• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
Mahakama yasitisha uchaguzi wa awamu ya pili Sierra Leone

Mahakama yasitisha uchaguzi wa awamu ya pili Sierra Leone

FREE TOWN, SIERRA LEONE

MAHAKAMA Kuu ya Sierra Leone, Jumamosi ilitoa agizo la kusimamisha awamu ya pili ya uchaguzi wa urais hadi iamue kesi iliyowasilishwa na wakili wa chama tawala.

Taharuki imetanda kabla ya uchaguzi huo huku kampeni zikikumbwa na ghasia. Wanasiasa na wafuasi pia wamekuwa wakitishwa na chuki za kikabila zimeongeka kufuatia kura hiyo.

Agizo la mahakama linazuia Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), kuandaa uchaguzi huo hadi kesi isikilizwe na kuamuliwa. Linazuia tume kuandaa uchaguzi ikiwa ni pamoja na kusambaza karatasi na vifaa vya kura.

Mahakama iliahirisha kesi hadi Jumatatu kupatia tume muda wa kuwasilisha swali katika Mahakama ya Juu na baadaye itaketi kushughulikia kesi hiyo.

“Kwa kuzingatia kuwa kesi hii itarudi kortini Jumatatu Machi 26, tume itasitisha kwa muda maandalizi ya awamu ya pili ya kura ya urais,” tume ilisema kwenye taarifa.

Wakili Ibrahim Sorie Koroma, mwanachama wa chama tawala cha All Peoples’ Congress (APC), alisema kwenye kesi yake kwamba madai ya wizi wa kura yanafaa kuchunguzwa kabla ya uchaguzi kuandaliwa.

Waangalizi wa kimataifa na wa Sierra Leone walisema kwamba uchaguzi wa raundi ya kwanza ulikuwa huru na wa haki.

Mgombea urais wa APC Samura Kamara, alikuwa wa pili nyuma ya Julius Maada Bio wa chama cha upinzani cha Sierra Leone People Party (SLPP) kwenye raundi ya kwanza Machi 7 lakini hakuna aliyepata asilimia 55 ya kura kutangazwa mshindi.

Kamara aliambia AFP kwamba alitarajia mahakama zitahakikisha NEC itaondoa makosa yaliyoshuhudiwa Machi 7 kabla ya awamu ya pili ya uchaguzi.

Tayari, upinzani unadai kwamba polisi wamekuwa wakitumiwa na APC baada ya kuingia ofisi za NEC na kuwahoji wafanyakazi wiki jana. Upinzani pia unasema kwamba chama tawala kinatumia mahakama kuchelewesha uchaguzi.

“Tunachukulia haya yanayoitwa maagizo ya muda ya mahakama kama njama za Rais Ernest Koroma za kutaka kuongeza muda wake mamlakani kinyume cha sheria,” SLPP ilisema kwenye taarifa Jumamosi.

“Dalili zote zinaonyesha kwamba Koroma hatapeana mamlaka bila shinikizo za jamii ya kimataifa kwa sababu ameingilia asasi zote za serikali ikiwa ni pamoja na Mahakama,” ilisema taarifa hiyo.

Polisi walivamia boma la mgombeaji wa SLPP, Bio baada ya raundi ya kwanza ya uchaguzi lakini hawakumkamata.

Mkuu wa Ofisi ya Umoja wa Mataifa Magharibi mwa Afrika (UNOWAS), Mohamed Ibn Chambas, Alhamisi alisema tume ya uchaguzi inakabiliwa na changamoto teke katika utekelezaji wa majukumu yake.

Alitaka pande zote kutoingilia au kutatiza uhuru na uadilifu wa NEC.

 

You can share this post!

Kidume mkono gamu amhepa kisura wake dukani

Kizaazaa Miguna kuzuiwa JKIA akitoka Canada

adminleo