Korti yampiga marufuku Uhuru kuendelea kushikilia uongozi wa Jubilee na Azimio
MAHAKAMA Kuu imesisitiza kuwa sheria inayomzuia Rais mstaafu kushikilia wadhifa wa uongozi katika chama cha kisiasa kwa zaidi ya miezi sita baada ya kuondoka mamlakani ipo na utekelezaji wake unastahili kuzingatiwa.
Uamuzi huo unaweza kuathiri nafasi ya Rais Mstaafu Uhuru Kenyatta kuendelea kuwa Kiongozi wa Jubilee na muungano wa Azimio.
Jaji Lawrence Mugambi alitupilia mbali ombi lililopinga Kifungu cha 6(1) cha Sheria ya Marupurupu ya Marais Wastaafu, akisema sheria hiyo haimzuii rais mstaafu kuwa mwanachama wa chama au kushiriki shughuli za kisiasa.
Hata hivyo, inamzuia kushikilia nafasi ya uongozi wa chama kwa zaidi ya miezi sita baada ya kustaafu.
“Kinachozuiwa ni kushikilia nafasi ya uongozi katika chama hicho kwa zaidi ya miezi sita baada ya kustaafu,” akasema Jaji.
Uamuzi huo unaangazia upya mzozo wa uongozi wa Jubilee ambao uliibuka baada ya Bw Kenyatta kustaafu Septemba 2022.
Bw Kenyatta amekuwa kiongozi wa Jubilee tangu chama hicho kilipoanzishwa mnamo 2017 na aliendelea kushikilia nafasi hiyo baada ya kuondoka ikulu.
Mnamo 2023, kundi la wanachama wa Jubilee lilitangaza nafasi yake kuwa wazi na kumteua Mbunge Maalum Sabina Chege kuwa kiongozi wa muda, likitaja sheria hiyo.
Hatua hiyo ilisababisha mzozo kuhusu nani alikuwa na mamlaka ya kuitisha mikutano ya chama, kuwaondoa maafisa na kuwasiliana na Msajili wa Vyama vya Kisiasa.
Bw Kenyatta na washirika wake walipinga mabadiliko hayo, wakisema yalikiuka katiba ya chama. Hata hivyo, Msajili alimtambua Bi Chege kama kiongozi na Mbunge wa EALA Kanini Kega kama katibu mkuu.
Bw Kenyatta alirejea uongozi wa Jubilee Juni 2025 baada ya Mahakama kubatilisha uamuzi uliomweka Bi Chege na kundi lake mamlakani.
Wakati huo huo, Bw Kenyatta pia ni mwenyekiti wa Baraza la Muungano wa Azimio la Umoja-One Kenya, jambo ambalo limekuwa likizua malalamishi kutoka kwa washirika wa Rais William Ruto wanaomshutumu kwa kuendelea kujihusisha kikamilifu na siasa.
Kesi iliyosababisha uamuzi wa sasa iliwasilishwa Mei 2023 na wanaharakati Peter Odhiambo Agoro, Paul Muiruri Kiguathi na Damon Onyango Osawa.
Walidai sheria hiyo inawabagua marais wastaafu na kukiuka haki za usawa, uhuru wa kujumuika na kushiriki siasa.
Mahakama, hata hivyo, ilisema haki hizo si kamili na zinaweza kuwekewa mipaka chini ya Katiba iwapo vizuizi hivyo ni vya busara na vinavyoweza kuhalalishwa katika jamii ya kidemokrasia.
Jaji Mugambi alisema rais mstaafu ana nafasi ya kipekee kutokana na mamlaka na ushawishi aliokuwa nao alipokuwa madarakani.
Mahakama pia ilisema sheria hiyo iliyopitishwa 2003 ililenga kuzuia marais wastaafu kuendelea kudhibiti siasa kupitia washirika wao baada ya kuondoka mamlakani.