Siasa

Ruto amponda tena Uhuru akimlaumu kuvunja makubaliano ya ‘Yangu kumi na Yako kumi’

Na DOMNIC OMBOK, GEORGE ODIWUOR September 18th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

RAIS William Ruto amemshambulia tena mtangulizi wake, Rais mstaafu Uhuru Kenyatta, akimlaumu kwa kusaliti makubaliano ya kisiasa waliyofikia walipokuwa washirika na sasa kufadhili siasa za upinzani dhidi ya serikali yake.

Dkt Ruto alisema yeye na Bw Kenyatta walikubaliana kuwa Rais huyo wa zamani angeongoza kwa miaka 10 kabla ya kumkabidhi yeye uongozi wa nchi kwa miaka mingine 10.

Hata hivyo, alidai Bw Kenyatta alipuuza makubaliano hayo ulipofika wakati wake wa kugombea urais na badala yake akamuunga mkono aliyekuwa kiongozi wa ODM Raila Odinga katika uchaguzi wa 2022.

“Hukutimiza. Badala yake, ulifanya kazi dhidi yangu,” Rais alisema alipokuwa akizungumza Sindo.

Dkt Ruto alisema alimuunga mkono Bw Kenyatta katika chaguzi nne na kusimama naye alipohitaji msaada wa kisiasa.

“Nilikuunga mkono katika chaguzi nne na nikakulinda. Ulipofika wakati wako wa kunisaidia, hukufanya hivyo hata kwa siku moja. Lakini baadaye Mungu alinisaidia kuwa Rais wa watu wa Kenya,” alisema.

Hata hivyo, Rais alisema hamlaumu Bw Kenyatta kwa kutomuunga mkono, akisema ilikuwa haki yake ya kidemokrasia kumuunga mkono mgombea aliyemtaka.

Lakini alimshutumu kwa kuhujumu serikali ya Kenya Kwanza na kufadhili siasa za upinzani.

“Unashusha hadhi ya afisi ya Rais mstaafu. Unashusha hadhi yako mwenyewe kama mtu,” alisema.

Kauli hizo zilitolewa muda mfupi baada ya Mahakama Kuu kuunga mkono sheria inayowazuia marais wastaafu kushikilia nyadhifa za uongozi katika vyama vya kisiasa zaidi ya miezi sita baada ya kuondoka madarakani.

Hata hivyo, mahakama haikuwazuia kuwa wanachama wa vyama au kushiriki shughuli za kisiasa.

Bw Kenyatta ametangaza ataacha uongozi wa Jubilee kufuatia uamuzi huo.

Dkt Ruto pia alikosoa rekodi ya kiuchumi ya serikali iliyotangulia, akidai serikali yake ilirithi uchumi uliokuwa katika hali mbaya.

“Tumelipa sehemu kubwa ya madeni na kupunguza mfumuko wa bei. Pia tumeongeza mara mbili akiba yetu ya fedha za kigeni,” alisema.

Alidai pia serikali yake imeajiri walimu 100,000, kujenga madarasa 23,000 na kufanya mabadiliko katika sekta ya afya.

Kauli za Rais zilijiri akimaliza ziara ya siku tano Nyanza, ambapo alitembelea Siaya, Kisumu, Homa Bay na Migori, akizindua miradi na kutangaza mipango mingine ya thamani ya mabilioni ya pesa.