• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 5:50 AM
Konsitebo wakongwe katika kikosi cha polisi roho mkononi

Konsitebo wakongwe katika kikosi cha polisi roho mkononi

Na MWANGI MUIRURI

INSPEKTA Mkuu wa Polisi Hillary Nzioki Mutyambai amezindua rasmi msasa wa kuwapandisha ngazi maafisa ambao wamedumu kwa muda mrefu katika ngazi ya chini zaidi ya konsitebo.

Kigezo kikuu katika msasa huo ni kuwa afisa huyo awe ametinga umri wa miaka 50 na hajawahi kupandishwa cheo na hana kesi yoyote ya kinidhamu inayoendelea.

Katika msingi huo, Bw Mutyambai amewaagiza wakuu wote wa vitengo wawasilishe orodha ya maafisa hao afisini mwake, makataa ya kupokezwa orodha hiyo yakiwa ni Mei 9, 2019.

“Barua hii ni ya kuwaagiza makamanda wa stesheni wawasilishe majina ya maafisa walio katika hali iliyoelezewa, wawe wako na zaidi ya miaka 50, wamedumu katika kiwango hicho cha konsitebo ambacho ni kundi la F katika huduma ya umma na wawe hawana kesi za kinidhamu,” barua ya Mutyambai yasema.

Wale ambao watapandishwa cheo hadi kwa mfano kuwa koplo au hata sajini watanufaika na kupanda kwa ujumla wa kitita cha kustaafu wakitinga miaka 60.

Walio na ulemavu hata hivyo hustaafu wakiwa na umri wa miaka 65.

Mmoja wa walio na hamu ya juu kushirikishwa katika kupandishwa cheo ni Konsitebo Joseph Gichuru ambaye aliingia rasmi katika kikosi cha polisi Oktoba 4, 1980, na ambapo tarehe yake rasmi ya kustaafu ni Juni 30, 2020.

“Sijawahi kuwa na kesi yoyote ya kinidhamu. Nimepigwa msasa wa ufaafu mara si haba na hata hadharani nimeomba wakubwa wangu wanipandishe cheo…Wale tulianza nao kazi leo hii wako na mamlaka ya juu na wengine hata ni wakubwa wangu Jijini Nairobi. Mimi huwa najiuliza kwanini nikawa na mkosi huu wote kazini na nimekuwa mwaadilifu kwa kazi yangu,” anasema Gichuru.

Konsitebo Joseph Kimaru Gichuru (kushoto) akiwa na kurutu mwenzake, James Mwangi ambaye leo hii ni Inspekta wa polisi, katika hii picha ya zamani wakiwa katika taasisi ya elimu ya polisi mwaka wa 1980. Picha/ Mwangi Muiruri

Anasema kuwa maisha yamekuwa magumu zaidi kazini kiasi kwamba hata kusomesha watoto wake amepata shida si haba.

“Ina maana kuwa kwa miaka hii yote 39 ambayo nimekuwa kazini sijawahi kupata nafasi ya kuitwa mkubwa na yeyote. Waliojiunga na kikosi hivi majuzi wakiwa sawa na rika la watoto wangu leo hii wengine ni wa kiwango cha Inspekta na ambapo ninafaa kuwanyenyekea na kuwaheshimu kama wakubwa wangu ilhali kwa tajiriba, nilianza kazi wakiwa bado kuzaliwa. Hii dunia mara nyingine haina haki,” anasema.

Sasa, imani yote ya Konsitebo Gichuru ambaye ni mzawa wa Kaunti ya Nyeri katika Kaunti ndogo ya Mathira ni Julai 17, 2019 ambapo afisi ya Mutyambai itatoa orodha rasmi ya wale ambao watapandishwa madaraka.

Bw Mutyambai pamoja na Mwenyekiti wa Tume ya Huduma kwa Polisi (NPSC) Eliud Kinuthia wanakiri kuwa shida hii yote imetokana na ukosefu wa sera maalumu kuhusu kupandisha vyeo maafisa.

Kuna maafisa ambao waliomba wasitajwe ambao wamekiri kuwa kupata madaraka ndani ya kikosi cha polisi ni sawa na kushuka mchongoma.

“Ikiwa wengi wetu wataandika vitabu vya kuelezea mahangaiko yetu tukisaka mamlaka…Wasomaji watashangaa kiasi cha kuzirai…Watasoma vile huwa tunatumia wakubwa wa jamii zetu, kuhongana kwa pesa na hata mahaba… Wengine wakishtaki kesi mahakamani za kushinikiza wapandishwe vyeo. Hii ni kazi ya mawazo na usishangae ni kwa nini visa vya mauti vimejaa ndani ya kikosi ambapo wengine huua wenzao na wengine wakijiua,” anasema mmoja wa makamanda wa Stesheni za polisi hapa nchini.

You can share this post!

UJASIRIAMALI: Mseto wa mboga hasa za kiasili unampa msingi...

‘Upekee ni sifa muhimu ya utafiti’

adminleo