Pigo kuu korti ikiagiza serikali irejeshe hisa za Safaricom ilizouzia kampuni ya Afrika Kusini
MAHAKAMA Kuu imebatilisha uuzaji wa asilimia 15 ya hisa za Serikali ya Kenya katika kampuni ya Safaricom kwa Vodacom Group, ikisema shughuli hiyo ilifanyika kinyume na Katiba na sheria za nchi.
Jopo la majaji watatu liliamuru hisa hizo zirudishwe serikalini, likibaini kuwa mchakato wa uuzaji ulikumbwa na dosari nyingi ikiwemo ukosefu wa ushiriki wa kutosha wa umma, kufichwa kwa taarifa muhimu, uwekaji wa bei usio na msingi wa wazi na kutoshughulikiwa kwa masuala ya usalama wa taifa yaliyotokana na kuhamishwa kwa udhibiti wa kampuni hiyo kwa wawekezaji wa kigeni.
“Kwa kuzingatia hitimisho letu, tunashikilia kuwa hakukuwa na ushiriki wa umma wa maana na wa kutosha kuhusu uuzaji huo. Hivyo basi, Kifungu cha 10 na 118 cha Katiba kilikiukwa,” walisema Majaji Francis Gikonyo, Roselyne Aburili na Tabitha Ouya.
Uamuzi huo ni pigo kubwa kwa mpango wa serikali wa kukusanya fedha za Hazina ya Kitaifa ya Miundombinu kupitia uuzaji wa mali ya umma.
Serikali iliuza hisa hizo kwa Sh204.3 bilioni kwa bei ya Sh34 kwa kila hisa.
Aidha, ilipata takriban Sh40.7 bilioni kutokana na kuuza haki zake za kupata mgao baadaye kutoka kwa asilimia 20 ya hisa ilizobaki.
Kesi hiyo iliwasilishwa mahakamani na mwanaharakati Tony Gachoka pamoja na wengine waliopinga uuzaji huo, wakisema Safaricom ni rasilimali muhimu ya kitaifa.
Mahakama ilikataa hoja ya Vodacom Group kwamba, kesi hiyo ilikuwa imepitwa na wakati baada ya Bunge kuidhinisha muamala huo Machi 31, 2026.
Majaji walisema kesi hizo zilipinga msingi wa kikatiba wa muamala wenyewe na kwamba, idhini ya baadaye ya Bunge isingeondoa ukiukaji uliodaiwa.
Mahakama ilisema kuwa ingawa Bunge lilifanya mikutano ya ushirikishaji katika kaunti 30, stakabadhi muhimu kama mkataba wa ununuzi wa hisa na makubaliano kuhusu haki za mgao wa baadaye hazikuwekwa wazi kwa umma.
“Tunakubaliana na walalamishi kwamba, taarifa na stakabadhi muhimu zilifichwa umma, Baraza la Mawaziri na Bunge la Taifa,” majaji walisema.
Mahakama ilisisitiza kuwa ushiriki wa umma si suala la kufanya mikutano pekee bali lazima uwe wa kweli, wa wazi, wa maana na unaowezesha wananchi kushawishi maamuzi yanayofanywa.
Majaji pia walibaini kuwa serikali iliwasilisha mpango huo kama uuzaji wa sehemu ya hisa, ilhali kwa hakika ulikuwa ni mchakato mpana zaidi wa marekebisho ya umiliki ambao ungeipa Vodacom udhibiti halisi wa Safaricom.
Chini ya mpango huo, hisa za Vodafone Kenya katika Safaricom zingepanda kutoka asilimia 39.9 hadi asilimia 55, huku Vodacom Group ikimiliki kikamilifu Vodafone Kenya.
Kwa mujibu wa mahakama, hatua hiyo ilifanana zaidi na unyakuzi wa kampuni kuliko uuzaji wa kawaida wa hisa za serikali.
Mahakama pia ilikosoa serikali kwa kutofungua uwekezaji huo kupitia mchakato wa wazi wa kuchagua mwekezaji wa kimkakati. Kuhusu bei ya Sh34 kwa kila hisa, majaji walikubaliana kuwa mchakato uliotumika haukuwa wa kimantiki na ulikuwa wa kiholela.
Zaidi, mahakama ilieleza kuwa muamala huo ulizua masuala mazito ya usalama wa taifa kwa kuwa Safaricom inaendesha miundombinu muhimu inayotumika katika uchaguzi, mifumo ya malipo ya serikali, huduma za fedha za simu na kuhifadhi data binafsi za mamilioni ya Wakenya.
Majaji walisema kuhamisha udhibiti wa miundombinu hiyo kwa kampuni ya kigeni bila tathmini ya awali ya usalama wa taifa kulikiuka wajibu wa serikali wa kulinda maslahi ya nchi.
Hivyo, mahakama ilitangaza uuzaji huo kuwa batili, ikafutilia mbali uamuzi wa Bunge uliouidhinisha pamoja na idhini yenyewe, mikataba na hatua zote zilizohusiana nao.
Mahakama iliamuru asilimia 15 ya hisa za Safaricom zirudishwe chini ya umiliki wa Serikali ya Kenya kwa niaba ya wananchi.
Pia ilikataa kusimamisha utekelezaji wa hukumu hiyo ili kuruhusu rufaa, na kuwaelekeza wahusika kuwasilisha ombi rasmi la kusitisha utekelezaji iwapo wanataka kufanya hivyo.