Afya na Jamii

Matatizo ya tumbo yasiyofaa kupuuzwa

Na WINNIE ONYANDO, ESTHER INTABO September 18th, 2026 Kusoma ni dakika: 4

BAADHI huchukulia kuumwa na tumbo mara kwa mara, kupata kiungulia, tumbo kujaa gesi au kushiba haraka kama jambo la kawaida tu.

Matatizo kama hayo yanapotokea, mtu atakimbia katika duka la kuuza dawa na kununua tembe mbili au tatu ili kutuliza mambo.
Lakini baada ya muda, maumivu yanarudi.

Kwa wengine, hali hii inaweza kuendelea kwa miezi bila mtu kufikiria kwamba huenda kuna tatizo kubwa zaidi.

Hii ni moja ya sababu zinazofanya saratani ya tumbo kugunduliwa ikiwa imefika hatua hatari, wataalamu wa afya wanaonya.

Dkt Joseph Abuodha, mtaalam wa saratani katika Hospitali ya Chuo Kikuu cha Aga Khan, anasema tatizo kubwa ni kuchelewa kwa utambuzi.

“Swali kubwa ni kwa nini idadi ya vifo iwe kubwa hivi? Ni kwa sababu tatizo hugunduliwa ikiwa imechelewa,” anasema.

Takwimu za Shirika la Kimataifa la Utafiti wa Saratani (IARC) zinaonyesha kuwa vifo vinavyokadiriwa kutokana na saratani ya tumbo duniani viliongezeka kutoka 642,000 mwaka 2024 hadi 654,000 mwaka 2025.

Wanaume ndio waathiriwa wakubwa wa aina hiyo ya saratani huku vifo miongoni mwao vikiongezeka kutoka 419,000 hadi 426,000 katika kipindi hicho.

Nchini Kenya, vifo vinavyohusishwa na saratani hii miongoni mwa wanaume viliongezeka kutoka 565 mwaka 2024 hadi 586 mwaka 2025, huku vile vya wanawake vikiongezeka kutoka 488 hadi 505.

Dalili zinazoweza kupuuzwa

Kinachofanya saratani ya tumbo kuwa ngumu kugundua mapema ni kwamba dalili zake za mwanzo zinaweza kufanana na matatizo ya kawaida ya tumbo.

Mtu anaweza kuhisi maumivu au usumbufu tumboni, tumbo kujaa gesi, kiungulia, gesi nyingi au dalili anazozihusisha na vidonda vya tumbo.

“Unaweza kuwa na maumivu ya tumbo, tumbo kujaa au dalili kama za vidonda vya tumbo. Pia kunaweza kuwa na asidi nyingi tumboni,” anasema Dkt Abuodha.

Hii ndiyo sababu mtu anaweza kutumia dawa za kupunguza asidi au kutibiwa bila kufikiria zaidi.

Tatizo ni pale dalili zinapoendelea kurudi licha ya matibabu.

Dkt Abuodha anasema wagonjwa wengi wanaofika hospitalini wakiwa tayari wamegunduliwa kuwa na saratani huwa waliwahi kufika hospitalini hapo awali.

“Mara nyingi tunakuta wagonjwa waliokuja kwetu na kupatikana wanaugua saratani ya tumbo waliwahi kufika hospitalini kwa wakati fulani kwa sababu ya tatizo hilo,” anasema.

Kwa hiyo, si kila maumivu ya tumbo yanamaanisha mtu ana saratani.

Hata hivyo, daktari huyo anasema kuwa maumivu yanayodumu, kubadilika au kurudi mara kwa mara hayafai kupuuzwa.

Dalili nyingine ambayo watu wengi wanaweza kuipuuza ni kushiba haraka.

Kwa mfano, mtu ambaye alikuwa akila sahani nzima ya ugali, nyama na mboga bila shida anaweza kuanza kushiba baada ya kula nusu ya chakula alichopakuliwa.

“Ukiwa ulikuwa unaweza kula sahani nzima ya ugali miezi sita iliyopita lakini sasa unashiba baada ya kula kidogo, huenda ni kwa sababu tumbo haliwezi kutekeleza wajibu wake kama kawaida,” anaeleza Dkt Abuodha.

Hali hii inaweza kuambatana na kupungua uzito bila mtu kukusudia.

Mtu anaweza kuendelea kula lakini mwili ukaendelea kupungua uzito.

Dalili nyingine inayopaswa kuangaliwa ni kinyesi kuwa cheusi, hali ambayo inaweza kuashiria kutokwa na damu tumboni.

Kutapika damu au kuona damu kwenye kinyesi pia kunahitaji mtu kutafuta matibabu haraka.

Kwa mtu anayesumbuliwa na kiungulia au vidonda vya tumbo, huenda matibabu ya kawaida yakasaidia.

Lakini ikiwa dalili zinaendelea licha ya matibabu yanayofaa, Dkt Abuodha anasema ni wakati wa uchunguzi zaidi.

“Baada ya vipindi kadhaa vya matibabu, ikiwa hujapona, unahitaji kufanyiwa vipimo vinavyojulikana kama endoscopy,” anasema.

Vipimo hivyo humwezesha daktari kuangalia ndani ya tumbo kwa kutumia kifaa maalumu.

Ikiwa kuna sehemu inayotia shaka, sampuli ya tishu inaweza kuchukuliwa na kufanyiwa uchunguzi kwenye maabara.

Uchunguzi huo wa tishu, unaojulikana kama histology, ndio njia muhimu zaidi ya kuthibitisha saratani ya tumbo.

Vipimo vingine kama CT scan au PET scan hutumika zaidi baada ya saratani kuthibitishwa ili kujua imeenea kwa kiwango gani na kusaidia kupanga matibabu.

Jambo jingine linalofanya saratani ya tumbo kuwa hatari ni kwamba katika hatua zake za mwanzo huenda mtu asiwe na dalili zozote zinazoonekana.

Mtu anaweza kuwa na tatizo la hapa na pale tumboni na baadaye kuwa sawa.

Katika baadhi ya visa, saratani hugunduliwa kwa bahati wakati mtu anafanyiwa kipimo kingine.

Kwa mfano, mtu anaweza kufanyiwa CT scan kutokana na maumivu ya tumbo na daktari akaona mabadiliko kwenye tumbo yanayohitaji uchunguzi zaidi.

Dkt Abuodha anaeleza kuwa eneo ambalo saratani imejitokeza pia huathiri dalili.

Tumbo lina sehemu ya juu ambako chakula huingia kutoka kwenye umio na sehemu ya chini ambako chakula hupita kuelekea kwenye utumbo.

Saratani ikijitokeza karibu na mojawapo ya sehemu hizi, hata uvimbe mdogo unaweza kuzuia chakula kupita vizuri.

Mtu anaweza kuhisi kama chakula kimekwama au hakipiti vizuri.

Lakini saratani inapokuwa katikati ya tumbo, dalili za mwanzo zinaweza kuwa za kawaida zaidi kama kujaa tumbo, kiungulia na maumivu yasiyo makali.

Maambukizi ya muda mrefu ya bakteria aina ya H. pylori ni miongoni mwa mambo yanayohusishwa na baadhi ya aina za saratani ya tumbo.

Watu walio na vidonda vya muda mrefu wanapaswa kufuatiliwa kulingana na hali zao.

Dkt Abuodha anasema mtu ambaye dalili zake zimebadilika au amepata tatizo jipya anapaswa kurudi hospitalini.

“Changamoto ni kutambua wakati dalili za kawaida zimechukua muda mrefu na zinahitaji uchunguzi zaidi,” anasema.

Umri pia ni sababu muhimu

“Kadri mtu anavyozidi kuzeeka, ndivyo uwezekano wa kupata ugonjwa huu unavyoongezeka,” anasema.

Uvutaji sigara na unywaji wa pombe kupita kiasi pia umehusishwa na hatari ya saratani ya tumbo.

Daktari pia anashauri watu kuwa waangalifu kuhusu tabia za ulaji, hasa vyakula vinavyosababisha usumbufu wa tumbo vinapoliwa mara kwa mara.

Hata hivyo, si kila mtu anayepata saratani ya tumbo huwa na historia ya familia ya ugonjwa huo.

Dkt Abuodha anasema chini ya asilimia tano ya visa vinaweza kuhusishwa moja kwa moja na sababu za kijenetiki.

Kwa nini wanaume wanaathirika zaidi?

Kwa ujumla, wanaume huathirika zaidi na saratani ya tumbo kuliko wanawake.

Dkt Abuodha anasema takriban wanaume wawili hupata saratani hii kwa kila mwanamke mmoja.

Anaeleza kuwa wanaume wanaweza kuwa na baadhi ya vihatarishi zaidi, huku pia wakichelewa kutafuta huduma za afya wanapopata dalili.

“Wanaume wanapopata maumivu, si rahisi kwao kutafuta huduma za afya,” anasema.

Hii inaweza kufanya ugonjwa ugunduliwe ukiwa umechelewa.

Ingawa mtu anapaswa kuwajibika kwa afya yake, kuchelewa kugundua saratani haimaanishi kila mara kuwa ni sababu ya mgonjwa kupuuza dalili.

Kuna pia changamoto katika mfumo wa afya

Baadhi ya wagonjwa wanaweza kuchelewa kupewa rufaa au kutumwa kwa mtaalamu anayefaa, huku gharama na upatikanaji wa vipimo kama endoscopy ukiwa kikwazo kwa wengine.

Dkt Abuodha anasema wagonjwa walio na dalili zinazotia shaka wanapaswa kuelekezwa upesi kwa mtaalam ili uchunguzi unaofaa ufanywe.

Anashauri kula chakula kilichopikwa vizuri, kupunguza vyakula vilivyosindikwa na kuzingatia ubora wa chakula badala ya wingi pekee.

Mazoezi ya mwili na kudhibiti uzito pia ni muhimu kwa afya kwa ujumla.

Anashauri pia kupunguza au kuacha kabisa uvutaji sigara na unywaji wa pombe kupita kiasi.

Kwa mtu anayepata usumbufu baada ya kula vyakula vyenye viungo vingi au vyakula vya moto sana, ni vyema kuwa mwangalifu na kutafuta ushauri wa daktari ikiwa hali hiyo inaendelea.

Muhimu zaidi, anasema mtu anayesumbuliwa na dalili za tumbo kwa muda mrefu hapaswi kujitibu.