• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 7:50 AM
KURUNZI YA PWANI: Wabunge 4 wasema 2022 Pwani itatoa mgombea urais

KURUNZI YA PWANI: Wabunge 4 wasema 2022 Pwani itatoa mgombea urais

Na CHARLES LWANGA na KALUME KAZUNGU

WABUNGE wanne kutoka eneo la Pwani wamesema watahakikisha eneo hilo limesimamisha mgombeaji wa urais atakayekabiliana na vinara wengine katika uchaguzi mkuu wa 2022.

Wakiongozwa na mbunge wa Ganze, Bw Teddy Mwambire, ambaye pia ni naibu mwenyekiti wa chama cha ODM kaunti ya Kilifi, walisema eneo hilo litaungana na kukubaliana mbombeaji atakayemenyana na wagombeaji wengine wa urais nchini.

Wabunge hao walisema hayo walipohudhuria mazishi ya jamaa ya mbunge wa Kilifi Kaskazini, Bw Owen Baya, eneo la Matsangoni.

Walisema wakati umefika ambapo eneo hilo ambalo lina watu zaidi ya milioni mbili kulingana na sensa ya 2009 kusimamisha mgombeaji wao wa urais.

“Tuko tayari kuunganisha eneo hili kabla ya kukabiliana na wagombeaji wengine kupata urais,” alisema na kuongeza, “hapo ndio tutaungana na maeneo mengine ili kuunda serikali baada ya uchaguzi.”

Baadhi ya wabunge kutoka pwani waliohudhuria mazishi hayo ni mbunge wa Kilifi Kusini, Ken Chonga na mwenzake wa Changamwe, Bw Omar Mwinyi.

Bw Chonga alisema wakati huu maeneo mengine ya Kenya yatashawishiwa ma Wapwani katika siasa za 2022 ili kuunda serikali.

Mbunge huyo pia alisema wanafanya kila wawezalo kuhakikisha eneo hilo halitagawanyika wakati wa uchaguzi mkuu sawa na inavyoshuhudiwa kila wakati kunapokuwa na uchaguzi.

“Tumekuwa tukigawanywa kwa miaka mingi na saa hizi tumeanza kampeni wa kuunganisha Wapwani kuwa kitu kimoja bila kuzingatia dini au kabila ili tuongee kwa saunti moja katika uchaguzi ujao,” alisema.

Kugawanyika

Mbunge wa Changamwe alisema wakazi wamekuwa wakigawanyika kwa msingi wa dini na kufanya eneo hilo kutengwa kimaendeleo na kusalia kuwa maskini kwa miaka mingi.

“Wanatumia utengano wetu kama unyonge ya kutufanya kusalia watumwa wa kupigia debe wagombeaji wao,” alisema.

Aliongeza: “ Tunafaa tuungane kufanya mambo makuu.”

Haya yanajiri wakati ambapo Gavana wa Mombasa Hassan Joho na mwenzake wa Kilifi, Bw Amason Kingi wametangaza kuwa watagombea kiti cha urais katika siasa za 2022.

Kwa upande wake, mbunge wa Soi Caleb Kositany ambaye pia alihudhuria mazishi hayo, alimtaka Rais Uhuru Kenyatta, naibu wake William Ruto pamoja na kinara wa ODM, Raila Odinga waunganishe wananchi hata wakati wanapokabiliana na vita didhi ya ufisadi.

Kwingineko, Gavana wa Lamu, Fahim Twaha ametimiza ahadi yake ya kubandika jina la mpinzani wake wa kisiasa, Issa Timamy kwenye moja ya wodi za wanaume katika hospitali kuu ya King Fahad mjini Lamu. Bw Twaha amechukua hatua hiyo licha ya mpinzani wake kupinga wazo hilo awali.

Katika kile kilichotajwa kuwa kejeli dhidi ya mpinzani wake, ambaye pia alikuwa gavana wa eneo hilo, Bw Twaha alihakikisha ahadi hiyo imetimizwa.

Alikuwa ametangaza mpango huo wakati wa kusherehekea ushindi wake baada ya kesi ya kuupinga iliyowasilishwa na Bw Timamy, kutupiliwa mbali.

Bw Twaha alisema wazo hilo ni dhirisho kwamba hana kinyongo na mtangulizi wake.

“Nataka kuwafahamisha wale ambao tulikuwa tukishindana nao kwamba mimi sina kinyongo nao kwani hayakuwa mashindano ya kivita,” alisema.

You can share this post!

KIPWANI: ‘Mungu aliniepusha na penzi...

Tunaangazia mechi nane za Super 8 Jumapili

adminleo