• Nairobi
  • Last Updated March 19th, 2024 10:15 AM
Raila apigia debe handisheki Uingereza

Raila apigia debe handisheki Uingereza

Na LEONARD ONYANGO

KIONGOZI wa ODM Raila Odinga ametumia ziara yake nchini Uingereza Jumatatu kupigia debe handisheki baina yake na Rais Uhuru Kenyatta.

Bw Odinga alisema kamati aliyobuni pamoja na Rais Kenyatta kukusanya maoni kutoka kwa wananchi kuhusu jinsi ya kumaliza uhasama wa kikabila nchini, maarufu BBI, itatoa mapendekezo yatakayosaidia kushughulikia dhuluma za kihistoria.

Alisema dhuluma za kihistoria zilizochochea vurugu za baada ya uchaguzi wa 2007, hazijapatiwa ufumbuzi kufikia sasa.

“Kofi Annan aliyetumwa kuja kunipatanisha na Rais Mwai Kibaki ili kumaliza vurugu alituhimiza kushughulikia dhuluma za kihistoria kama njia mojawapo ya kuepuka ghasia za uchaguzi katika siku za usoni.

‘Lakini kufikia sasa kuna mambo mengi ambayo hayajashughulikiwa na nina imani kamati ya BBI itatoa mapendekezo yatakayotusaidia kutafutia ufumbuzi dhuluma hizo,” akasema Bw Odinga aliyekuwa akihutubia wasomi katika taasisi ya Chatham House, Uingereza wakati wa kongamano la kukumbuka mafanikio ya mafanikio ya aliyekuwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Kimataifa (UN) Kofi Anna.

Wakati wa hotuba yake Bw Odinga aliibua hisia kali kuhusu mauaji ya kinyama yaliyotokea baada ya uchaguzi wa 2007 ambapo zaidi ya watu 1,300 waliangamia na wengine maelfu kupoteza makao.

“Nilikuwa naongoza katika uchaguzi kwa zaidi ya kura milioni 2 lakini ilipofika jioni televisheni ziliagizwa kutopeperusha matokeo.chantha

“Muda mfupi baadaye, tuliambiwa kwamba mpinzani wangu ameibuka mshindi. Hapo ndipo Wakenya waligeukiana na kuanza kuuana. Kwa mfano, watu waliokuwa wamejisiti kanisani waliteketezwa kwa moto,” akasema.

Bw Odinga alielezea juhudi za Annan aliyeaga dunia mnamo, Agosti 2018, katika kumpatanisha na rais Kibaki ambaye sasa amestaafu.

“Vurugu zilipozuka nilipokea simu kutoka kwa Waziri Mkuu wa Uingereza Gordon Brown aliyeniuliza ikiwa nilikuwa tayari kupatanishwa,” akasimulia.

Waziri Mkuu wa zamani alisema kuwa Annan alikuwa amekataliwa na upande wa Bw Kibaki.

“Ilibidi waziri mkuu wa Uingereza Bw Brown kuingilia kati ndiposa upande wa Rais Kibaki ukamkubali,” akasema Bw Odinga.

Waziri Mkuu wa zamani alisema, Rais Kibaki alishinikizwa kukubali kuunda serikali ya mseto iliyomaliza mapigano ya kikabila.

“Watu tuliokuwa tumeteua kutuwakilisha katika meza ya mazungumzo walikosa kuafikiana. Hapo ndipo Annan alisisitiza kwamba alitaka kukutana na mimi pamoja na Rais Kibaki.

“Tulikutana katika afisi ya rais (Jumba la Harambee) na hapo ndipo Kibaki alilazimishwa kukubali mambo ambayo kikosi chake kilikuwa kimekataa kuhusiana na majukumu ya waziri kuu,” akasema.

You can share this post!

ODM wapinga noti mpya

Ruto aahidi wakazi wa Mwiki shule mpya

adminleo