Habari za Kaunti

Ukuta waangukia nyumba na kuua wanafamilia wawili baada ya mvua kubwa Mombasa

Na WINNIE ATIENO September 14th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WATU wawili walifariki baada ya ukuta kuangukia nyumba katika eneo la Jomvu, Kaunti ya Mombasa, usiku wa kuamkia Jumatatu.

Bi Clemence Saru, aliyepoteza mume na mtoto wake katika kisa hicho, alieleza kwamba alikuwa katika kanisa la Anointed Rock Ministry kwa maombi wakati aliposikia kishindo kikubwa.

Alitoka kanisani ili kujua kilichokuwa kimetokea kisha akasikia kilio cha mumewe na watoto wao wakimwomba msaada.

Dakika chache baadaye, vilio hivyo vilikoma, hali iliyothibitisha hofu yake kubwa zaidi.

Ukuta wa uzio wa kampuni ya Cevas Logistics uliangukia nyumba yake katika kijiji cha Cambodia, Jomvu, na kumuua mumewe pamoja na mwanao walipokuwa wamelala majira ya saa tano na dakika 20 usiku.

Mtoto wao mwingine alinusurika lakini alijeruhiwa na kupelekwa katika Hospitali ya Mikindani Medical na majirani.

Kamanda wa Polisi wa Kaunti ya Mombasa Stella Cherono, alithibitisha kisa hicho.

Janga hilo limeibua upya wasiwasi miongoni mwa wakazi wanaoishi karibu na kituo cha kuhifadhi na kusafirisha makontena (CFS), ambao wanasema sehemu za ukuta wake wa uzio zimeanguka mara kadhaa hapo awali.

Wakazi walisema mvua kubwa iliyonyesha katika eneo la Pwani wiki iliyopita huenda ilidhoofisha zaidi ukuta huo.

Bw Peter Ulinda, mkazi, alisema alikuwa amelala aliposikia kishindo.

“Nilitoka mbio na kumwona jirani yangu akilia akiomba msaada baada ya ukuta kuangukia nyumba yake. Mama alikuwa kanisani akiomba wakati ukuta ulipoanguka juu ya nyumba yake, na kumuua mumewe pamoja na mtoto mmoja. Inasikitisha sana,” alisema Bw Ulinda.

Alisema majirani walikimbilia kuwaokoa waathiriwa na kuwapeleka hospitalini, lakini wawili walikuwa tayari wamefariki.

“Polisi walifika saa tatu baadaye baada ya sisi kufanya kila kitu,” alisema.

Bw Ulinda alisema wakazi walikuwa wameibua wasiwasi kuhusu ukuta huo.

“Hii ni mara ya nne kwa ukuta huu kuanguka na hatujawahi kufidiwa licha ya watu wetu kujeruhiwa. Tuna ushahidi. Katika tukio la mwisho, jirani yetu alijeruhiwa na hadi leo hajawahi kuwa kama alivyokuwa awali,” alisema.

Bw Ulinda pia aliachwa bila makao baada ya ukuta huo kuharibu nyumba yake.

Mkazi mwingine, Bi Chenda Baya, alisema mwanawe alijeruhiwa wakati ukuta huo ulipoanguka mwaka jana lakini familia hiyo haikuwahi kufidiwa.

Wasiwasi wa wakazi hao umejitokeza wakati nchi ikijiandaa kukabiliana na mvua kubwa zinazohusishwa na hali ya El Niño, hali inayozua hofu kuhusu usalama wa majengo katika maeneo ambayo tayari yanachukuliwa kuwa hatarini kukumbwa na mafuriko na hatari nyingine zinazohusiana na hali ya hewa.

Viongozi wa eneo hilo wakiongozwa na Bw Beuta Mogaka waliitaka Serikali ya Kaunti ya Mombasa kukagua majengo na kuta katika kaunti nzima ili kuhakikisha zinakidhi viwango vya usalama.

Bw Mogaka alisema mazingira yaliyopelekea ukuta huo kuanguka yanapaswa kuchunguzwa na hatua kuchukuliwa dhidi ya waliohusika iwapo itabainika kuwa kulikuwa na makosa.

Mwanaharakati wa kutetea haki za binadamu, Bw Mathias Shipeta pia alitaka uwajibikaji, akihoji iwapo kanuni za ujenzi zilifuatwa.

Mzee wa kijiji, Bi Sally Wawuda, aliwataka wakazi wanaoishi karibu na kituo hicho cha mizigo kuzingatia kuhama eneo hilo kutokana na kile alichokielezea kuwa ni hatari inayokaribia.

Kanisa la Anointed Rock Ministry lililokuwa karibu, pia liliathiriwa ambapo sehemu ya ukuta wa kanisa iliharibiwa.