Serikali yadumisha bei za mafuta licha ya gharama kupanda kimataifa
MAMLAKA ya Kudhibiti Kawi na Petroli (EPRA) jana ilitangaza kuwa bei ya mafuta itasalia jinsi ilivyo mwezi huu hadi Oktoba 14, 2026.
Licha ya mabadiliko ya bei za mafuta katika soko la kimataifa na gharama ya kuyafikisha nchini, EPRA ilisema bei za sasa zitaendelea kutumika katika maeneo mbalimbali nchini.
Nairobi, lita moja ya Petroli itaendelea kuuzwa kwa Sh214.03, dizeli Sh217.86 na mafuta ya taa Sh191.38.
Mombasa, Super Petrol itauzwa kwa Sh210.87 kwa lita, dizeli Sh214.58 na mafuta ya taa Sh188.09.
Nakuru, lita moja ya petroli itagharimu Sh212.92 na dizeli Sh217.27, huku Eldoret na Kisumu petroli ikiuzwa kwa Sh213.69 kwa lita.
Bei hizo zinajumuisha VAT, kwa mujibu wa Sheria ya VAT ya 2013, pamoja na marekebisho ya kodi yaliyoainishwa katika sheria mbalimbali za kodi na viwango vipya vya ushuru wa bidhaa vilivyorekebishwa kulingana na mfumuko wa bei.