Mwanamume amshtaki Sifuna akitaka kujua alivyotumia Sh55 alizomchangia
Bw Alan Masakhalia anataka mahakama iamuru Bw Sifuna na viongozi wa Linda Mwananchi kutoa taarifa kamili ya michango yote iliyotumwa kupitia nambari ya Paybill 3033049 pamoja na njia nyingine zozote zilizotumika kukusanya fedha.
Bw Masakhalia anasema kuwa wananchi waliochanga fedha kwa hiari yao baada ya kualikwa hadharani kufanya hivyo wana haki ya kufahamu jinsi fedha hizo zinavyohifadhiwa, kusimamiwa na kutumiwa.
Aidha, anataka mahakama kubaini ni hatua gani za kisheria zinazoweza kuchukuliwa iwapo mradi huo wa kisiasa utaachwa, kubadilishwa mwelekeo, kuhamishwa kwa mtu mwingine au kufanyiwa mabadiliko makubwa yanayokwenda kinyume na maelezo yaliyotolewa wakati fedha zilipoombwa.
Bw Masakhalia anasema kuwa kesi hiyo haisukumi ajenda ya kibinafsi ya kisiasa kwamba Bw Sifuna anapaswa kugombea urais.
Badala yake, anasema inalenga kupata ufafanuzi kuhusu wajibu wa kisheria unaohusishwa na fedha zinazochangwa na umma kwa madhumuni mahsusi ya kisiasa.
Kulingana naye, baada ya kukusanya kiasi kikubwa cha fedha kutoka kwa Wakenya, Bw Sifuna anaweza kuamua kutowania urais, kuunga mgombea mwingine na kumhamishia miundombinu iliyoanzishwa kupitia mradi huo, au kutumia fedha hizo kwa madhumuni tofauti na yale yaliyoelezwa kwa waliochangia.
“Hali kama hiyo itazua swali muhimu iwapo wananchi waliochangia fedha zao wana maslahi ya kikatiba na kisheria yanayoweza kutekelezwa kuhusu uhifadhi, uwajibikaji na matumizi halali ya fedha pamoja na mradi wa kisiasa waliofadhili,” alisema.
Anataka mahakama kubaini iwapo Bw Sifuna anaweza kukusanya fedha kutoka kwa wananchi kwa ajili ya azma ya urais, kisha baadaye kuachana na azma hiyo au kumuunga mkono mgombea mwingine baada ya fedha hizo kupatikana.
Bw Masakhalia alikumbusha kuwa mnamo Julai 21, 2026, Bw Sifuna alizindua hadharani Paybill nambari 3033049 na kuwaalika Wakenya kutoa michango ya kifedha kusaidia vuguvugu la Linda Mwananchi.
Anadai kuwa waandalizi walitangaza hadharani kwamba, watu 9,419 walichanga takriban Sh519,144 katika siku ya kwanza ya shughuli hiyo ya kuchangisha fedha.
“Ndani ya takriban saa 36, jumla ya pesa zilizoripotiwa hadharani iliongezeka hadi karibu Sh2,210,836.82,” alisema.
Mlalamishi huyo anasema kuwa sehemu kubwa ya michango ilikuwa ni michango midogo, mingine ikiwa ya chini hadi Sh10, jambo linaloonyesha kuwa mpango huo uliwasilishwa kama mradi wa kisiasa unaofadhiliwa na wananchi badala ya shughuli binafsi ya kifedha.
Anasema kuwa alitoa mchango wake kwa hiari na kwa kutegemea maelezo yaliyotolewa hadharani kuhusu malengo ya mradi huo na sababu zilizowafanya wananchi waombwe kuchangia.
“Sikutoa mchango huo kama zawadi binafsi kwa mshtakiwa wa Kwanza kwa matumizi yake mwenyewe. Wala sikuwa nikichangia harambee ya matibabu au elimu. Mchango wangu ulikuwa wazi kwa ajili ya hazina ya kampeni ya urais ya Mheshimiwa Sifuna,” alisema.
Bw Masakhalia aliongeza kuwa ombi hilo la kuchangisha fedha lilivutia michango kutoka kwa Wakenya wengi wengine.
Baadhi ya michango hiyo, alisema, ilikusanywa kupitia ndoo zilizowekwa katika masoko ya Naitiri, Butula, Kakamega na Kabuchai zikiwa na mabango ya Bw Sifuna ambayo waliochangia waliamini yalihusishwa na kampeni ya urais.
“Ninaamini kuwa uhuru wa kikatiba wa kiongozi wa kisiasa kufanya maamuzi ya kisiasa hauondoi, kwa wenyewe, wajibu wa kisheria kuhusu fedha zilizoombwa na kupokelewa kutoka kwa wananchi kwa madhumuni ya kisiasa yaliyowasilishwa hadharani,” alisema.
Mlalamishi huyo anataka mahakama ibaini iwapo wananchi waliochangia kifedha katika mradi huo wa kisiasa uliotangazwa hadharani walipata haki za kikatiba na kisheria zinazoweza kutekelezwa kuhusu matumizi, uwajibikaji na ufichuzi wa michango yao.
Miongoni mwa maagizo anayotaka ni amri itakayomlazimisha Bw Sifuna na vuguvugu la Linda Mwananchi kutoa hesabu kamili na zilizothibitishwa za fedha zote zilizopokelewa kupitia Paybill nambari 3033049 pamoja na njia nyingine zozote.
Pia anataka mahakama kuwaamuru washtakiwa kufichua matumizi yote ya fedha hizo, ikiwemo stakabadhi za malipo, kumbukumbu za malipo na stakabadhi nyingine zozote zinazothibitisha matumizi hayo.