Kujiondoa kwa Uhuru kwafungua vita vya ubabe Jubilee kati ya Matiang’i na Kioni
CHAMA cha Jubilee kimetumbukia katika vita vipya vya uongozi huku aliyekuwa Rais Uhuru Kenyatta akijiandaa kuacha rasmi uongozi wa chama hicho baada ya Mahakama Kuu kuamua kuwa marais wastaafu hawawezi kuendelea kushikilia nyadhifa za uongozi wa vyama zaidi ya miezi sita baada ya kuondoka Ikulu.
Uamuzi huo umefungua mapambano mapya ya kumrithi Bw Kenyatta, huku Naibu Viongozi wa Jubilee Jeremiah Kioni na Fred Matiang’i wakiwa miongoni mwa wanachama muhimu katika mchuano huo.
Kiini cha mzozo huo si kiti cha kiongozi pekee, bali pia udhibiti wa mtandao wa chama, mali, fedha na ushawishi wa kisiasa kuelekea Uchaguzi Mkuu wa 2027.
Bw Kioni Jumanne alitangaza nia yake ya kuwania wadhifa wa Kiongozi wa Jubilee, siku moja tu baada ya Bw Kenyatta kutangaza atasalimisha uongozi wa chama.
Katika taarifa yake, Bw Kenyatta alisema yuko tayari kukabidhi uongozi wa Jubilee kupitia mchakato unaozingatia katiba ya chama.
Bw Kenyatta alikuwa amebaki katika uongozi wa Jubilee licha ya mzozo wa ndani uliochelewesha mabadiliko.
Mnamo Machi 2025, alirejea kudhibiti chama hicho baada ya mapambano ya muda mrefu kati ya makundi hasimu.
Hata hivyo, uamuzi wa Jaji Lawrence Mugambi sasa umefanya kuondoka kwake kuwa suala la kisheria badala ya uamuzi wa kisiasa.
Jaji Mugambi alifafanua kuwa marais wastaafu hawazuiwi kuwa wanachama wa vyama au kushiriki shughuli za kisiasa.
Kilichozuiwa ni kushikilia rasmi uongozi wa chama baada ya muda uliowekwa.
Uamuzi huo umeacha Jubilee katika mchakato nyeti wa kutafuta atakayechukua nafasi ya Bw Kenyatta na kuamua mwelekeo wa chama kabla ya uchaguzi ujao.
Bw Kioni sasa anataka uongozi huo upatikane kupitia Kongamano la Kitaifa la Wajumbe (NDC), akipinga uwezekano wa kiongozi mpya kupitia makubaliano ya ndani.
“Jubilee ni chama cha kitaifa na kilikuwa chama tawala. Kwa hivyo, viongozi wetu hawateuliwi, wanachaguliwa na wajumbe katika Kongamano la Kitaifa la Wajumbe,” alisema.
Kauli hiyo imeleta mtazamo tofauti kuhusu urithi wa chama, hasa ikizingatiwa kuwa Bw Matiang’i tayari ndiye mgombea urais wa Jubilee wa 2027.
Baadhi ya wafuasi wa Bw Matiang’i walitarajia kuwa hadhi yake ya kisiasa pamoja na uteuzi wake kuwa mgombea urais ungemweka katika nafasi nzuri ya kurithi uongozi wa chama baada ya Bw Kenyatta.
Lakini kuibuka kwa Bw Kioni kumefanya swali hilo kuwa tata zaidi.
Mmoja wa watu wa karibu na chama alisema nafasi ya kiongozi wa chama na mgombea urais ni tofauti, na kwamba mmoja hawezi kumpisha mwingine moja kwa moja.
“Uzuri wa Jubilee ni kwamba, kiongozi wa chama anapoondoka, manaibu wawili wana haki, nafasi na uwezo sawa wa kuwania nafasi hiyo. Hiyo ndiyo demokrasia,” alisema.
Bw Kioni na Bw Matiang’i wote ni manaibu wa kiongozi wa Jubilee, jambo linaloweka msingi wa ushindani wa moja kwa moja kati ya makundi yanayowaunga mkono.
Jubilee ni miongoni mwa vyama vilivyotawala siasa za Kenya wakati wa utawala wa Bw Kenyatta, ikiwa na wabunge na viongozi wengi wa kaunti.
Nguvu zake zimepungua tangu Bw Kenyatta alipoondoka madarakani, lakini chama bado ni sehemu muhimu ya siasa za upinzani na mipango ya miungano kuelekea 2027.
Pia kuna suala la fedha.
Jubilee imewahi kuwa miongoni mwa wanufaika wakubwa wa Hazina ya Vyama vya Kisiasa, ikipokea takriban Sh240.4 milioni katika mwaka wa 2017/18, Sh434.6 milioni mwaka uliofuata, Sh564.2 milioni mwaka wa 2019/20, Sh515 milioni mwaka wa 2020/21 na Sh1.02 bilioni mwaka wa 2021/22.
Kwa jumla, chama kilipokea zaidi ya Sh2.77 bilioni katika miaka hiyo mitano. Hata hivyo, mgao huo umepungua kutokana na kuporomoka kwa nguvu zake za kisiasa.
Katika mwaka wa kifedha wa 2026/27, Jubilee imetengewa Sh128.86 milioni kutoka kwa Hazina ya Vyama vya Kisiasa.
Mchanganuzi wa siasa Geoffrey Mboya alisema fedha ni sehemu tu ya mvuto wa chama hicho.
Alisema udhibiti wa Jubilee pia unamaanisha kushikilia miundo ya wanachama, mtandao wa kitaifa, chapa ya chama na mamlaka ya kujadiliana kuhusu nafasi yake katika miungano ya kisiasa.
Wakati huo huo, chama hicho kinakabiliwa na shinikizo la kurekebisha miundo yake kabla ya uchaguzi wa 2027.