• Nairobi
  • Last Updated March 19th, 2024 6:55 AM
KAULI YA MATUNDURA: Urasmishaji wa Kiswahili nchini Rwanda badala ya Kifaransa hauna upya wowote

KAULI YA MATUNDURA: Urasmishaji wa Kiswahili nchini Rwanda badala ya Kifaransa hauna upya wowote

Na BITUGI MATUNDURA

JUMA lililopita, wabunge wa Rwanda waliidhinisha Kiswahili kuwa lugha rasmi na ‘kuitupilia mbali’ lugha ya Kifaransa na kukiweka pembezoni Kiingereza.

Hatua hiyo ilipokelewa kwa hisia mbalimbali; baadhi ya watu wakiisherehekea na wengine wakionyesha masikitiko.

Baadhi ya watu walisema kwamba hatua hiyo ni nzuri; ingawa kuna wasiwasi kuwa huenda ikaighadhabisha Ufaransa.

Athari za hatua hiyo kwa mujibu wa wataalamu zitaanza kuonekana ikitarajiwa kwamba Ufaransa huenda ikaiadhibu Rwanda kwa kufadhili vyama vya upinzani kupinga utawala wa Rais Paul Kagame.

Baadhi ya wataalamu walihisi kwamba hatua hiyo ni ishara na mfano maridhawa unaopaswa kuigwa na nchi za Afrika ambazo bado zinakumbatia lugha za watawala wao wa zamani na hivyo basi kuendelea kudumisha ukoloni mamboleo.

Nilimuuliza Afisa Mkuu Mtendaji wa Kamisheni ya Kiswahili ya Afrika Mashariki (KAKAMA) – Prof Inyani Simala – atoe kauli kuhusu hatua hiyo ya Rwanda kukikumbatia Kiswahili badala ya Kifaransa.

Hatua hiyo inaashiria nini?

Athari yake katika Sera ya Lugha Afrika ya Mashariki na Kati ni ipi?

Prof Simala alisema kwamba hatua hiyo haikuwa ngeni kwa sababu maamuzi hayo yalifanywa mnamo mwishoni mwa 2017 na mwanzoni mwa 2018.

Prof Simala alitahadharisha kwamba kabla ya kuisherehekea hatua hiyo ambayo haina upya wowote, ni muhimu kuelewa muktadha mzima kwanza uliochangia katika nchi hiyo kufikia maamuzi hayo.

Alisema kwamba maamuzi hayo yalichukuliwa na nchi zote za Afrika ya Mashariki.

Alifafanua kwamba Kamisheni ya Kiswahili ya Afrika Mashariki imekwisha kuweka na kuimarisha mikakati ya kukiendeleza Kiswahili.

Alisema, kwa sasa, Kiswahili si lugha rasmi ya Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Kwa sababu hiyo Kamisheni ilishirikiana na Bunge la Jumuiya ya Afrika Mashariki (EALA) na kupitisha kwamba Kiswahili kiwe lugha rasmi.

Mwongozo wa kisera

Baada ya tamko hilo, KAKAMA ilishauri Baraza la Mawaziri wa Afrika Mashariki kutoa mwongozo wa kisera wa utekelezwaji wa azimio hilo. Baraza hilo chambacho Mwalimu Simala lilitoa maelekezo matano kwa nchi zote wanachama.

Kwanza, kila nchi ikitangaze Kiswahili kuwa lugha rasmi.

Pili, kila nchi ianzishe Baraza la Kiswahili.

Tatu, kila nchi iwe na Chama cha Kitaifa cha Kiswahili. Nne, Kiswahili kitumiwe katika Nyanja rasmi ikiwa ni pamoja na mifumo ya elimu na vyambo vya habari.

Mwisho, shughuli za Kiswahili zifadhiliwe pale inapowezekana.

Kwa hiyo, Prof Simala alifafanua kwamba nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki zimo katika hatua mbalimbali za utekelezwaji wa mambo haya.

“Rwanda ikitangaza Kiswahili kuwa lugha rasmi, inachofanya ni kutekeleza maazimio hayo kupitia elimu.”

Alifafanua pia kuwa, sera ya lugha nchini Rwanda inatoa nafasi kwa lugha nne rasmi: Ikinywarwanda; Kiingereza; Kiswahili na Kifaransa.

Kutokana na maelezo na ufafanuzi wa Prof Simala, sikosei kudai kwamba nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki zinajikokota katika kusukuma mbele ajenda ya Kiswahili.

Nchini Kenya kwa mfano, hatua za kubuniwa kwa Baraza la Kitaifa la Kiswahili la Kenya (BAKIKE) zimekwama.

Mchakato wa kuandaa Rasimu ya Sera ya Lugha ya Kenya (Kenya Language Policy Draft Bill) ulikwama miaka mingi imepita sasa.

Prof Kimani Njogu, mtaalamu wa lugha na utamaduni pendwa anasema kwamba mchakato huo umekuwa ukizunguka kwenye mduara.

Anapendekeza kwamba Chama cha Kiswahili cha Taifa (CHAKITA) kijifungate masombo kuhakikisha kwamba mchakato huo unaanzishwa tena.

Kiswahili ni lugha muhimu sana katika ukanda wa Afrika Mashariki kwa kuwa ndiyo lugha ya mawasiliano mapana.

Baruapepe: [email protected]

You can share this post!

KAULI YA WALIBORA: Huenda sera duni ya elimu Tanzania inaua...

MAPITIO YA TUNGO: Sikitiko la Sambaya; Riwaya inayoakisi...

adminleo