Habari za Kitaifa

Oburu asafiri Uingereza kwa matibabu, ODM ikitoa ratiba ya ukumbusho wa Raila

Na NDUBI MOTURI September 11th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

KIONGOZI wa ODM, Oburu Oginga, amesafiri Uingereza kwa uchunguzi wa kawaida wa afya huku akitarajiwa kushiriki shughuli za kisiasa na Wakenya wanaoishi nchini humo.

Safari hiyo imejiri wakati ambapo chama cha ODM kimezindua ratiba ya shughuli za mwezi mzima za kumuenzi marehemu Raila Odinga, ambazo zitafanyika katika sehemu mbalimbali za nchi hadi mwishoni mwa Oktoba.

Mkurugenzi wa Mawasiliano wa ODM, Philip Etale, alisema kuwa safari ya Dkt Oburu haipaswi kutafsiriwa kama jambo la dharura la kiafya kwani ni ukaguzi wa kawaida ambao kiongozi huyo hufanyiwa mara kwa mara.

Alifafanua kuwa Dkt Oburu, ambaye wiki iliyopita alionekana katika hospitali moja jijini Nairobi kwa matibabu ya kawaida, ameelekea Uingereza kwa uchunguzi zaidi pamoja na majukumu ya kisiasa.

“Oburu ni binadamu wa kawaida kama wengine. Ameenda kwa ukaguzi wa afya pamoja na shughuli za kisiasa,” alisema Bw Etale.

Kwa mujibu wa afisa huyo wa ODM, Dkt Oburu pia anapanga kukutana na Wakenya wanaoishi jijini London ambao wamemualika kwa mazungumzo kuhusu hali ya kisiasa nchini Kenya na mustakabali wa taifa kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2027.

“Watakuwa na mazungumzo kuhusu nchi yetu na masuala mbalimbali yanayohusu Kenya,” aliongeza Bw Etale.

Safari hiyo imezua mjadala kutokana na historia ya changamoto za kiafya ambazo zimewahi kumkumba kiongozi huyo mwenye umri wa miaka 83.

Hata hivyo, ODM imesema hakuna sababu ya kuwa na wasiwasi kwani ratiba yake ya afya na shughuli za kisiasa zinaendelea kama kawaida.

Tangazo la safari ya Dkt Oburu limejiri huku chama hicho kikitangaza mpango wa kitaifa wa kumuenzi Raila Odinga, ambaye ODM inamtaja kama mmoja wa viongozi waliotoa mchango mkubwa katika kupigania demokrasia na haki za kisiasa nchini.

Mbunge wa Kisumu Magharibi, Bi Rosa Buyu, alisema shughuli hizo zitatoa nafasi kwa wanachama na wafuasi wa ODM kuadhimisha maisha, kazi na maadili ya Raila huku wakijitolea upya kuyasimamia.

Ratiba hiyo itaanza rasmi Oktoba 12 kupitia shughuli zitakazoandaliwa na familia ya Raila kabla ya kufikia kilele katika hafla ya kumbukumbu itakayofanyika Kango Ka’Jaramogi huko Bondo.

Baadaye, Oktoba 17, chama hicho kitafanya mkutano mkubwa wa kumbukumbu katika mji wa Garissa utakaowaleta pamoja wanachama na viongozi kutoka kaunti za Garissa, Wajir, Mandera na Marsabit.

Vilevile, shughuli za kumbukumbu zitafanyika katika eneo la Pwani kati ya Oktoba 18 na 19 kabla ya taifa kuadhimisha Siku ya Mashujaa Oktoba 20.

Baada ya hapo, shughuli hizo zitaendelea Kaunti ya Kajiado Oktoba 21 kabla ya Turkana ambako mikutano mbalimbali itafanyika kuanzia Oktoba 23 hadi 25.

ODM imesema lengo la ratiba hiyo ni kupeleka urithi wa Raila katika maeneo mengi ya nchi na kuwafikia wafuasi nje ya ngome za jadi za chama hicho.

Hii ni pamoja na maeneo ya Kaskazini mwa Kenya, Pwani, Kajiado na Turkana.

Shughuli zote zitahitimishwa Oktoba 31 jijini Nairobi katika mkutano mkubwa wa kumbukumbu ambao ODM imetaja kama kilele cha maadhimisho ya “Mwezi wa Baba”.

“Mnamo Oktoba 31, 2026, ambao ni mwezi wa Baba, tutakuwa na mkutano mkubwa wa kumbukumbu Nairobi. Tunawaomba wafuasi wote kujitolea upya kwa maadili na misingi aliyotuachia Baba,” alisema Buyu.