• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 6:50 PM
TAHARIRI: Mafuriko ya sasa yawe funzo kwa umma na serikali

TAHARIRI: Mafuriko ya sasa yawe funzo kwa umma na serikali

Na MHARIRI

MAAFA na uharibifu wa mali unaendelea kushuhudiwa katika maeneo mbalimbali kutokana na mvua kubwa inayoendelea kushuhudiwa humu nchini.

Kufikia Jumamosi, zaidi ya watu 20 walikuwa wameripotiwa kufariki kutokana na mafuriko katika kaunti tofauti tofauti.

Aidha, hiyo Jumamosi magari saba ya kifahari yaliharibiwa baada ya kuangukiwa na miti katika hoteli ya Serena.

Japo Gavana wa Nairobi Mike Sonko aliomba radhi kutokana na hali hiyo, kunahitajika juhudi zaidi ili watu wasiwe wakitatizika wala kupoteza maisha au mali yao wakati wa mvua.

Katika taarifa yake ya kuomba msamaha, Gavana Sonko alimlaumu mtangulizi wake Dkt Evans Kidero kwa matumizi mabaya ya Sh10 bilioni zilizotengwa kutengeneza mabomba ya njia za maji jijini.

Ni vyema Bw Sonko aelewe kuwa huu si wakati wa kulaumiana. Anapaswa kufanya kazi na fedha alizo nazo na kuachia taasisi husika kuchunguza ubadhirifu anaodai ulitekelezwa.

Serikali za kaunti na wakazi wa maeneo mengine ambako mvua inaendelea kunyesha, wanapaswa kuhifadhi maji ya mvua ili kuepuka upungufu wa maji baada ya misimu ya mvua kuisha.

Itakuwa aibu sana kwa wakazi kuanza kuhangaika wakitafuta maji, wakati mamilioni ya tani za maji zinaendelea kupotea wakati wa mvua.

Mbali na mafuriko, ni vyema wananchi wawe makini kwa sababu mvua inayoendelea kushuhudiwa inaweza kusababisha maradhi kutokana na uhaba wa maji safi na salama pamoja na kuwapo kwa mfumo hafifu wa majitaka hususan katika miji.

Ni vyema serikali itoe tahadhari kwa wadau wa sekta ya uvuvi, kilimo, mifugo, chakula na wanyamapori wafuate maagizo ya watabiri wa hali ya hewa. Kuwa na ufahamu wa mapema kutasaidia kujipanga kukabiliana na hali hiyo bila kukurupushwa.

Tahadhari hiyo pia inapaswa kutolewa kwa wachimbaji madini katika maeneo mbalimbali ya nchi.

Tunaamini kwamba pamoja na kuomba Serikali na taasisi zake kuchukua tahadhari, wananchi nao pia wanapaswa kuacha kufanya shughuli kwenye mikondo ya maji kama vile ujenzi.

Aidha, ni muhimu ikumbukwe kwamba Idara ya Hali ya Hewa imesema kuwa mvua itaendelea kunyesha na hivyo basi ni muhimu kwa wananchi pamoja na serikali kuhakikisha wameshirikiana ili kupunguza maafa ya watu na uharibifu wa mali.

You can share this post!

Je, ni nembo ya ‘usaliti’ kwa Raila kumkumbatia Uhuru?

JAMVI: Mkataba wa Raila na Uhuru wazalisha mayatima wa...

adminleo