• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
Kila mwanahisa wa Eveready apokea Sh1 kwa kila hisa

Kila mwanahisa wa Eveready apokea Sh1 kwa kila hisa

Na PETER MBURU

WENYEHISA wa kampuni ya kuuza betri ya Eveready East Africa PLC walipokea Sh1 kwa kila hisa, kutokana na pesa za mauzo ya shamba la ukubwa wa ekari 18.5 ililokuwa ikimiliki kampuni hiyo eneo ghali mjini Nakuru.

Baada ya kuuza shamba hilo kwa Sh1.14bilioni, kampuni hiyo ilitumia Sh525 milioni kulipa madeni yaliyokuwa yakiisakama baada ya kutengana na kampuni ya Energizer Holdings, na kubakisha Sh210milioni kama faida kwa wenye hisa.

Habari hizi zilitolewa wakati wa mkutano wa mwaka wa kampuni hiyo (AGM) ulioandaliwa katika hoteli ya Merica mjini Nakuru Jumatano.

“Lakini tuna furaha kufahamu kuwa sasa hatuna deni na mtu kwani tulilipa madeni yote na hata kubakisha Sh150 milioni za kupanua biashara,” akasema mkurugenzi mkuu wa kampuni hiyo Jackson Mutua.

Bodi ya wakurugenzi aidha ilisema kampuni hiyo ilikuwa ikijikokota kushika mizizi sokoni, kwani licha ya kuwepo kwa zaidi ya miaka 50, nyingi za biodhaa zao zilizinduliwa kwa kipindi cha mwaka uliopita baada ya kutofautiana na kutengana na kampuni ya Energizer Holdings.

Bodi hiyo ilisema kampuni hiyo iliingiza hasara ya zaidi ya Sh300 milioni kipindi cha mwaka uliopita wa pesa, kutokana na gharama nyingi za kubadili uongozi, kugharamia kesi nyingi kortini na hali ya biashara kuvurugwa na uchaguzi wenye utata.

“Sisi ni biashara ambayo bado ipo utotoni kwani tumeingiza bidhaa nyingi sokoni mwaka uliopita, lakini bado tuna ubora wa betrii na wateja wengi wanatuamini,” akasema Bw Mutua.

Kampuni hiyo aidha ilitangaza mpango wa kuondoa betriizijulikanazo kama D-sized sokoni, kutokana na ugumu wake wa kutupwa zinapoharibika na badala yake kuingiza betri ndogo.

Bodi ya uongozi ilitilia hofu deni wanalodai kampuni ya Nakumatt kuwa huenda likapotelea, baada ya Nakumatt kuanguka kwa viwango vikubwa na kutoonyesha dalili za kulipa.

Mwenyekiti wao Bi Lucy Waithaka, hata hivyo, alitetea kampuni hiyo kuwa sasa baada ya kujitenga na Energizer Holdings walikuwa na nafasi kufanya vyema sokoni.

“Hii ni kwa kuwa sasa sisi ndio waamuzi wa biashara yetu kinyume na mbeleni ambapo maamuzi yalifanywa na watu wasiofahamu changamoto na mahitaji ya sokoni,” akasema Bi Waithaka.

 

You can share this post!

Wakenya sasa kufanya biashara popote Afrika bila vikwazo

GWIJI WA WIKI: Timothy Kinoti M’Ngaruthi

adminleo