• Nairobi
  • Last Updated April 23rd, 2024 9:40 PM
Malkia Strikers wailima Ethiopia kunusia All African Games

Malkia Strikers wailima Ethiopia kunusia All African Games

Na GEOFFREY ANENE

MALKIA Strikers iko pua na mdomo kuingia mashindano ya All-African Games baada ya kubwaga Ethiopia kwa seti 3-0 kwenye mchujo wa Ukanda wa Tano wa voliboli ya wanawake jijini Kampala nchini Uganda, Jumatatu.

Mabingwa wa All-African Games mwaka 1991, 1995, 1999 na 2015 Kenya walienda katika mapumziko ya kwanza mawili ya lazima wakiongoza seti ya kwanza kwa alama 8-3 na 16-8 kabla ya kuinyakua 25-13.

Kenya ilikuwa katili zaidi katika seti ya pili ambayo iliongoza 11-2, 16-5 na 20-6 kabla ya kuishinda 25-8.

Malkia, ambayo inanolewa na makocha Shailene Shamdoo (Italia), Japheth Munala na Josp Barasa, ilikamilisha kazi kwa kubeba seti ya tatu kwa alama 25-10 baada ya kuongoza 9-3 na 17-8.

Wakenya wako juu ya jedwali la mchujo huu wa mataifa manne kwa alama sita. Waliingia mechi ya Ethiopia na motisha ya kucharaza Rwanda 3-0 (25-10, 25-17, 25-10) mnamo Mei 19.

Ethiopia imebanduliwa nje ya kampeni ya kufika All-African Games nchini Morocco mwezi Agosti mwaka 2019.

Waethiopia waliteremka katika ukumbi wa Lugogo kumenyana na Kenya wakiwa wanauguza kichapo cha seti 3-0 dhidi ya Uganda. Kenya na Uganda zitakabiliana Mei 21. Uganda itamenyana na Rwanda katika mechi yake ya pili baadaye Mei 20.

Kikosi cha Kenya: Mercy Moim, Sharon Chepchumba, Noel Murambi, Leonida Kasaya, Violet Makuto, Immaculate Chemutai, Jane Wacu, Janet Wanja, Edith Wisa, Triza Atuka, Lorine Chebet na Agripina Kundu.

You can share this post!

Wakazi wa Zimmerman waahidiwa hatimiliki

Mfumo wa kidijitali bungeni kurahisisha huduma

adminleo