• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 3:10 PM
JAMVI: Raila apania kujaribu bahati yake Ikulu kwa mara ya tano?

JAMVI: Raila apania kujaribu bahati yake Ikulu kwa mara ya tano?

Na BENSON MATHEKA

Kitendawili kuhusu iwapo kinara wa NASA Raila Odinga anapanga kugombea urais kwa mara ya tano kwenye uchaguzi mkuu wa 2022 kimezonga muungano huo wa upinzani.

Wadadisi wanasema  japo wandani wake wa kisiasa wanamshinikiza kujaribu bahati yake tena 2022 atakapokuwa na umri wa miaka 77, Bw Odinga anajikuna kichwa kwa sababu ya mkataba wa maelewano aliotia  sahihi na vinara wenza katika NASA kwamba hatagombea urais tena.

“Ukifuatilia kwa makini kinachoendelea katika chama cha ODM, utabaini kuna msukumo fulani unaolenga Bw Odinga kugombea 2022 na kukiuka mkataba wake na vinara wenzake.

Kitendawili ni iwapo atafaulu akigombea peke yake au iwapo ni kuunda muungano mpya wa kisiasa na uwezo wa muungano huo kumfaidi,” asema mwanasiasa wa NASA ambaye hakutaka tutaje jina lake kwa sababu ya jukumu analotekeleza katika muungano huo.

Kulingana na mwanasiasa huyo, Bw Odinga mwenyewe anajivuta kukubali mipango ya wandani wake wa kisiasa katika ODM ambao wanapanga mikakati ya chama chao kutema wenzao katika NASA.

“Kwa Bw Odinga, NASA haijafanikiwa katika jukumu lake kuu la kupigania haki katika uchaguzi ambayo vinara wenzake Kalonzo Musyoka, Musalia Mudavadi na Moses Wetangula wanakubali kwamba ni lazima iwapo uchaguzi wa 2022 utakuwa huru na haki.

Hata hivyo, shinikizo za wandani wake katika ODM wanaowachukulia vinara wenza kama waoga zinamfanya kujikuna kichwa na akiwaachia kuamua mambo, hatakuwa na jingine ila kuondoka NASA. Kitendawili ni kuwa ODM kikiondoka NASA kitaelekea wapi?”  anahoji mdadisi wa masuala ya kisiasa David Wafula.

 

Wasiwasi

Anasema kwamba kwa ODM kuagiza tathmini ya uchaguzi mkuu kuanzia 2007 na ushirikiano wake na vyama vingine vya kisiasa, vyama vingine tanzu vya Wiper, ANC na Ford Kenya vinafaa kuwa na wasiwasi. Bw Odinga mwenyewe amekuwa akasisitiza kuwa NASA ingali imara na kutaja tofauti zinazoshuhudiwa katika muungano huo kama za kawaida.

“Usisubiri Bw Odinga atangaze mara moja kujitenga na vinara wenzake, mwenye macho haambiwi tazama. Kuna moshi katika NASA na ni wakati tu kabla ya moto kulipuka,”asema.

Vyama tanzu vya NASA vinaonekana kutegua kitendawili hicho kwa kueleza jinsi Bw Odinga alivyowapiga chenga vinara wenza kuhudhuria hafla ya kumuapisha kama rais wa wananchi ambayo wanasiasa wa ODM wamekuwa wakitumia kumtaka kujitenga vinara hao kwa kutohudhuria.

Kulingana na Bw Barrack Muluka ambaye ni Katibu Mkuu wa ANC, Bw Odinga aliwachezea shere vinara wenza kuhudhuria hafla hiyo.

“Wanaowaita vinara wenza waoga hawaelewi kilichotendeka. Nilikuwepo na nilikuwa nikisubiri Raila awasiliane na vinara wenza walivyokuwa wamekubaliana lakini badala ya kufanya hivyo, alipenya na kuelekea Uhuru Park kula kiapo, “ Bw Muluka alisema.

Kulingana na Bw Francis Ikedi, mdadisi wa siasa madai ya Bw Muluka yanawiana na ya aliyekuwa seneta wa Kakamega Boni Khalwale ambaye wiki jana alimlaumu Bw Odinga kwa kuwasaliti vinara wenza katika NASA na kuhudhuria hafla ya kiapo.

 

Mara tano

“Ukifuatilia yaliyotokea katika NASA tangu wakati huo wa kiapo Januari 30, utagundua kuna mwelekeo mpya katika ODM huku vyama vya Wiper, ANC na Ford Kenya vikionekana kujitenga na maamuzi ya chama cha chungwa japo vinara wamekuwa wakitoa taarifa zinazosemekana kuwa za pamoja.

Kuna kitendawili ambacho kitateguliwa muda unaposonga kuelekea 2022 na kinahusu iwapo Raila ana azma ya kuingia katika vitabu vya historia kama mmoja wa watu waliogombea urais kwa zaidi ya mara tano, “ alisema Bw Ikedi.

Mbali na Bw Mudavadi, Bw Musyoka na Bw Wetangula kuapa kuwa kwenye debe 2022, manaibu wa Bw Odinga, Ali Hassan Joho na Wycliffe Oparanya ambao wamehudumu kipindi cha mwisho kama magavana wametangaza kuwania urais 2022.

Bw Ikedi anahoji kuwa huenda ODM ina njama za kumtenga Bw Musyoka kwenye uchaguzi mkuu wa 2022 ambaye chama chake cha Wiper kimekuwa kikimtaka Bw Odinga kumuunga mkono.

“Hii tathmini ya uchaguzi na ushirikiano na vyama vya kisiasa huenda inalenga Bw Musyoka ambaye wanasiasa wa ODM wanamchukulia kama kizingiti kikuu cha Bw Odinga kujaribu bahati tena 2022,” asema Bw Ikedi.

Kulingana na Bw Wafula hata ODM kikijiimarisha bila kushirikiana na vyama vingine hakiwezi kushinda uchaguzi na Bw Odinga anajua hivyo.

You can share this post!

TAHARIRI: Mazungumzo ni hatua nzuri ya kukuza utaifa

Magufuli apiga marufuku maandamano nchini mwake

adminleo