Habari

Maafisa 20 wa IEBC wahamishwa uchaguzi ukikaribia

Na JUSTUS OCHIENG September 19th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

TUME Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) imeanza kupanga upya uongozi wake katika kaunti kwa kuwahamisha zaidi ya maafisa 20 wakuu wa uchaguzi katika maeneo mbalimbali nchini, huku maandalizi ya Uchaguzi Mkuu wa 2027 yakishika kasi.

Uhamisho huo uliotangazwa katika barua iliyotiwa saini na Kaimu Afisa Mkuu Mtendaji wa IEBC Ruth Kulundu.

IEBC imesema mabadiliko hayo ni sehemu ya zoezi la kawaida la kiutawala la kujaza nafasi zilizo wazi, kuwaweka maafisa waliopandishwa vyeo katika vituo vipya na kuimarisha utendaji wa tume mashinani.

Mabadiliko hayo yanajiri siku chache baada ya IEBC kutangaza Jumanne, Agosti 10, 2027 kuwa siku ya kupiga kura.

Mwenyekiti wa IEBC Erastus Ethekon amepuuza madai kwamba uhamisho huo umechochewa na siasa au una uhusiano na uadilifu wa maafisa wanaohusika.

Alisema ni utaratibu wa kawaida baada ya tume kuajiri maafisa wapya kuchukua nafasi za waliostaafu, waliofariki au walioondoka kazini.

“Tumeajiri maafisa wapya wa uchaguzi wa kaunti. Hiyo inamaanisha lazima wapangwe upya na kupelekwa katika vituo vipya,” Bw Ethekon alisema katika mahojiano na Taifa Leo.

Alisema takriban maafisa 17 wameajiriwa na kupandishwa vyeo, hivyo kuhitajika kupelekwa katika kaunti mbalimbali.

“Kuna waliostaafu, wengine walifariki na wengine wakaondoka. Kwa hivyo wako takriban 17 ambao tumeajiri,” alisema.

Baadhi ya maafisa waliohamishwa ni Beatrice Muli kutoka Kiambu hadi Taita-Taveta; Hudson Salenoi kutoka Vihiga hadi Turkana; Rebecca Abwaku kutoka Homa Bay hadi Trans Nzoia; Reuben Mbuu kutoka Makueni hadi Kitui na Amosi Chilai kutoka Nairobi hadi Kakamega.

Wengine ni Japheth Lagat kutoka Trans Nzoia hadi Pokot Magharibi; Grace Anyang kutoka Migori hadi Kericho; Husna Hassa kutoka Mombasa hadi Kilifi; Zahara Hassan kutoka Mandera hadi Wajir na Sheikh Abdi kutoka Wajir hadi Garissa.
Engor Emmanuel amehamishwa kutoka Turkana hadi Narok, Frank Boinet kutoka Elgeyo-Marakwet hadi Baringo, Sidney Namulungu kutoka Kericho hadi Marsabit, John Mwangi kutoka Baringo hadi Kirinyaga na Saumu Chirchir kutoka Murang’a hadi Bomet.

Maafisa wa uchaguzi wa kaunti wana jukumu muhimu katika maandalizi ya uchaguzi, ikiwa ni pamoja na usajili wa wapigakura, mafunzo, usafirishaji wa vifaa na uendeshaji wa shughuli za kupiga kura.

Bw Ethekon alisema zoezi hilo litaendelea huku nafasi zilizo wazi katika ngazi ya maeneo bunge zikijazwa.

“Tunaendelea kuwapeleka katika vituo vyao. Hatua inayofuata ni kujaza nafasi zilizo wazi katika ngazi ya maeneo bunge,” alisema.

IEBC pia imeweka ratiba ya shughuli kuelekea uchaguzi wa 2027. Vyama vya kisiasa vinatarajiwa kuwasilisha majina na saini za maafisa wao walioidhinishwa kufikia Oktoba 15, 2026.

Sheria za uteuzi wa vyama zinatarajiwa kuthibitishwa na Msajili wa Vyama vya Kisiasa kufikia Oktoba 30 na kuwasilishwa kwa IEBC kufikia Novemba 6.

Maafisa wa umma wanaonuia kugombea uchaguzi huo watahitajika kujiuzulu nyadhifa zao kufikia Februari 10, 2027.

Kampeni rasmi zinatarajiwa kuanza Mei 29, 2027 na kumalizika Agosti 7, siku mbili kabla ya uchaguzi.

Bw Ethekon alisema mabadiliko hayo yanalenga kuhakikisha kila kaunti ina afisa anayefaa kabla ya shughuli za uchaguzi kuingia katika hatua muhimu zaidi.

Alisisitiza kuwa maafisa hawana haki ya kudumu katika kituo fulani.

“Ukiambiwa uende kituo kipya, unaenda na kufanya kazi. Hauwezi kusema lazima ufanye kazi mahali pamoja,” alisema.

Bi Kulundu aliteuliwa kuwa Kaimu Afisa Mkuu Mtendaji wa IEBC Agosti 5, baada ya kumalizika kwa muda wa miezi sita wa Moses Ledama Sunkuli katika afisi hiyo.