• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
Ni aibu kwa serikali kumnyanyasa raia aliyezaliwa Kenya – Mashirika

Ni aibu kwa serikali kumnyanyasa raia aliyezaliwa Kenya – Mashirika

Na BENSON MATHEKA
MASHIRIKA ya kutetea haki za binadamu humu nchini na ya kimataifa,  yameshutumu serikali ya Kenya kwa kumnyanyasa wakili Miguna Miguna na kumnyima haki yake ya uraia wa kuzaliwa.

Serikali ilimzuia Miguna kuingia Kenya tangu Jumatatu hadi Jumatano ilipomfurusha nchini kwa nguvu kwa mara ya pili hadi Dubai ikidai hakuwa na paspoti.

Juhudi za kumtaka kuomba uraia wa Kenya ziligonga mwamba alipotaka arejeshewe paspoti yake ya Kenya iliyotwaliwa na serikali na kuharibiwa alipokamatwa na kufurushwa Kenya mara ya kwanza Februari.

Alhamisi, Tume ya Taifa ya Haki za Binadamu (KNHRC) na shirika la Human Right Watch yalisema kwenye taarifa tofauti kwamba Bw Miguna anafaa kuruhusiwa kuingia na kuishi Kenya.

Mwenyekiti wa KNHRC, Kagwiria Mbogori alisema Bw Miguna hawezi kupokonywa uraia wake wa Kenya kwa sababu ni wa kuzaliwa. “Bw Miguna ana haki ya kupatiwa paspoti ya Kenya.

Serikali inafaa kufuata ibara ya 16 ya katiba ambayo inafafanua wazi kuwa mtu hawezi kupokonywa uraia wa kuzaliwa,”alisema Bi Mbogori.

Akihutubia wanahabari jijini Nairobi, Bi Mbogori alilaumu maafisa wa idara ya uhamiaji kwa kumhangaisha Bw Miguna kwa kumzuia kuingia Kenya mahakama ilivyoagiza.

“Bw Miguna hakunyanyaswa alipotoka kwa ndege na kupitia eneo la abiria isipokuwa alipofika kwa maafisa wa uhamiaji ubishi ulipoanza. Bw Miguna aliwataka wampe paspoti yake ili wapige muhuri,” alisema.

Bi Mbogori alisema kulingana na katiba ya Kenya, raia kwa kuzaliwa hawezi kupoteza uraia wake akipata uraia wa nchi nyingine na kwamba akipata uraia wa nchi nyingine, anabaki kuwa raia wa Kenya.

Kulingana KNHRC, mtu hawezi kupokonywa uraia bila kupatiwa nafasi ya kujitetea ikiwa ni pamoja na kutafuta haki mahakamani.

“Kabla ya mtu kupokonywa uraia anafaa kufahamishwa sababu za na kupatiwa nafasi ya kujibu ikiwa ni pamoja na haki ya kujitetea mahakamani,” alisema Bi Mbogori.

Aidha, alisema haki ya uraia imelindwa na sheria za kimataifa kuhusu haki za binadamu na kwamba hakuna mtu anayefaa kupokonywa uraia kiholela.

KNHRC ilifuatilia hatua za kurejea nchini kwa Miguna ilivyoagizwa na mahakama. Tume ilikuwa imewasiliana na idara za serikali zinazohusika na kuhakikishiwa kuwa Bw Miguna angeruhusiwa kurejea nchini jambo ambalo halikutendeka.

Kwenye taarifa, Human Rights Watch lilisema kwamba  Bw  Miguna Miguna anafaa kuruhusiwa kuingia na kutoka Kenya bila kutatizwa.

“Chini ya katiba ya Kenya iliyopitishwa  2010,  Kenya  haiwezi kumpokonya yeyote aliyepata uraia kwa kuzaliwa nchini humo,” HRW lilisema kwenye taarifa.

You can share this post!

LSK yakerwa na mazoea ya maafisa wa serikali kudharau sheria

MCK yataka visa vya wanahabari kuvamiwa vichunguzwe

adminleo