• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 11:42 PM
AKILIMALI: Mbinu mpya ya kufuga samaki bila vidimbwi

AKILIMALI: Mbinu mpya ya kufuga samaki bila vidimbwi

Na RICHARD MAOSI

SAMAKI ni lishe miongoni mwa Wakenya wengi; aidha wafanyabiashara wamekuwa wakijipatia kipato kizuri kwa kufanya biashara ya samaki.

Mbali na samaki kutumika kutengeneza vitoweo mbalimbali pia huunda sampuli ya mafuta yanayotumika kama lishe kwa watoto.

Biashara ya kufuga samaki ina faida nzuri kwa sababu soko lake ni pana na wala sio la kuhangaika, muradi mkulima azalishe samaki wa kutosha.

Mradi huu unaweza kumsaidia mkulima akaanzisha kukuza aina nyingine ya mimea kama vile mawele ambayo hutoa lishe kwa samaki.

Akilimali ilifanya ufuatiliaji wa karibu kuhusu suala la ufugaji wa samaki kwa mtindo wa kisasa katika Shule ya Wavulana ya Jomo Kenyatta inayopatikana eneo la Bahati, Kaunti ya Nakuru na kujifunza jinsi wakulima wanaweza kufaidika.

Badala ya kutegemea vidimbwi na mabwawa kama ilivyofanywa na wafugaji siku za mbeleni, uvumbuzi mpya umefanya ufugaji wa samaki kuwa rahisi ikiaminika kuwa changamoto sio upatikanaji wa maji bali kufanya shughuli nzima ipasavyo.

Lilian Wangare, msimamizi wa shughuli za ufugaji wa samaki kwenye Shule ya Wavulana ya Jomo Kenyatta, Nakuru, anasema kwa ushirikiano na serikali ya kaunti shule yake iliona haja ya kuwekeza kwenye mradi huu.

Lengo la kubuni mradi wenyewe likiwa ni kuwapatia wanafunzi ujuzi wa kimaisha mbali na ule wa vitabuni ili waje kuwa watu wa kujitegemea maishani.

Ijapo mfumo wa samaki unahitaji maji yaliyotulia, mkulima anahitaji kuwa na samaki watatu mmoja awe wa kike na mwingine wa kiume. Haijalishi yule wa tatu ni wa kike au kiume, kwa sababu kazi yake ni kushinikiza uzalishaji.

Unayachukua mayai ya samaki kisha yakachanganywa na chembe chembe za uzalishaji kutoka kwa samaki wa kiume, ambao huchukua masaa 48 kuzalisha samaki wadogo (fingerlings).

Samaki wadogo huchukua siku tano kabla ya kulishwa vyakula vya kawaida vilivyochanganywa na unga na viungo muhimu vya majani.

“Ujuzi wa kufuga samaki niliupata mtandaoni, ndio maana nikaishawishi shule kukumbatia mtindo huu wa kisasa ili kuzalisha samaki kwa ajili ya kutoa mafunzo ya kitaalam kwa nwanafunzi na kutosheleza mahitaji ya shule,” akasema Wangare.

Ufugaji wa samaki kupitia mbinu za kisasa unaweza kusaidia kwenye utunzaji wa mali asili, pasipokuwa na uchafuzi wa maji wala mazingira wanamokulia viumbe hawa

Lilian anasema mkulima anaweza kufuga samaki kwenye kipande kidogo cha ardhi, ambayo kufikia sasa ni teknolojia ya kisasa ambayo ni nyepesi kujifunza.

Fursa hii ya kisasa inawalenga wakulima wadogo wanaopatikana mijini, wenye ari ya kuwekeza kwenye mradi wenyewe.

Huu ni ufugaji ambao tunaweza kusema unajumuisha makasha makubwa au matangi safi kuhifadhi samaki, hata wakulima wanaoishi kwenye maeneo kame wanaweza kufuga samaki.

Labda matanki haya yalikuwa yakitumia kuhifadhi maji lakini yakabadilishwa kufugia samaki, ambapo kila tanki hubeba takriban lita 4,000 ya maji.

Aidha, Lilian anasema mtu mmoja anatosha kuwafuga samaki muradi maji na hewa zinapenya kwenye muundo mzima wa mikondo ya maji na hewa safi.

Kinachohitajika ni kuhakikisha samaki wanapata lishe kwa wakati ufaao.

“Kila tanki linaweza kulinda samaki aina ya tilapia wakubwa wenye kilo zaidi ya 25,” Lilian aliongezea.

Mtaalam huyu anahimiza samaki wenyewe kulishwa na chakula kinachozalishwa humu nchini, aidha mkulima anaweza kuanza na samaki wadogo 200 kwenye tanki moja kisha akaendelea kuongeza matanki ya kufugia kadri wakati unavyozidi kusonga.

Matanki haya ya kisasa yasipungue kina cha mita mbili, bwawa la tanki lisiwe fupi kwenye kina kwani kuwa samaki wanahitaji maji ya kina kirefu ili waweze kukua kwa haraka.

Kilimo hiki kinaweza kumsaidia mkulima kuweka samaki wengi kwenye nafasi ndogo, ambapo maji yanayoingia na kutoka kupitia mikondo ya paipu hupishana.

Maji ya kufugia samaki lazima yawe baridi, na kwa sababu kaunti ya Nakuru ina maji chumvi chumvi haishauriwi kuwafuga ndani ya maji ya chumvi. Inatakiwa kiwango cha chumvi ndani ya maji kupimwa ili kubaini endapo samaki wanaweza kuishi salama bila kupata maradhi au kupigana na chumvi nyingi ya mwilini.

“Mkulima atumie eneo tulivu ambalo halina migogoro, lenye maji ya kutosha lakini pia atengeneze bwawa la kuhifadhi maji ili maji yasipungue wakati wa ufugaji,” akasema.

Aliongezea kuwa ikiwezekana mkulima anaweza kuwafuga samaki wadogo sawia na wale wakubwa ili kupunguza shinikizo la samaki kupungua baada ya kuwauza.

Lilian anaamini kuwa kabla ya mkulima kuwekeza kwenye mradi wa kufuga samaki waanze kwa kutumia elimu sahihi ya kitaalam.

Hata hivyo, anasema ikiwa mkulima atazingatia hatua zote zinazohitajika kwenye mradi wa kufuga samaki changamoto za ufugaji huwa zinapungua.

“Kwanza ninawahimiza wafugaji kuchunguza ubora wa maji, ikiwa mkulima atashindwa kubadilisha maji ya kufugia samaki wake kwa wakati ina maana kuwa samaki wataanza kuugua,” Lilian alisema.

Fangasi

Ugonjwa mkubwa unaosumbua samaki ni ule wa fangasi ambao hutokana na maji machafu, magamba huanza kumtokea samaki.

Ili mfugaji aweze kuanza ufugaji wa samaki ni muhimu kupata kibali cha matumizi ya maji kwa mfano kupata kibali kutoka kwa serikali kwa sababu samaki ni tofauti na wanyama wengine.

“Samaki anaishi kwenye maji anakula kwenye maji na anategemea kila kitu kwa mujibu wa maji yanayopatikana,” aliongezea.

Ili mkulima aweze kufuga samaki kibiashara mkulima anahitaji kuwa na mabwawa takriban sita ili uvunaji wa samaki usipunguze upatikanaji wa bidhaa hii muhimu sokoni.

“Mkulima akiwa na bwawa moja hatuwezi kusema anafuga samaki bali anajifundisha tu kufuga samaki,” alisema.

Aliongezea kuwa ikiwa maji na hewa ya majini ni chafu samaki hupata wasiwasi na wakajaribu kuhama na baadhi yao kufa.

Tiba ya haraka anayotakiwa kutoa mkulima anapopata baadhi ya samaki wameanza kupoteza maisha ni muhimu kusafisha bwawa kwa haraka.

Ikiwa mkulima si mzoefu pia anaweza kutafuta ushauri kutoka kwa mtaalam ili kujipunguzia hasara zinazoweza kuepukika.

You can share this post!

Uhuru atangaza marufuku ya chupa za plastiki nchini

AKILIMALI: Njugu, na udogo wake zilivyofaulu kumtimizia...

adminleo