• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 11:42 PM
Uchafuzi wa maziwa ya Bonde la Ufa unavyoathiri utalii

Uchafuzi wa maziwa ya Bonde la Ufa unavyoathiri utalii

NA RICHARD MAOSI

SHIRIKA la Huduma za Wanyamapori nchini (KWS) mwaka 2018 ilitoa ripoti yenye utata iliyosema kuwa kiwango cha maji katika ziwa Nakuru kilikuwa kimepanda na kuzamisha baadhi ya mijengo.

Aidha waziri wa utalii Najib Balala miezi miwili iliyopita, alipozuru mbuga ya wanyama ya Ziwa Nakuru, alinukuliwa na vyombo vya habari akisema ziwa hilo lilikuwa limechakaa na kupoteza hadhi yake, kinyume na siku za mbeleni lilipokuwa na uhai.

Ingawa washikadau wamepinga mawazo haya, wanasayansi kwa upande mwingine wamefichua kuwa maziwa yanayopatikana katika Bonde la Ufa yanaangamia kutokana na uchafuzi wa mikondo ya maji inayoelekea kwenye mbuga za wanyama na maziwa.

Mwanasayansi Daktari Silas Simiyu anasema hili limechangiwa na ongezeko la idadi ya watu, wanaoishi kandokando ya maziwa makuu na mito inayobeba maji kuelekea mbuga ya wanyama ya Ziwa Nakuru.

Mbuga ya ziwa Nakuru ni kivutio cha The Big Five yaani simba, ndovu, vifaru, chui na duma. Isitoshe, ni mbuga ya kipekee Afrika Mashariki yenye vifaru weupe ambao wameadimika kutokana na uwindaji haramu.

Kumbukumbu za miaka miwili iliyopita, tangu watu tano waangamie katika ziwa Nakuru baada ya mkasa wa ndege kutumbukia ziwa Nakuru,hali ya uchafuzi haionekani kukoma kwa sababu ya maji taka yanayoingia ziwani.

Operesheni ya kutafuta miili ya walioaga dunia wakati huo, iliwaachia wazamiaji maradhi ya ngozi ambayo yamechukua muda mrefu kutibika,jambo hili likiakisi hali halisi ya kiwango cha uchafuzi katika ziwa Nakuru.

Shughuli ya uokozi ilichukua muda mrefu ikiaminika kuwa baadhi ya wazamiaji wa majini walihofia kuingia ndani ya ziwa, ili wasipate madhara ya ngozi.

Ndege za kijeshi ndizo zilitumika kutafuta mabaki ya manusura,juhudi za wazamiaji na meli zilipokosa kuzaa matunda wiki moja hatimaye.

Miaka kumi iliyopita maeneo yanayozunguka ziwa Nakuru hayakuwa na makazi rasmi ya watu, lakini watu walianza kujenga ndiposa mitaa kama vile Rhonda,Langalanga,Kivumbini na Madaraka ikatokea.

“Baadae mitaa karibu na Lake view ilianza kukua na kukaribia ziwa Nakuru,kwani serikali husika haikutilia maanani mpangilio wa ukuaji wa mji,”alieleza Simiyu.

Anasema kwa sababu ya miundo mbinu duni,serikali ya kaunti ya Nakuru ilishindwa kutekeleza wajibu wake wa kuzoa taka mitaani ipasavyo,huku mirundiko inayobaki ikisombwa na kuingia kwenye mitaro ya maji.

Kulingana naye ongezeko la idadi ya watu umesababisha ukataji miti kiholela na kusababisha mmomonyoko wa udongo unaochafua maji,”akasema Silas Simiyu.

Alieleza kuwa mchanganyiko wa kemikali kutoka kwenye viwanda,pamoja na maji chafu yanayotokea kwenye makazi ya watu ndio jinamizi linalokodolea macho ziwa Nakuru,ikionekana kuwa swala hili haliwezi kuepukika,

Changamoto nyingine inayokumba ziwa Nakuru ni ukaribu wake na ziwa Elementaita ambayo ina kiwango kikubwa cha maji ya chumvi.

Wakati wa joto jingi mvua hunyesha na kuongeza idadi ya chumvi ndani ya ziwa Nakuru hali ambayo ni hatari kwa maisha ya ndege na wanyama wanaotegemea ziwa Nakuru.

Hali hiyo hufanya samaki kuhamia pembeni mwa bahari na kutaga mayai ambayo hayawezi kuangua kwa wakati, kutokana na msukosuko wa maji.

Aidha Simiyu alieleza idadi ya flamingo wanaopatikana katika ziwa Nakuru imepungua kutoka milioni moja hadi famingo 200 tu,katika kipindi cha miaka mitano iliyopita.

“Ndege wengi walipoteza maisha na waliobaki kuhamia ziwa Bogoria katika juhudi za kutafuta mazingira tulivu,”akasema.

Mbali na makazi ya watu kulaumiwa kwa sababu ya kumwaga maji taka yanayoingia ziwani,wenye viwanda vya kutengeneza bidhaa za plastiki pia hawajasazwa kwa kukosa njia mbadala ya kutupa bidhaa zao.,

Mtaalam wa mazingira James Wakiba anasema ingawa UNESCO inatambua ziwa Nakuru kama eneo lenye chemichemi za maji na kivutio cha watalii,kiwango cha uchafuzi kimepoteza hadhi yake.

Katika matembezi yake kwenye ziwa Nakuru, aligundua kuna mito midogo 26 inayoingiza maji chafu ndani ya ziwa Nakuru sita yazo ikiwa ni kutoka kwenye viwanda.

Wakiba anaona kuwa kuna mito zaidi ambayo bado haijatambuliwa,lakini ameachia jukumu hilo KWS tawi la Nakuru, kupekua mazingira ya mbuga ya ziwa Nakuru kwa kina.

Anasema vianzo vya maji pia vipo hatarini ,ishara tosha kutokana na mmomonyoko wa udongo unaoteremsha mchanga kutoka kwenye milima ya Dundori kupitia eneo la Lanet na baadae ziwa Nakuru.

Mto Makalia,Nderit na Njoro ndiyo ilikuwa ikibeba maji safi hadi kwenye ziwa Nakuru lakini kufikia wakati wa upekuzi wa Taifa dijitali mito hiyo imekauka, labda msimu huu wa mvua ndio maji kidogo yanatiririka.

Kwa upande mwingine baadhi ya mito inayotoa maji safi kama vile Rongai, imefungiwa na wawekezaji wa kibinafsi wanaokuza maua.

Licha ya kutolewa marufuku kuhusu utumiaji wa mifuko ya plastiki,inaonekana kuwa idadi kubwa ya wanyama pori wanaoangamia katika ziwa Nakuru ni kwa sababu ya kutafuna mifuko ya plastiki inayoingia mbugani.

“Idadi kubwa ya wanyama wanaopoteza maisha ni pundamilia,swara,viboko,nyani na flamingo wanaopigania kunywa maji kwenye mito inayoingia ndani ya ziwa Nakuru,”akasema.

Mnamo 2016 Christine Mwinzi anasema takriban kilo 540 ya taka zilikuwa zikizolewa kila siku kutoka ndani ya Ziwa Nakuru.

2019 Taifa dijitali ilishuhudia usimamizi wa uzoaji taka kutoka ziwa Nakuru ambapo tani 6 zilitolewa kwa siku mbili.Usimamizi wa mbuga ya Nakuru uliajiri jumla ya vibarua 8 waliozoa taka na kupakia ndani ya malori.

” Wanyama wanaokaa ndani ya ziwa hunywa maji haya,hawana njia mbadala na ndio sababu huenda baadhi ya wanyama wamekuwa wakiugua na hata kufa mkurupuko wa maradhi yanapotokea,”akasema

Ziwa la pili lililopata pigo ni ziwa Naivasha kilomita chache kutoka Nakuru, ambalo hutegemewa kwa shughui za uvuvi na utalii kwa sababu ya maji yake safi.

Mbali na ziwa hili kuwa mojawapo wa maziwa makubwa katika bonde la ufa, washikadau wanasema huenda ziwa Naivasha lisiwe la manufaa yeyote kwa wakazi siku za mbeleni.

Mbali na uvuvi kupita kiasi baadhi ya watu wameanza kuweka makazi yao kando ya ziwa hilo kwa sababu ya uwekezaji katika ukulima na upungufu wa kipande cha ardhi.

Kwa kipindi cha miaka miwili kiwango cha samaki wanaovuliwa kutoka ziwa Naivasha kimepungua kutoka takriban tani 1,180 hadi tani 964.

Jambo hili lilifanya onyo kali kutolewa na serikali dhidi ya wavuvi wanaofanya shughuli zao wakati wa giza.

Mkurugenzi anayesimamia matumizi ya maji katika ziwa Naivasha Enock Kiminta anasema uvuvi haramu ndio chanzo cha ushukaji wa kiwango cha maji katika ziwa Naivasha.

Pili ongezeko la magugu maji ndani ya ziwa Naivasha ni jambo linalofanya samaki kukosa virutubisho na oksijeni.Wengi wa samaki hapa wamehamia maji ya kina kirefu wasipatikane kwa urahisi.

Mbwana Mbogo Kamau mtaalam wa mazingira anasema ongezeko la shuguli za binadamu kando ya mito pia ina mchango katika upatikanaji wa magugu katika ziwa Naivasha.

Kiminta anasema wizara ya mazingira kwa ushirikiano na NEMA zina wakati mgumu kukabili maji taka yanayoingia kwenye mito hususan msimu wa mvua.

Ziwa Nakuru limejaribu kuweka kichujio kabla ya maji kuingia kwenye mbuga lakini hali hii haijasaidia kitu kwa sababu mifuko ya plastiki inapoziba mikondo ya maji,mchanga hupenya na kuingia ndani ya mbuga..

You can share this post!

Chuma ki motoni kwa maafisa wa serikali walevi

WANDERI: Kisa cha Ng’ang’a ishara ya uasi wetu kwa Mungu

adminleo