• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 10:08 PM
Cherargei amtaka Gavana Sang ajiuzulu kwa ‘kupoteza’ Sh2.3b

Cherargei amtaka Gavana Sang ajiuzulu kwa ‘kupoteza’ Sh2.3b

Na CHARLES WASONGA

SENETA wa Nandi Samson Cherargei sasa anamtaka Gavana wa kaunti hiyo Stephen Sang’ kujiuzulu la sivyo atimuliwe afisini na wananchi kwa kile anachodai ni kupotea kwa takriban Sh2.3 bilioni pesa za umma.

Kwenye kikao na wanahabari katika majengo ya bunge Jumatano, Seneta Cherargei pia alimtaka Mkurugenzi wa Idara ya Upelelezi wa Jinai George Kinoti kumchunguza Bw Sang kwa lengo la kupendekeza kushtakiwa kwake kwa kutoweka kwa pesa hizo.

“Ripoti ya Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali Edward Ouko imeibua maswali kuhusu kupotea kwa jumla ya Sh2.3 bilioni tangu Gavana Sang’ alipoingia mamlakani mnamo 2017. Pesa hizi zimepotea katika idara sita za utawala wa Sang,” akasema Bw Cherargei.

Seneta huyo alidai kuwa hatua ya Bw Sang’ ya kuwasimamisha kazi maafisa 16 wa serikali yake, wakiwemo mawaziri watatu ni hatua ya kujiondolea lawama ilhali yeye ndiye chanzo cha uovu huo katika serikali yake.

“Gavana Sang’ asitudanganye kwa kuwasimamisha maafisa 16 kutoka na kutoweka kwa vifaa vya thamani ya Sh234 milioni vilivyonunuliwa na Idara ya Elimu ya Chekechea kwa ajili ya ujenzi wa shule za chekechea katika kaunti ya Nandi. Takriban Sh2.3 bilioni zimepotea chini ya usimamizi wa Sang’ tangu alipoangia afisini na anafaa kuwajibikia uovu huo.

“Kwa hivyo, kama mtetezi wa ugatuzi katika kaunti ya Nandi nataka DCI, DPP na EACC kumchunguza Bw Sang’ kwa lengo la kumshtaki kwa kosa hilo. Kabla ya hapo nataka ajiuzulu mara moja la sivyo sisi kama wakazi wa Nandi tutamwandama na kumkamata,” seneta huyo aliyeonekana mwenye hamaki akasema.

Na bila kutoa ithibati, Seneta Cherargei alidai kuwa mwaka 2018 Gavana Sang’ alitumia Sh2.4 milioni kukodi helikopta aliyotumia kwenda kujivinjari katika Mbuga ya Kitaifa ya Maasai Mara.

“Hizi Sh2.4 milioni ambazo Gavana Sang’ alitumia kwa starehe zake zinaweza kufadhili ujenzi wa zaidi ya madarasa matano kwa gharama ya Sh500,000 kwa kila darasa. Hatuwezi kuvumilia ubadhirifu wa pesa kiwango hiki,” akasema Bw Cherargei, akiongeza kuwa matumizi ya pesa hizo yaligunduliwa na katika ripoti ya Bw Ouko ya miaka ya kifedha ya 2017/2018 na 2018/2019.

You can share this post!

HUDUMA NAMBA: Sababu ya Wakenya kujikokota kujisajili

IEBC yajitetea kuhusu matumizi ya Sh690m kwa mapochopocho

adminleo