Mawimbi yakumba ukumbusho wa Raila
CHAMA cha ODM na familia ya aliyekuwa Waziri Mkuu Raila Odinga, wako katika mzozo mkali kuhusu mipango ya kuadhimisha mwaka mmoja tangu kifo chake.
Taifa litaadhimisha mwaka mmoja tangu kifo cha Raila mnamo Oktoba 15. Raila alifariki siku hiyo baada ya kupata mshtuko wa moyo mjini Kochi, India.
Katika taarifa iliyotolewa Jumapili, familia hiyo ilisema kumbukumbu hiyo si ya mtu binafsi wala taasisi yoyote, siku chache tu baada ya ODM kutangaza mipango ya misururu ya mikutano kote nchini kwa ajili ya kumuenzi mwanzilishi wake.
Taarifa hiyo ilisambazwa kwenye mitandao ya kijamii na binti wa Raila, Winnie Odinga, na dada yake Ruth Odinga, ambaye pia ni Mwakilishi wa Kike wa Kisumu.
Lakini Raila Junior, mwanawe Raila ambaye baada ya kutangaza nia ya kuwania ubunge wa Kibra amekuwa akiandamana na viongozi wa ODM katika mikutano ya kisiasa, hakusambaza taarifa hiyo kwenye mitandao yake ya kijamii.
Raila Junior pia ameandamana na viongozi hao katika ziara ya siku tatu ya Rais William Ruto eneo la Nyanza.
Aidha, mama yake, Ida Odinga, ambaye kwa sasa ni Balozi wa Kenya na Mwakilishi wa Kudumu katika Shirika la Umoja wa Mataifa la Mazingira (UNEP) baada ya kuteuliwa na Rais Ruto mapema mwaka huu, hakusambaza taarifa hiyo.
Hata hivyo, jana jioni Winnie alikanusha kuwa kuna uhasama kati ya chama na familia kuhusu maadhimisho hayo.
Aliambia Taifa Leo kuwa kumteua Prof Adams Oloo kusimamia maandalizi ya ukumbusho huo ni njia ya kuhakikisha kwamba hakuna anayefungiwa nje kushiriki maadhimisho ya Raila.
“Sidhani kama kuna mzozo. Hakuwezi kuwa na mzozo kuhusu maadhimisho,” akasema.
Alisema wazo la kuwa na hafla inayoshirikisha wote itawaleta wandani na waliokuwa wapinzani wa marehemu Raila pamoja.
“Hatutaki iwe siku ambayo watu wanazuiwa kwa sababu watu hawakupata muda wa kumwomboleza,” akaongeza.
Winnie na Ruth wamekuwa wakikosoa namna ODM inavyoendeshwa baada ya kifo cha Raila.
Katika baadhi ya matukio, wawili hao wamewashutumu hadharani baadhi ya viongozi wa chama hicho wakidai wanalemaza umaarufu wake.
Taifa Leo ilipowasiliana na Ruth, ambaye kwa sasa yuko London pamoja na kaka yake aliye pia kiongozi wa ODM, Oburu Oginga, ili kujua iwapo familia hiyo ina tatizo kuhusu ratiba na mpango uliotangazwa na ODM, alikataa kutoa maoni.
Badala yake, alimwelekeza mwandishi kwa Winnie, ambaye hakujibu maswali yaliyotumwa kwake.
Awali, Ruth aliwataja baadhi ya viongozi wa chama hicho ambao hakuwataja majina, kuwa wanalenga kutumia maadhimisho hayo kujinufaisha kisiasa.
“Tunaelekea Oktoba 15 na tayari watu wa vikombe na mahema ya ODM wanapanga mambo yao. Raila alikuwa mtu wa kipekee! Acheni upuuzi!” akasema Ruth.
Katika taarifa yao, familia ilisema imemteua Prof Adams Oloo kuongoza kamati itakayoratibu shughuli za kumuenzi Raila mwezi ujao.
“Kwa hivyo, tunataka kumbukumbu hii ya kwanza iwe wakati wa wananchi kuwa na Baba yao, kumkumbuka, kumuomboleza, kusherehekea maisha yake na kuheshimu safari waliyoshiriki pamoja naye,” ikasema taarifa ya familia.
“Kamati hii kwa sasa inaandaa mpango ambao familia itautangaza kwa wakati unaofaa. Yeyote anayetaka kushiriki, kusaidia au kuandaa shughuli yoyote kama sehemu ya kumbukumbu hiyo anaombwa kufanya hivyo kupitia kamati,” ikaeleza.
ODM, wiki iliyopita ilitangaza misiruru ya mikutano ya kisiasa ya kumuenzi marehemu Raila ikilenga kuitumia kuvumisha chama kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027.
Kwa mujibu wa chama hicho, mikutano hiyo itafanyika Siaya, Kakamega, Garissa, Mombasa, Kajiado, Turkana na hatimaye Nairobi. Maeneo hayo yalikuwa ngome za kisiasa za Raila.
“Kuanzia Bondo hadi Garissa, kutoka Kakamega hadi Nairobi na kila sehemu nchini Kenya, tutamheshimu mtu aliyetufundisha kwamba mamlaka ni ya wananchi,” akasema Mwenyekiti wa kitaifa wa ODM na Gavana wa Homa Bay Gladys Wanga.
Mnamo Oktoba 9, wafuasi wa ODM kutoka Kakamega, Vihiga, Busia, Bungoma na Trans Nzoia watakutana Kakamega mjini kwa mkutano mkubwa wa kumuenzi Bw Odinga.
Hii itafuatwa na shughuli zinazoongozwa na familia katika Kang’o Ka Jaramogi, Bondo, kuanzia Oktoba 10 hadi 15.
Chama hicho kitafanya mkutano mwingine wa kumbukumbu Garissa Oktoba 17, huku viongozi wa ODM, wanachama na wafuasi kutoka Garissa, Wajir, Mandera, Isiolo na Marsabit wakitarajiwa kuhudhuria.