzi wa 2027, wakishutumu serikali yake kwa udikteta na kutowajali wananchi wa kawaida.
Bw Sifuna alisema mapokezi waliyopata Nairobi ni ishara kwamba Wakenya wamekerwa na uongozi wa Kenya Kwanza.
“Ruto hajafahamu ujumbe wetu. Mitaa ya mabanda Nairobi si tatizo la nyumba bali ni tatizo la mapato. SHA haifanyi kazi na ndiyo maana hata Rais bado anatoa pesa katika michango ya harambee, jambo ambalo aliahidi wakati wa kampeni kulikomesha,” akasema Bw Sifuna.
 Seneta huyo alisema anahitaji uungwaji mkono wa wakazi wa Nairobi katika azma yake ya kuwania urais, lakini akasisitiza kuwa kumng’oa Dkt Ruto kutahitaji nguvu za pamoja za viongozi wa upinzani.
Alitaja kiongozi wa DCP Rigathi Gachagua, Kalonzo Musyoka wa Wiper Patriotic Front na naibu kiongozi wa Jubilee Fred Matiang’i miongoni mwa viongozi ambao wanapaswa kuungana.
“Watu katika maeneo mengine ya nchi wanataka kunipeleka kwenye kazi fulani. Je, nyinyi pia mnataka niende kwenye kazi hiyo? Haitakuwa rahisi. Lazima tutembee pamoja na Kalonzo Musyoka, Rigathi Gachagua na viongozi wengine wote wa upinzani,” akasema
Nairobi ina maeneobunge 17, wadi 85 na zaidi ya wapiga kura milioni 2.7 waliosajiliwa. Idadi hiyo inatarajiwa kufikia milioni 3.1 katika uchaguzi wa 2027, hivyo kuifanya Nairobi kuwa muhimu kwa yeyote anayelenga kuingia Ikulu.
Bw Sifuna pia alieleza sababu ya kutofautiana kwake na Kiongozi wa ODM Dkt Oburu Oginga, akisema hawezi kukubali kumuunga mkono Dkt Ruto kutokana na kile alichodai kuwa ni kuongezeka kwa gharama ya maisha.
Linda Mwananchi inalenga kurithi maeneo ya uungwaji mkono ya marehemu Raila Odinga, ikidai kundi la Dkt Oginga limeharibu falsafa ya uongozi wa mwanasiasa huyo mkongwe wa upinzani.
Kwa miongo kadhaa, Bw Odinga alikuwa na ushawishi mkubwa Nairobi, jiji ambalo lilikuwa nguzo muhimu ya miungano yake ya kitaifa.
Katika mkutano wa jana, viongozi wa Linda Mwananchi pia walionya kuwa hawatasita kupinga matokeo ya uchaguzi katika Mahakama ya Juu iwapo yatachakachuliwa.
Gavana wa Trans Nzoia George Natembeya alidai Mahakama ya Juu iliwahi kutumiwa kumnyima Bw Odinga ushindi wa urais.
Bw Odinga alipinga matokeo ya uchaguzi wa 2013, 2017 na 2022. Mnamo 2017, Mahakama ya Juu chini ya aliyekuwa Jaji Mkuu David Maraga ilibatilisha ushindi wa Rais Uhuru Kenyatta na kuamuru uchaguzi mpya.
Katika Uwanja wa Jacaranda, viongozi hao pia walimpigia debe Bw Babu Owino kuwania ugavana wa Nairobi.
Walimshtumu Gavana Johnson Sakaja kwa kushindwa kutatua matatizo ya wakazi wa Nairobi licha ya kaunti hiyo kupokea mgao mkubwa zaidi wa fedha kutoka kwa serikali kuu.
Bw Owino alisema Bw Sakaja amelemewa na majukumu na akadai kuwa makubaliano ya Sh80 bilioni kati ya kaunti na serikali kuu yalilenga kuficha uzembe wa utawala wake.
“Wakazi wa Nairobi huamka kila siku na kukabili jiji chafu kwa sababu Sakaja hawezi kulisafisha jiji. Hilo litakuwa jambo la zamani chini ya uongozi wangu,” akasema Bw Owino.
Viongozi wengine waliohudhuria mkutano huo, Seneta wa Kakamega Boni Khalwale, Seneta Crystal Asige, aliyekuwa Gavana wa Meru Kawira Mwangaza, aliyekuwa Rais wa LSK Faith Odhiambo na Wakili Laureen Mogotsi ambaye analenga kiti cha Ubunge Ikolomani Kaunti ya Kakamega.