• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 11:33 AM
SHAIRI: Siasa nimekuacha, kwaheri tutaonana

SHAIRI: Siasa nimekuacha, kwaheri tutaonana

Ni tafakari ya babu, au kichwa cha gazeti?

Nayatafuta majibu, kwalo hili swali nyeti,

Kenya ina maajabu, ukifanya utafiti, 

Siasa nimekuacha, kwaheri tutaonana.

 

Majuzi mulisikika, mukifoka kwa hasira,

Sote tukaghadhibika, kuitaka haki bora,

Kumbe hadithi za paka, kukimbizana na chura,

Siasa nimekuacha, kwaheri tutaonana.

 

Tulowaamini ndio, watudandanya mchana,

Walivileta vilio, wenyewe tukatengana,

Leo hii hao hao, mikono wanapeana!,

Siasa nimekuacha, kwaheri tutaonana.

 

Wapiganapo fahali, nyasi huikosa kinga,

Ulipozuka muhali, tulicharazwa mapanga,

Amani ikawa ghali, sawa na bei ya unga,

Siasa nimekuacha, kwaheri tutaonana.

 

Mpendwa dada na kaka, keti chini tafakari,

masikio toa taka, wasije tena tughuri,

Sote tuipe talaka, siasa iso na Kheri,

Siasa nimekuacha, kwaheri tutaonana.

 

Na KHASIM AHMED, Mombasa

You can share this post!

DOMO KAYA: Muacheni Bahati na ya kwake, hayawahusu ndewe...

Kenya kuunda kikosi cha Cecafa U-17

adminleo