• Nairobi
  • Last Updated April 20th, 2024 3:03 PM
JAMVI: ‘Kieleweke’ kutaka kutambuliwa Bungeni ni dalili ya Jubilee kufifia

JAMVI: ‘Kieleweke’ kutaka kutambuliwa Bungeni ni dalili ya Jubilee kufifia

Na CHARLES WASONGA

HATUA ya wabunge wanaopinga azma ya Naibu Rais William Ruto kuingia Ikulu mwaka wa 2022 kumwandikia Spika wa Bunge Justin Muturi wakitaka kundi lao almarufu “Kieleweke” litambuliwe bungeni imeibua hisia mseto katika ulingo wa siasa.

Wadadisi wa kisiasa wanafasiri hatua hiyo kuashiria uhalisia wa mpasuko ulioko ndani ya chama tawala cha Jubilee na kujitolea kwa mirengo ya Kieleweke na Tanga Tanga kuendelea kuendeleza tofauti zao kuelekea uchaguzi mkuu ujao.

Wabunge wa “Team Tanga Tanga” sasa wanamtaka Bw Muturi kukataa ombi hilo wakisema wabunge hao wanaongozwa na “nia mbaya ya kutumia bunge kama jukwaa la kuendelesha vita vyao dhidi ya Naibu Rais”.

“Tunamtaka Spika wetu kukataa ombi kama hilo. Hawa watu wamegundua kwamba wananchi hawataki propaganda ambao wao hueneza kila mara makanisani na kwenye hafla ya mazishi. Hii ndio maana sasa wanataka kutumia bunge kama jukwaa la kuendeleza porojo zao dhidi ya Naibu Rais. Tunamhimiza Spika kuwapuuzilia mbali,” akasema Mbunge wa Mathira Rigathi Gachagua ambaye ni mwanachana wa vuguvugu la Team Tanga Tanga.

Na kulingana na mchanganuzi wa masuala ya kisiasa Martin Andati, ombi hilo la vuguvugu la Kieleweke kwa Bw Muturi ni ithibati tosha kuwa chama cha Jubilee kimesambaratisha kabisa kundi lake la wabunge.

“Hii ina maana kuwa licha ya ingawa Naibu Rais amekuwa akishikilia kuwa Jubilee bado iko pamoja, chama hiki kimesambaratika kuwili. Na ikiwa ni kweli wale wanaojiita Kieleweke wametuma ombi la kutaka watambuliwe bungeni, bado lile kundi la wabunge wa Jubilee (PG) haliko kabisa kwani sasa ni wazi kwamba hawako tayari kushiriki meza moja na wenzao ambao ni wandani wa Ruto,” anasema.

Wabunge wa mrengo wa Kieleweke wanataka waruhusiwe kuendesha shughuli zao bungeni kwa kutambuliwa kwa jina jipya la, “Wabunge Watetezi wa Umoja.” Kundi hilo linajumuisha wabunge wa chama tawala Jubilee na vyama vya upinzani kama vile, ODM, Wiper na ANC.

Chini ya uongozi wa Mbunge wa Nyeri Mjini Ngunjiri Wambugu na Mbunge Maalum Maina Kamanda, wabunge hao hawaelewani na kundi la “Team Tanga Tanga” ambalo limekuwa likimpigia debe Dkt Ruto na kumtaja kama mgombeaji urais anayefaa kuingia Ikulu baada ya Rais Uhuru Kenyatta kukamilisha muhula wake wa pili na wa mwisho mnamo 2022.

“Ni kweli tumemwandikia barua Spika Justin Muturi barua tukitaka kutambuliwa kama kundi rasmi la wabunge. Lengo letu ni kuendeleza ajenda ya rais ya kutumia bunge kama jukwaa la kuhimiza umoja na utangamano wa kitaifa,” Bw Wambugu akasema.

“Hatua hii ni kinyume na ile ambayo imechukuliwa na wenzetu ambao wameanza kampeni za urais mapema ilhali huu ni wakati wa kuhimiza umoja na kuendeleza ajenda nne kuu za maendeleo zilizotangazwa na serikali,” anaongeza

Wanachama wa vuguvugu la Kieleweke wamekuwa wakimshutumu Dkt Ruto na wandani wake katika Tanga Tanga wakidai wanahujumu vita dhidi ya ufisadi na muafaka wa maridhiano kati ya Rais Kenyatta na kiongozi wa ODM almaarufu Handisheki.

Isitoshe, wabunge hao wamemtaka Naibu Rais ajiuzulu kwa kuendelea kukaidi misimamo ya Rais Kenyatta.

“Unawezaje kudai kuwa wewe ni mdogo wa Rais ilhali unakwenda kinyume cha ushauri wake kwa kuanzisha kampeni za mapema ya kutaka kiti anachokalia sasa. Badala ya kuungana naye kuendelea ajenda za serikali kama vile vita dhidi ya ufisadi anadai vita hivyo vinalenga watu wake pekee,” anasema Bw Kamanda.

“Hii ndio maana sisi kama wabunge ambao tunapinga kampeni za mapema za urais, vita dhidi ya ufisadi na muafaka wa maridhiano ulioanzishwa na Rais pamoja na Bw Odinga, tunataka tutambuliwe bunge ili tuweze kuendeleza ajenda hiyo,” akaongeza.

Kulingana na Bw Kamanda, kundi la Kieleweke lina zaidi ya wabunge 70 kutoka vyama mbalimbali vya kisiasa. Hata hivyo, kando na Kamanda na Wambugu, wabunge wengine ambao huandamana na wao katika ibada za Jumapili na mikutano mingine ya kisiasa ni; Joshua Kutuny (Cherangany), Anthony Oluoch (Mathare), Paul Koinange (Githunguri, Jubilee), Robert Mbui (Kathiani, Wiper), Gathoni Wa Muchomba (Kiambu, Jubilee), Muturi Kigano (Kangema, Jubilee), Godffrey Osotsi (Mbunge Maalum, ANC).

Duru kutokana afisi ya Spika Muturi zilisema kuwa barua ya wabunge hao imepokewa na “itashughulikiwa kabla ya bunge kurejelea vikao vyake Jumanne”.

“Nadhani barua ya wabunge hao ni miongoni mwa barua nyingi ambazo afisi ya Spika itashughulikia kabla ya bunge kurejelea vikao vya Jumanne alasiri baada ya likizo fupi,” afisa mmoja, ambaye hakutaka kutajwa, aliambia ukumbi wa Jamvi.

Sheria za Bunge zinampa Spika wa Bunge kuidhinisha kuundwa kwa makundi mbalimbali ya wabunge baada ya kuridhinika na malengo yao. Kwa mfano, kando na makundi ya wabunge wanachama wa vyama mbalimbali vinavyowakilishwa bungeni, bunge la sasa la 12 lina makundi mengine.

Kundi la wabunge kutoka eneo la ukuzaji wa miwa kwa wingi linaloongozwa na Mbunge wa Muhoroni Onyango K’Oyoo, kundi la wabunge walemavu linaloongozwa na Seneta Maalum Isaac Mwaura, kundi la wabunge Waumini wa Kanisa Katoliki linaloongozwa na Mbunge wa Kiminini Chris Wamalwa, kati ya makundi mengine.

You can share this post!

JAMVI: Ruto aanza kuzima vyama hasimu kabla ya 2022

Mabunda ya Sh1m yapatikana kwa buti ya gari la kaunti...

adminleo