• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 2:07 PM
Atakayefichua mwanamume anayewatapeli wabunge kutuzwa Sh20,000

Atakayefichua mwanamume anayewatapeli wabunge kutuzwa Sh20,000

Na STELLA CHERONO

MKURUGENZI Mkuu wa Ujasusi(DCI) George Kinoti ametoa Sh20,000 kwa yeyote aliye na habari kuhusu aliko mwanamume aliyetuhumiwa kuwalaghai wabunge.

Benson Wazir Chacha Masubo anahitajika kwa kudaiwa kupata pesa kwa kujifanya, na kwa kutumia vitisho katika intaneti.

Bw Masubo alishutumiwa kwa kuwalaghai wabunge kwa kujifanya kuwa Mwakilishi wa Kike wa Kaunti ya Murang’a Bi Sabina Chege.

Alhamisi, Bw Kinoti aliambia Kamati ya Bunge ya Usalama kwamba baada ya uchunguzi wa kina, walibaini kuwa kulikuwa na uhusiano maalum kati ya mshukiwa na walalamishi.

“Tumefanya uchunguzi wa kina kuhusiana na suala hili na tumetamatisha kuwa kuna uhusiano maalum kati ya walalamishi na mshukiwa ambao na sihisi vyema kujadili suala hilo hadharani,” alisema Bw Kinoti.

Ni kutokana na kauli hiyo ambapo wanahabari walishauriwa kuondoka nje ili Bw Kinoti aweze kueleza zaidi.

Miongoni mwa wa waliolaghaiwa na mwanamume huyo ni Spika wa Bunge la Kitaifa Justin Muturi ambaye alimtumia Sh30,000, aliyekuwa mbunge wa Gem MP Jakoyo Midiwo (Sh20,000), na mawaziri Eugene Wamalwa (Ugatuzi), Peter Munya (Jumuia ya Afrika Mashariki), Margaret Kobia (Huduma ya Umma) na Sicily Kariuki (Afya).

Mwezi Februari, mshukiwa aliweka mtandaoni picha zake alizopigwa na aliyekuwa Mwakilishi wa Kike wa Bomet Cecilia Ng’etich na kuonekana kusingizia uhusiano kati yao.

Picha hizo zilisambazwa sana katika mitandao ya kijamii. Wakati wa mahojiano, Bi Ng’etich alisema mwanamume huyo alikuwa laghai na alikuwa akitaka Sh2 milioni kwa kumtishia.

Aliwataka maafisa wa polisi kumchunguza, na kuongeza kuwa alikuwa mtu wa kutiliwa shaka.

 

You can share this post!

Msituhusishe kwa mzozo wenu, Mutula awaambia vinara wa NASA

27 wakamatwa kufuatia ghasia Kakamega

adminleo