Siasa

Wanasiasa vuguvugu Nyanza waanza kuhisi joto wapigakura wakiwataka kuchukua msimamo

Na CECIL ODONGO September 15th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

VIONGOZI wa ODM ambao wamekuwa na msimamo vuguvugu katika kuunga mkono azma ya Rais William Ruto kuwania muhula wa pili wameanza kuhisi joto kutoka kwa wapigakura wa Nyanza, wanaowataka wachukue msimamo wa wazi kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027.

Mbunge wa Suba Kaskazini, Millie Odhiambo, alizomewa Jumapili jijini Kisumu, hali iliyoonyesha kutoridhika kwa baadhi ya wapigakura na viongozi wanaoonekana kuegemea upande wa upinzani na wakati huo huo kushirikiana na Serikali Jumuishi.

Bi Odhiambo, ambaye anahudumu muhula wake wa nne na pia ni Kiranja wa Wachache katika Bunge la Kitaifa, alikumbana na wakati mgumu alipokuwa akihutubia wakazi wa Kisumu katika mkutano wa Rais Ruto na viongozi wa Nyanza.

Baadhi ya wakazi walimpigia kelele wakisema, “Ondoka, toka hapa,” huku wengine wakimwambia, “Wewe kaa tu kwenye fensi.”

“Wale wanaomuunga mkono Ruto inueni mikono. Kitu kizuri kinaporudiwa huwa kizuri zaidi. Mimi Amillo gesa gesa, mnanipigia kelele. Nilizaliwa nikiwa mkaidi na ninamuunga mkono Ruto jinsi ninavyotaka. Na ninawaambia sijali,” akasema Bi Odhiambo.

Baadaye mbunge huyo aliandika kwenye mitandao ya kijamii akisema alifedheheshwa na kuzomewa huko Kisumu.

“Leo nilizomewa sana Kisumu. Tangu wakati huo, niko kwenye chumba cha kuhifadhi maiti, nimekufa. Ninasubiri yanayofuata. Hata hivyo, nilikuwa mjanja sana. Kubali tu ulale,” akaandika.

Mbali na Bi Odhiambo, viongozi wengine ambao hawajakuwa na msimamo ni Mbunge wa Rarieda Otiende Amollo, Mbunge wa EALA Winnie Odinga, Seneta wa Homa Bay Moses Kajwang’ na Mbunge Mwakilishi wa Kike wa Kisumu Ruth Odinga.

Mabw Kajwang’ na Amollo walihudhuria mkutano huo na kuunga mkono azma ya Rais Ruto ya muhula wa pili.

“Kama Mzee Oburu angekuwa hapa angesema tunataka mamlaka kwa sababu hatuwezi kuwa bila mamlaka. Rais, tunataka kukuunga mkono kwa yale ambayo umefanyia eneo letu, unayofanya na unayonuia kufanya kwa eneo letu. Tutakuunga mkono bila masharti kwa maendeleo ambayo umetuletea,” akasema Bw Kajwang’.

Wiki mbili zilizopita, Bw Kajwang’ pia alimuunga mkono mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino kuwania ugavana wa Nairobi.

Kwa upande wake, Bw Amollo alisema anaunga mkono Rais Ruto bila masharti kutokana na heshima yake kwa marehemu Raila Odinga, miradi ya maendeleo inayoendelea na upanuzi wa reli ya kisasa ya SGR hadi Kisumu.

Hapo awali, Bw Amollo alilazimika kutetea msimamo wake wa kutoonekana kuunga mkono serikali, akisema bado ni mwanachama mwaminifu wa ODM.

Bi Winnie Odinga amekuwa kimya na hajaonekana katika baadhi ya mikutano muhimu ya kisiasa ya ODM.

Bi Ruth Odinga hakuhudhuria mkutano wa Kisumu kwa kuwa ameandamana na Dkt Oburu Oginga nchini Uingereza kwa uchunguzi wa kawaida wa afya.

Gavana wa Siaya James Orengo na Mbunge wa Suba Kusini Caroli Omondi ni miongoni mwa viongozi wachache wa ODM wanaopinga waziwazi azma ya Rais Ruto ya kuwania muhula wa pili.

Kura ya maoni ya TIFA iliyotolewa Julai 26 ilionyesha Rais Ruto akiwa mgombea maarufu zaidi Nyanza kwa asilimia 30.

Mchanganuzi wa masuala ya kisiasa Javas Bigambo alisema viongozi wanaokwepa kuchukua msimamo wanaweza kukumbana na shinikizo kubwa kutoka kwa wapigakura.

“Kilichompata Millie kinaonyesha kuwa wale wanaokaa kwenye uzio wameketi juu ya bomu linalosubiri kulipuka na wapigakura hawaridhishwi nao. Wapigakura wanataka wapiganaji na huwezi kosa kuwa upande wowote wakati wa vita,” alisema Bw Bigambo.

“Hata mgombea huru anaweza kumshinda anayekaa kwenye uzio kwa sababu ana msimamo. Kwa Millie, baadhi ya kauli ambazo amekuwa akitoa zimefasiriwa kuwa zinaunga mkono kundi la Linda Mwananchi,” akaongeza.